Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafundishe Watoto Wako

Are You Ever Jealous? Joseph’s Brothers Were

Are You Ever Jealous? Joseph’s Brothers Were

ACHENI tuzungumze kuhusu maana ya kuwa na wivu. Umewahi kushindwa kumpenda mtu kwa sababu watu wanasema kwamba ni mzuri, ana sura nzuri, au ana akili nyingi? *— Ndivyo inavyoweza kuwa ikiwa unamwonea mtu fulani wivu.

Kunaweza kuwa na wivu katika familia ikiwa wazazi wanampendelea mtoto mmoja. Biblia inasimulia kuhusu familia iliyopatwa na tatizo kubwa kwa sababu ya wivu. Acheni tuchunguze matatizo yaliyotokea na funzo tunaloweza kupata kutokana na kisa hicho.

Yosefu alikuwa mwana wa 11 wa Yakobo, na ndugu wa kambo wa Yosefu walimwonea wivu. Unajua ni kwa nini?— Ni kwa sababu Yakobo baba yao, alimpendelea Yosefu. Kwa mfano, Yakobo alikuwa amemshonea Yosefu koti maridadi lenye mistari. Yakobo alimpenda sana Yosefu “kwa sababu alikuwa mwana wa uzee wake” na mtoto wa kwanza wa mke wake mpendwa Raheli.

Biblia inasema kwamba ‘ndugu za Yosefu walipoona kwamba baba yao alimpenda zaidi, wakaanza kumchukia Yosefu.’ Kisha siku moja Yosefu aliiambia familia yake kwamba aliota kuwa wote walikuwa wamemwinamia, kutia ndani baba yao. Biblia inasema kwamba ‘ndugu zake walianza kumwonea wivu,’ na hata baba ya Yosefu alimkaripia kwa kuwaambia kuhusu ndoto hiyo.—Mwanzo 37:1-11.

Muda fulani baadaye, Yosefu alipokuwa na umri wa miaka 17, ndugu zake walikuwa wameenda mbali kulisha kondoo na mbuzi za familia yao. Kwa hiyo, Yakobo akamtuma Yosefu akawajulie hali ndugu zake. Je, unajua kile ambacho wengi wao walitaka kufanya walipomwona akija?— Walitaka kumwua! Lakini wawili kati yao, yaani, Rubeni na Yuda hawakutaka kufanya hivyo.

Wanabiashara fulani walipokuwa wakipita wakielekea Misri, Yuda akasema: “Tumuuze.” Wakafanya hivyo. Kisha wakamwua mbuzi na kutumbukiza koti la Yosefu ndani ya damu yake. Baadaye, walipomwonyesha baba yao koti hilo, alilia hivi kwa sauti: ‘Mnyama-mwitu mkali amemla!’—Mwanzo 37:12-36.

Baada ya muda, Yosefu akapendwa na Farao, mtawala wa Misri kwa sababu kwa msaada wa Mungu, aliweza kueleza maana ya ndoto mbili za Farao. Ndoto ya kwanza ilihusu ng’ombe saba wenye afya ambao walifuatwa na ng’ombe saba waliokonda. Ndoto ya pili ilihusu masuke saba ya nafaka yaliyokuwa mazuri na masuke saba ya nafaka yaliyonyauka. Yosefu alisema kwamba ndoto zote mbili zilimaanisha kungekuwa na miaka saba ya mavuno mengi ikifuatwa na miaka saba ya njaa. Farao akaagiza Yosefu awe msimamizi wa kuhifadhi chakula wakati wa mavuno mengi ili kujiandaa kwa ajili ya miaka ya njaa.

Njaa ilipoanza, familia ya Yosefu iliyokuwa ikiishi mbali sana ilihitaji chakula. Yakobo aliwatuma ndugu kumi wakubwa wa Yosefu huko Misri kutafuta chakula. Wakaja kwa Yosefu, lakini hawakumtambua. Bila kujitambulisha, Yosefu alitaka kuona ikiwa ndugu zake walikuwa wamebadilisha maoni yao kumwelekea, na akaona kwamba walikuwa wamejuta sana kwa kumtendea mabaya. Kisha Yosefu akawaambia yeye ni nani. Walikumbatiana na kushangilia kama nini!—Mwanzo, sura ya 40 hadi 45.

Unaweza kujifunza nini kuhusu wivu kutokana na hadithi hiyo ya Biblia?— Wivu unaweza kutokeza tatizo kubwa, hata kumfanya mtu atake kumwumiza ndugu yake! Acheni tusome Matendo 5:17, 18 na Matendo 7:54-59 na tuone wivu uliwafanya watu fulani wawatendee wanafunzi wa Yesu kwa njia gani.— Baada ya kusoma masimulizi hayo, je, unaona ni kwa nini tunapaswa kujihadhari dhidi ya kuwa na wivu?—

Yosefu aliishi kufikia umri wa miaka 110. Alilea watoto ambao walizaa wajukuu, kisha wao wakazaa vitukuu. Tunaweza kuwa na hakika kwamba Yosefu aliwafundisha mara nyingi kupendana na kujiepusha na wivu.—Mwanzo 50:22, 23, 26.

^ fu. 3 Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.