Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vitabu vya Injili Vinategemeka Kadiri Gani?

Vitabu vya Injili Vinategemeka Kadiri Gani?

Vitabu vya Injili Vinategemeka Kadiri Gani?

“Sasa vitabu vya injili vinapaswa kuonwa kuwa vilitokana na hadithi za kubuniwa za Wakristo wa mapema.”—Burton L. Mack, profesa aliyestaafu wa masomo ya Agano Jipya.

MBALI na profesa anayenukuliwa hapo juu, kuna watu wengine walio na maoni kama hayo. Wasomi kadhaa wameshuku kutegemeka kwa vitabu vya Injili vya Mathayo, Marko, Luka, na Yohana—masimulizi ya Biblia kuhusu maisha na huduma ya Yesu. Kwa nini watu fulani wanaviona vitabu vya Injili kuwa hadithi za kubuniwa? Je, maoni yao yanapaswa kukufanya uwe na mashaka kuhusu ukweli wa vitabu hivyo? Hebu tuchunguze uthibitisho uliopo.

Mashaka Kuhusu Kutegemeka kwa Vitabu vya Injili

Katika karne 17 za kwanza za Wakati wetu wa Kawaida, kutegemeka kwa vitabu vya Injili hakukutiliwa shaka. Hata hivyo, hasa kuanzia karne ya 19 na kuendelea, wasomi kadhaa wamesema kwamba vitabu vya Injili havikuongozwa na roho ya Mungu bali vilitungwa na wanadamu. Isitoshe, wamepinga kwamba waandikaji wa vitabu vya Injili waliandika habari za Yesu walizojionea wenyewe na wamesisitiza kwamba wanaume hao hawangeweza kuandika historia inayotegemeka. Zaidi ya hilo, wamekata kauli kwamba kwa kuwa muundo na maandishi ya vitabu vitatu vya kwanza vya Injili yanalingana, hilo linaonyesha kwamba waandikaji hao waliangalia maandishi ya wenzao walipokuwa wakiandika. Wachambuzi pia wamekataa miujiza ya Yesu na ufufuo wake kama ulivyofafanuliwa katika vitabu vya Injili. Wengine wamedai kwamba Yesu hakuwa mtu halisi!

Watu haohao wamekata kauli kwamba Marko ndiye aliyeandika kitabu cha kwanza cha Injili, kwa kuwa anaongezea habari chache kwa vitabu vya Mathayo na Luka. Pia wachambuzi hao wamedai kwamba Mathayo na Luka walitumia kitabu cha Marko kuandika vitabu vyao na kwamba walitumia hati ya ziada iliyoitwa na wasomi Q (herufi inayotokana na neno la Kijerumani Quelle, au “chanzo”). Kulingana na msomi wa Biblia A.F.J. Klijn, nadharia hiyo inayojulikana sana “inawafanya waandikaji wa Injili kuwa wakusanyaji wa hadithi mbalimbali tu.” Wazo hilo linawafanya waandikaji wa Injili kuwa wezi wa maandishi na watungaji wa hadithi. Hilo linawafanya watu wasiamini kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Mungu.—2 Timotheo 3:16.

Je, Waandikaji wa Injili Waliiba Maandishi?

Je, ulinganifu uliopo kati ya vitabu vitatu vya kwanza vya Injili unathibitisha kwamba waandikaji wake waliiba maandishi? Hapana. Kwa nini? Jambo moja ni kwamba Yesu aliwaahidi wanafunzi wake roho takatifu ambayo ‘ingewakumbusha mambo yote aliyokuwa amewaambia.’ (Yohana 14:26) Kwa hiyo, haishangazi kwamba waandikaji wa Injili walikumbuka na kuandika matukio fulani yanayofanana. Ni kweli kwamba huenda waandikaji fulani wa Biblia walisoma na kurejelea maandishi ya waandikaji wengine wa Biblia, lakini hilo linaonyesha kwamba walifanya utafiti kwa makini bali hawakuiba maandishi. (2 Petro 3:15) Kwa kuongezea, kamusi moja ya Biblia (The Anchor Bible Dictionary) inasema: “Kwa kuwa mapokeo yalipitishwa kwa mdomo inaeleweka ni kwa nini maneno muhimu ambayo Yesu alisema yaliandikwa na waandikaji mbalimbali kwa njia ileile.”

Luka alisema kwamba alizungumza na watu wengi waliojionea mambo yaliyotendeka na ‘alifuata kwa uangalifu mambo yote tangu mwanzo kwa usahihi.’ (Luka 1:1-4) Je, hilo linamfanya Luka awe mwizi wa maandishi au mtungaji wa hadithi? Hapana! Baada ya kuchunguza kwa makini maandishi ya Luka, mtaalamu wa vitu vya kale William Ramsay alisema hivi: “Luka ni mwanahistoria wa hali ya juu: si eti tu maandishi yake yanategemeka, bali pia alijua jinsi matukio ya historia yalivyofuatana . . . Mwandikaji huyo anapaswa kuwekwa katika orodha ya wanahistoria bora.”

Ushuhuda wa waandikaji wa kale wa mafundisho ya Kikristo kutia ndani mwanatheolojia Origen, unaonyesha pia kwamba mtume Mathayo ndiye aliyekuwa wa kwanza kuandika kitabu cha Injili. Origen aliandika hivi: “Kitabu cha kwanza kiliandikwa na Mathayo, aliyekuwa mkusanya-kodi, lakini baadaye akawa mtume wa Yesu Kristo, alikiandika katika Kiebrania kwa ajili ya Wayahudi waliogeuzwa imani.” Ni wazi kwamba mtume Mathayo aliyekuwapo mambo aliyoandika yalipotukia hakuhitaji kuiba maandishi ya Marko ambaye hakujionea matukio hayo. Basi, je, kuna uthibitisho unaoonyesha kwamba Mathayo na Luka waliiba maandishi ya Marko na kutumia ile hati inayoitwa Q?

Je, Injili ya Marko Iliandikwa Kwanza?

Wazo la kwamba Injili ya Marko iliandikwa kwanza na kwamba ilitumiwa na Mathayo na Luka halina “msingi hakika,” inasema kamusi moja ya Biblia (The Anchor Bible Dictionary). Hata hivyo, wasomi wengi wanaamini kwamba Marko aliandika Injili yake kabla ya Mathayo na Luka kwa sababu wanadai kwamba Marko hakuandika mambo mengi ya ziada kuliko Injili nyingine. Kwa mfano, msomi wa Biblia wa karne ya 19 Johannes Kuhn alisisitiza kwamba ni lazima Injili ya Marko iwe iliandikwa kwanza. La sivyo, Kuhn alisema, “mtu angehitaji kufikiri kwamba Marko alikata Injili ya Mathayo na Luka katika vipande vidogo-vidogo na kuvichanganya kwenye nyungu na kutokeza Injili kutokana na mchanganyiko huo.”

Kwa kuwa Injili ya Marko ndiyo fupi zaidi, haishangazi kwamba ina habari chache za pekee. Hata hivyo, hilo halithibitishi kwamba ni lazima iwe iliandikwa kwanza. Zaidi ya hilo, si kweli kwamba Marko haandiki mambo yoyote ya ziada kuliko yale yaliyo katika Injili ya Mathayo na Luka. Katika simulizi linaloambatanisha kwa haraka matukio ya huduma ya Yesu kuna habari zenye kupendeza na mistari zaidi ya 180 ambayo haipatikani katika Mathayo na Luka, hivyo kulifanya kuwa simulizi la pekee la maisha ya Yesu.—Ona  sanduku kwenye ukurasa wa 13.

Namna Gani Hati Inayoitwa Q?

Ni nini kinachoweza kusemwa kuhusu hati Q, ambayo wengine hudai kwamba ilitumiwa kuandika Mathayo na Luka? James M. Robinson, profesa wa dini, anasema: “Bila shaka, Q ni maandishi muhimu zaidi ya Kikristo ambayo tunayo.” Maneno hayo yanashangaza kwa kuwa hakuna hati inayojulikana kama Q, na kwa kweli, hakuna mtu anayeweza kuthibitisha kwamba ilikuwapo! Kutoweka kwake kunashangaza hata zaidi kwa sababu wasomi wanadai kwamba kulikuwa na nakala kadhaa za hati hizo. Kwa kuongezea, hati Q haitajwi na waandikaji wa kale wa maandishi ya Kikristo.

Fikiria kuhusu hili. Inaaminiwa kwamba Q ilikuwapo na inathibitisha kwamba Injili ya Marko iliandikwa kwanza. Je, hiyo si nadharia inayotegemea nadharia nyingine? Inapohusu nadharia kama hizo, ni jambo la hekima kukumbuka methali hii: “Mujinga anaamini kila neno: lakini mwenye akili anaangalia sana namna anavyokwenda.”—Methali 14:15, Zaire Swahili Bible.

Vitabu vya Injili Ni vya Kweli na Vinategemeka

Kwa sababu ya makisio na nadharia zao zisizo na msingi, wachambuzi wamewakengeusha watu wengi wasichunguze masimulizi yanayotegemeka ya Injili kuhusu maisha na huduma ya Yesu. Masimulizi haya yanaonyesha waziwazi kwamba Wakristo wa mapema hawakuona matukio ya maisha, huduma, kifo, na ufufuo kuwa hadithi za kubuniwa. Mamia ya mashahidi walithibitisha ukweli wa matukio hayo. Wakristo hao wa mapema, waliokuwa tayari kukabili mnyanyaso na kifo ili kuwa wafuasi wa Yesu, walitambua kwamba kuwa Mkristo kungekuwa jambo lisilopatana na akili ikiwa huduma na ufufuo wa Yesu yalikuwa mambo ya kuwaziwa tu.—1 Wakorintho 15:3-8, 17, 19; 2 Timotheo 2:2.

Akizungumzia ubishi kuhusu nadharia kwamba Injili ya Marko iliandikwa kwanza na hati Q ambayo ilipotea kwa njia zisizoeleweka, George W. Buchanan, profesa wa theolojia, anasema: “Kukazia fikira nadharia kuhusu chanzo cha habari kunamfanya mwanafunzi wa Biblia asijifunze maandishi yenyewe.” Hilo linapatana na maneno ambayo mtume Paulo alimwandikia Timotheo kwamba ‘asisikilize hadithi za uwongo na mambo ya kutafuta-tafuta ukoo, ambayo mwisho wake si kitu, lakini ambayo hutokeza maswali ya utafiti badala ya kugawa kitu chochote kutoka kwa Mungu kuhusiana na imani.’—1 Timotheo 1:4.

Vitabu vya Injili vinategemeka. Vina masimulizi yanayoaminika ya watu waliojionea matukio yenyewe. Vilifanyiwa utafiti mwingi. Vinatufundisha mambo mengi yanayopendeza kuhusu maisha ya Yesu Kristo. Kwa hiyo, kama Timotheo wa kale, inafaa tutii maneno haya ya Paulo: “Endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini.” Tuna sababu nzuri za kukubali kwamba “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu,” kutia ndani vitabu vyote vinne vya Injili.—2 Timotheo 3:14-17.

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

 Kama Kitabu cha Marko Hakingeandikwa, Hatungejua Kwamba . . .

Yesu alitazama huku na huku kwa ghadhabu, akiwa amehuzunishwa na jinsi mioyo yao ilivyokuwa migumu (Marko 3:5)

Yohana na Yakobo waliitwa Boanerge (Marko 3:17)

mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu alikuwa ametumia mali zake zote (Marko 5:26)

Herodia alikuwa na kinyongo moyoni kumwelekea Yohana Mbatizaji na Herode alikuwa akimwogopa Yohana naye alikuwa akimlinda (Marko 6:19, 20)

Yesu aliwaambia wanafunzi wake wapumzike kidogo (Marko 6:31)

Mafarisayo walinawa mikono yao mpaka kwenye kiwiko (Marko 7:2-4)

Yesu aliwakumbatia watoto (Marko 10:16)

Yesu alimpenda yule mtawala kijana (Marko 10:21)

Petro, Yakobo, Yohana, na Andrea walimuuliza Yesu faraghani (Marko 13:3)

kijana fulani aliacha vazi lake la kitani (Marko 14:51, 52)

Isitoshe, mfano mmoja wa Yesu na miujiza yake miwili inapatikana tu katika kitabu cha Marko.—Marko 4:26-29; 7:32-37; 8:22-26.

Injili ya Marko ina masimulizi mengi ya watu waliojionea wenyewe matukio ambayo hayapatikani katika vitabu vingine vya Injili. Uthamini wetu kwa ajili ya kitabu hicho utaongezeka tukitenga wakati ili kutafakari thamani ya habari hizo zote muhimu.