Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Matukio Yaliyotabiriwa Kuhusu Siku Zetu

Matukio Yaliyotabiriwa Kuhusu Siku Zetu

Matukio Yaliyotabiriwa Kuhusu Siku Zetu

BIBLIA inatabiri kwamba Ufalme wa Mungu utaleta amani na furaha ya kudumu duniani. (Danieli 2:44) Katika sala ya Baba Yetu, au Sala ya Bwana, Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Katika unabii wake unaojulikana sana aliowaambia wanafunzi wake kwenye Mlima wa Mizeituni, Yesu alitabiri matukio na hali hususa ambazo zingekuwapo kabla tu ya Ufalme huo kuja. Matukio hayo yangekuwa ishara ambayo ingeonekana wazi kwa watazamaji wenye mioyo minyoofu. Ni sehemu gani za ishara hiyo zinazofuata ambazo umejionea mwenyewe?

Vita vya Kimataifa. Yesu alitabiri: “Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme.” (Mathayo 24:7) Kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu mnamo 1914, hakukuwa na vita vya kimataifa. Lakini Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilihusisha sehemu kubwa ya ulimwengu na pia vikachochea kutengenezwa kwa silaha hatari zaidi kuliko zile ambazo mwanadamu alikuwa amewahi kutengeneza. Kwa mfano, ndege zilizokuwa zimetoka tu kuvumbuliwa zilitumiwa kuangushia raia mabomu. Utengenezaji wa silaha kwa kiwango kikubwa uliongeza idadi ya watu waliouawa kufikia viwango ambavyo havikuwahi kuwaziwa, kwani karibu nusu ya askari milioni 65 waliopigana walikufa au wakajeruhiwa. Hata hivyo, karne ya 20 ilivyozidi kusonga, ndivyo mauaji yalivyoongezeka. Kulingana na mwanahistoria mmoja, idadi ya wanajeshi na raia waliouawa katika Vita vya Pili vya Ulimwengu “haitawahi kujulikana.” Na bado vita vinaendelea.

Njaa Ulimwenguni Pote. “Kutakuwa na upungufu wa chakula,” Yesu alitabiri. (Mathayo 24:7) Mnamo 2005, gazeti fulani (Science) lilisema: “Watu milioni 854 ulimwenguni (asilimia 14 hivi ya watu ulimwenguni) hawana chakula cha kutosha.” Katika mwaka wa 2007, shirika la Umoja wa Mataifa liliripoti kwamba nchi 33 hazina chakula cha kutosha kuwalisha raia wake. Hilo linawezekana jinsi gani huku kiwango cha nafaka kikiongezeka ulimwenguni? Jambo moja ni kwamba ardhi na nafaka ambayo ingetumiwa kuwalisha watu, inatumiwa kutokeza mafuta kwa ajili ya magari. “Kiasi cha mafuta kinachohitajika kujaza gari kubwa linaloendeshwa kwa magurudumu manne kinalingana na nafaka inayotosha kumlisha mtu mmoja kwa mwaka mzima,” linaripoti gazeti moja la Afrika Kusini (The Witness). Pia, katika nchi zilizoendelea, bei ya chakula inayozidi kuongezeka inawafanya wengi wachague kulipia mahitaji muhimu kama vile dawa badala ya kula chakula cha jioni.

Matetemeko Makubwa ya Nchi. Yesu alisema: “Kutakuwa na matetemeko makubwa ya nchi.” (Luka 21:11) Ikiwa unaona kwamba siku hizi watu wengi zaidi kuliko wakati mwingine wowote wanaathiriwa na matetemeko ya nchi, hujakosea. Mtaalamu Mhindi wa matetemeko ya nchi, R. K. Chadha, alisema hivi mnamo 2007: “Kwa ghafula, tunaona ongezeko la utendaji chini ya ardhi unaosababisha matetemeko ulimwenguni pote. . . . Hakuna mtu anayejua sababu.” Zaidi ya hayo, kuongezeka kwa watu katika maeneo yanayokumbwa na matetemeko ya nchi kumeongeza idadi ya wale wanaoathiriwa na misiba hiyo. Tetemeko lililokumba Bahari ya Hindi mnamo 2004 na tsunami iliyofuata ilifanya mwaka huo kuwa “na matetemeko hatari zaidi kwa miaka 500 hivi” na “wa pili hatari zaidi kuwahi kurekodiwa,” kulingana na Shirika la Marekani la Uchunguzi wa Jiolojia.

Magonjwa Yasiyoweza Kuzuiwa. “Kutakuwa na tauni,” Yesu alitabiri. (Luka 21:11) Ulimwenguni pote, magonjwa ya zamani na mapya yanawapata watu wengi zaidi, na ni vigumu kuyatibu. Kwa mfano, muda wa kufikia miradi ya kimataifa ya kumaliza malaria umehitaji kusogezwa mbele mara kadhaa kwa kuwa ugonjwa huo unaendelea kuwashinda wanadamu. Kwa kuongezea, mamilioni wanakufa kwa sababu ya magonjwa ya zamani, kutia ndani kifua kikuu (TB), UKIMWI, na magonjwa mengine mapya. “Asilimia 33 hivi ya watu ulimwenguni wameambukizwa TB,” linaripoti Shirika la Afya Ulimwenguni. Shirika hilo pia linasema kwamba virusi vya UKIMWI vinachangia kuongezeka kwa TB katika nchi nyingi. Kila sekunde, kuna mtu anayeambukizwa TB, na ugonjwa huo unazidi kushinda madawa nguvu. Mnamo 2007 mgonjwa huko Ulaya aliambukizwa TB ambayo “ilishinda madawa yote tuliyo nayo,” linaripoti gazeti moja (New Scientist).

Kuharibika kwa Maadili na Jamii. “Kwa sababu ya kuongezeka kwa uasi-sheria upendo wa walio wengi zaidi utapoa,” akasema Yesu. (Mathayo 24:12) Zaidi ya kile ambacho Yesu alitabiri, mtume Paulo alielekeza kwenye wakati ambapo viwango vya kijamii na vya maadili vingeporomoka. Alifafanua “siku za mwisho” zilizo ngumu ambazo zingekuja kabla tu ya Ufalme wa Mungu kukomesha mfumo huu wa ulimwengu. “Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu, wasio na upendo wa asili, wasiotaka makubaliano yoyote, wachongezi, wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, wasaliti, wenye vichwa vigumu, wenye kujivuna kwa kiburi, wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu wakiwa na namna ya ujitoaji-kimungu lakini wakizikana nguvu zake.” (2 Timotheo 3:1-5) Je, umeona kwamba watu wanaonyesha sifa hizo mbaya leo zaidi ya walivyofanya zamani?

Yesu na Paulo hawakuorodhesha mambo yote ya kihistoria, kijamii, na kisiasa yanayosababisha hali hizo zote ulimwenguni. Hata hivyo, unabii wao ulieleza kwa usahihi matukio na mitazamo tunayoona leo. Namna gani wakati ujao? Unabii wa Isaya uliotabiri kwa usahihi kuja kwa Masihi pia unaeleza mabadiliko yenye faida ambayo Ufalme wa Mungu utaleta duniani. Acheni tuchunguze mambo hayo katika habari inayofuata.

[Picha katika ukurasa wa 6]

“Taifa litasimama kupigana na taifa”

[Picha katika ukurasa wa 7]

“Kutakuwa na tauni”

[Hisani]

© WHO/P. Virot