Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutabiri Wakati Wetu Ujao

Kutabiri Wakati Wetu Ujao

Kutabiri Wakati Wetu Ujao

ALIPOKUWA akizungumzia wakati ujao wa wanadamu na dunia, mtume Petro aliandika hivi: “Kulingana na ahadi yake [Mungu] tunangojea mbingu mpya na dunia mpya, na humo uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13) Mwanzoni ahadi ya “mbingu mpya na dunia mpya” ilitolewa kupitia nabii Isaya. (Isaya 65:17; 66:22) Kwa kunukuu unabii huo, Petro alionyesha kwamba katika siku zake haukuwa umetimizwa kikamili.

Baadaye, mnamo 96 W.K., Ufunuo ambao mtume Yohana alipewa ulihusianisha ‘dunia hiyo mpya’ na baraka za Ufalme wa Mungu. (Ufunuo 21:1-4) Maneno ya Yesu na pia ya mtume Paulo kuhusu hali za ulimwengu kabla tu ya kuja kwa Ufalme wa Mungu yanatimia sasa. Hivyo, tunaweza kutarajia kwamba Ufalme huo utaleta ulimwengu mpya. Ulimwengu huo utakuwa na hali gani? Kitabu cha Biblia cha Isaya kinatuambia.

Baraka Katika Ulimwengu Mpya

Amani Ulimwenguni Pote na Umoja wa Ibada. “Watafua panga zao ziwe majembe na mikuki yao iwe miundu. Taifa halitainua upanga juu ya taifa, wala hawatajifunza vita tena.”—Isaya 2:2-4.

Amani Kati ya Wanadamu na Wanyama. “Mbwa-mwitu kwa kweli atakaa pamoja na mwana-kondoo kwa muda fulani, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi, na ndama na mwana-simba mwenye manyoya shingoni na mnyama aliyelishwa vizuri wote pamoja; na mvulana mdogo atakuwa kiongozi juu yao. Na ng’ombe na dubu watakula pamoja; watoto wao watalala pamoja. Na hata simba atakula majani kama ng’ombe. . . . Hawatasababisha madhara yoyote wala kusababisha uharibifu wowote katika mlima wangu wote mtakatifu; kwa maana dunia hakika itajawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.”—Isaya 11:6-9.

Chakula Tele kwa Wote. “Yehova wa majeshi hakika atavifanyia vikundi vyote vya watu, katika mlima huu, karamu ya vyakula vinono vilivyotiwa mafuta, karamu ya divai iliyowekwa kwenye machicha, ya vyakula vinono vilivyotiwa mafuta vilivyojazwa urojorojo, ya divai iliyowekwa kwenye machicha, iliyochujwa.”—Isaya 25:6.

Hakuna Kifo Tena. “Yeye [Mungu] kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote. Na shutuma ya watu wake ataiondoa katika dunia yote, kwa maana Yehova mwenyewe amesema hayo.”—Isaya 25:8.

Wafu Wafufuliwa. “Wafu wako wataishi tena, maiti zao zitafufuka. Amkeni, shangilieni, enyi mnaokaa katika mavumbi. . . . Nchi itawarudishia uzima wale waliokufa.”—Isaya 26:19, Verbum Bible.

Masihi Ni Hakimu Mwadilifu. “Hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu, wala kukaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake. Naye atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, atakaripia kwa unyoofu kwa ajili ya watu wapole wa dunia.”—Isaya 11:3, 4.

Vipofu na Viziwi Waponywa. “Macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa.”—Isaya 35:5.

Eneo Kame Latokeza Mazao. “Nyika na nchi isiyo na maji itafurahi; na nchi tambarare ya jangwani itakuwa na shangwe na kuchanua maua kama zafarani. Itachanua maua bila shaka, nayo itashangilia kwa shangwe na kwa kilio cha furaha.”—Isaya 35:1, 2.

Dunia Mpya. “Ninaumba mbingu mpya [serikali mpya ya kimbingu] na dunia mpya [jamii mpya ya wanadamu waadilifu]; na mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, na muwe na shangwe milele katika hivi ninavyoumba. . . . Hakika wao [wakaaji wa ulimwengu mpya ulioahidiwa na Mungu] watajenga nyumba na kukaa ndani yake; na hakika wao watapanda mashamba ya mizabibu na kula matunda yake. Hawatajenga na mtu mwingine akae ndani yake; hawatapanda na mtu mwingine ale. Kwa maana siku za watu wangu zitakuwa kama siku za mti; na watu wangu waliochaguliwa wataitumia kazi ya mikono yao wenyewe kikamilifu. Hawatafanya kazi ya bure, wala hawatazaa kwa ajili ya kupata usumbufu; kwa sababu wao ni uzao wa watu wa Yehova waliobarikiwa, na wazao wao pamoja nao. Na kwa kweli itakuwa kwamba kabla hawajaita mimi mwenyewe nitajibu; wakiwa bado wanasema, mimi nitasikia.” “‘Kama vile mbingu mpya na dunia mpya ninazozifanya zinavyosimama mbele zangu,’ asema Yehova, ‘ndivyo uzao wenu na jina lenu litakavyoendelea kusimama.’”—Isaya 65:17-25; 66:22.

Kutabiri Kuhusu Wakati Ujao Mzuri Ajabu

Mbali na Isaya, kuna vitabu vingine vya Biblia vinavyotabiri kuhusu baraka za wakati ujao. Biblia imejaa unabii unaofafanua mambo mazuri ambayo Mungu atatimiza kupitia Ufalme wake ulio mikononi mwa Kristo. * Je, ungependa kuishi chini ya hali hizo za kiparadiso? Unaweza! Jichunguzie kile ambacho Biblia inafundisha kuhusu makusudi mazuri ya Mungu kwa ajili ya wakati ujao na ujifunze jinsi unavyoweza kuwepo wakati huo. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Kwa habari zaidi kuhusu Ufalme wa Mungu na yale ambayo utatimiza, ona ukurasa wa 76-85 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Wanadamu watakuwa na amani kati yao na pamoja na wanyama

[Picha katika ukurasa wa 9]

Wafu wataishi tena

[Picha katika ukurasa wa 10]

Dunia yote itakuwa paradiso