Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Machozi Katika Kiriba

Machozi Katika Kiriba

Machozi Katika Kiriba

KIJANA huyo alikuwa mkimbizi. Akiwa amelemewa na kufadhaika, huku macho yake yakilengwa-lengwa na machozi, alimwomba Mungu wake, Yehova fadhili na huruma akimsihi hivi: “Uyaweke machozi yangu katika kiriba chako.” (Zaburi 56:8) Mtu huyo alikuwa Daudi, ambaye baadaye angekuwa mfalme wa Israeli. Lakini kiriba alichorejelea kilikuwa nini, na Mungu anaweza kuweka machozi yetu katika kiriba jinsi gani?

Daudi alijua kiriba ni nini. Kilikuwa chombo kilichotumiwa kuweka maji, mafuta, divai, au hata siagi. Wahama-hamaji wa jangwa la Sahara, kama vile Watuaregi, wangali wanatumia viriba vilivyotengenezwa kwa ngozi ya mbuzi au kondoo. Viriba kama hivyo vinaweza kubeba maji mengi ikitegemea ukubwa wa mnyama. Viriba vinajulikana kwa kuweka maji yakiwa baridi, hata kukiwa na joto kali sana jangwani. Zamani, kwa kawaida vilibebwa na punda au ngamia. Siku hizi, unaweza kuona vikiwa vimefungwa kwenye magari yanayotumiwa jangwani!

Maneno yenye kugusa moyo ya Daudi kuhusu kiriba yanaweza kuwa muhimu kwetu pia. Jinsi gani? Biblia inaeleza kwamba Shetani anaudhibiti ulimwengu huu na ana “hasira kali” katika siku zetu. Ndiyo sababu dunia ina ole nyingi. (Ufunuo 12:12) Kwa sababu hiyo, kuna wengi ambao kama Daudi, wanateseka kihisia, kiakili, au kimwili, hasa wale wanaojaribu kumpendeza Mungu. Je, unakabili hali kama hizo? Kwa ujasiri, hata ‘wanapolia,’ watu hao waaminifu hawaachi kujitahidi kuishi maisha ya utimilifu. (Zaburi 126:6) Wanaweza kuwa na hakika kwamba Baba yao wa mbinguni haoni tu majaribu wanayokabili bali pia anaona jinsi yanavyowaathiri kihisia. Anaelewa kabisa uchungu unaowapata watumishi wake, na anakumbuka kwa huruma machozi na kuteseka kwao, kana kwamba ameyahifadhi katika kiriba.