Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Anayeweza Kujua Wakati Ujao?

Ni Nani Anayeweza Kujua Wakati Ujao?

Ni Nani Anayeweza Kujua Wakati Ujao?

“Mimi ni Mungu . . . , Yeye anayetangaza tangu mwanzo ule mwisho, na kutoka zamani za kale mambo ambayo hayajafanywa.”—Isaya 46:9, 10.

KATIKA nyakati hizi zenye msukosuko, wataalamu wa masuala ya kisiasa, kiuchumi, na kijamii wanachunguza historia na mielekeo ya kisasa wakijaribu kutabiri wakati ujao. Wengine wanaotaka sana kujua hali yao ya wakati ujao wanachunguza nyota au kuwasiliana na pepo. Mara nyingi, watu kama hao wanakatishwa tamaa. Je, ni vigumu kujua kile ambacho kitatokea katika ulimwengu huu, kitakachotupata sisi, na familia zetu? Je, kuna mtu yeyote anayeweza kutabiri kuhusu wakati ujao?

Katika maneno aliyomwambia nabii Isaya, ambayo yamenukuliwa hapo juu, Mungu Mweza-Yote, Yehova, alieleza kuhusu uwezo wake wa kutabiri wakati ujao. Kupitia Isaya, Mungu alitabiri kuhusu kuachiliwa kwa Waisraeli wa kale kutoka utumwani Babiloni na kurudi kwao ili wajenge tena Yerusalemu na hekalu lake. Unabii huo ulikuwa sahihi kadiri gani? Miaka 200 hivi mapema, Isaya alitaja kwa usahihi jina la Koreshi ambaye angeshinda Babiloni. Isitoshe, Isaya alitaja kwa usahihi mbinu ya Koreshi, yaani, kugeuza mkondo wa Mto Efrati ambao ulilinda jiji hilo. Hata alitabiri kwamba Koreshi angepata ile milango mikubwa yenye pande mbili ya jiji hilo ikiwa imeachwa wazi, na hivyo kumfanya ashinde kwa urahisi.—Isaya 44:24–45:7.

Akilinganishwa na Mungu, mwanadamu hana uwezo wa kutabiri wakati ujao. “Usijisifu kwa sababu ya siku inayofuata,” akaandika Mfalme Sulemani mwenye hekima, “kwa maana hujui siku itazaa nini.” (Methali 27:1) Bado maneno hayo ni ya kweli. Hakuna mwanadamu anayeweza kutabiri wakati wake ujao. Ni nini kinachomfanya Mungu awe tofauti? Anaelewa kabisa kila kitu ambacho ameumba, kutia ndani utu na mielekeo ya mwanadamu. Anapoamua kufanya hivyo, Mungu anaweza kuona kimbele jinsi watu na mataifa watakavyotenda. Zaidi ya hayo, ana uwezo usio na mipaka wa kudhibiti jinsi mambo yatakavyotukia. Anapotabiri kupitia manabii kwamba jambo fulani litatokea, yeye anakuwa “Yule anayelitimiza neno la mtumishi wake, na Yule anayelitekeleza kikamilifu shauri la wajumbe wake.” (Isaya 44:26) Ni Yehova Mungu peke yake ambaye anaweza kusema hivyo.

Isaya aliishi zaidi ya miaka 700 kabla ya Yesu, yule Masihi. Hata hivyo, Isaya alitabiri kuhusu kuja kwa Masihi. Lakini hasa kuanzia karne ya 18 na kuendelea, wachambuzi wa Biblia wameshambulia uasilia wa kitabu cha Isaya. Wanadai kwamba unabii huo kuhusu Masihi si unabii wa kweli, eti uliandikwa baada ya matukio yenyewe. Je, hilo ni kweli? Mnamo 1947, nakala ya kitabu cha Isaya pamoja na vitabu vingine vya zamani vya kukunjwa viligunduliwa katika pango karibu na Bahari ya Chumvi. Wasomi walikadiria kwamba nakala hiyo iliandikwa zaidi ya miaka 100 kabla ya kuzaliwa kwa Masihi aliyetabiriwa au Kristo. Ndiyo, Biblia ilifunua mambo ya wakati ujao!

Isaya na waandikaji wengine wa Biblia hawangetabiri kuhusu wakati ujao kwa kutegemea hekima yao wenyewe. Badala ya hivyo, “walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.” (2 Petro 1:21) Katika habari zinazofuata, tutakazia mambo hususa kuhusu maisha ya Yesu kama yalivyotabiriwa na Isaya. Kisha tutachunguza matukio ambayo Yesu na wanafunzi wake walitabiri kuhusu wakati wetu na wakati ujao.