Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Fundisho Lililoenea

Fundisho Lililoenea

Fundisho Lililoenea

“Niliota kwamba nilikuwa nikiungua katika moto wa mateso! Nilipokuwa nikiota niligutuka na kuamka nikipiga mayowe. Kwa sababu hiyo, nilijaribu sana nisitende dhambi.”—Arline.

JE, UNAAMINI kwamba watenda-dhambi watateswa katika moto wa mateso? Watu wengi wanaamini hivyo. Kwa mfano, mnamo 2005 msomi mmoja katika Chuo Kikuu cha St. Andrews huko Scotland aligundua kwamba asilimia 33 hivi ya viongozi wa kidini nchini humo waliamini kwamba moto wa mateso ni mahali ambapo watu wanaojitenga na Mungu watateseka milele kiakili. Asilimia 20 kati yao waliamini kwamba watu wanaoenda kwenye moto wa mateso watateseka kimwili.

Katika nchi nyingi, watu wengi wanaamini kuna moto wa mateso. Kwa mfano, kura ya maoni iliyofanywa nchini Marekani mnamo 2007 ilionyesha kwamba asilimia 70 hivi ya watu waliohojiwa wanaamini kuna moto wa mateso. Hata katika nchi ambazo watu wengi hawapendezwi na dini, bado wengi wanaamini kuna moto wa mateso. Kura ya maoni iliyofanywa mnamo 2004 ilionyesha kwamba nchini Kanada, asilimia 42 ya watu wanaamini kuna moto wa mateso. Na nchini Uingereza, asilimia 32 wana uhakika kwamba kuna moto wa mateso.

Viongozi wa Kidini Wanafundisha Nini?

Viongozi wengi wa kidini wameacha kufundisha kwamba moto wa mateso ni mahali ambapo watu wanateswa kimwili. Badala yake, wanaunga mkono ufafanuzi unaotolewa katika kitabu kimoja cha Kikatoliki kilichochapishwa mnamo 1994 (Catechism of the Catholic Church). “Adhabu kuu ya moto wa mateso,” kinasema kitabu hicho, “ni kutenganishwa milele na Mungu.”

Hata hivyo, fundisho la kwamba moto wa mateso ni mahali watu wanateswa kiakili au kimwili bado linaendelezwa. Watu wanaounga mkono fundisho hilo wanasema linatoka katika Biblia. R. Albert Mohler, msimamizi wa Seminari ya Theolojia ya Southern Baptist anasema: “Ni fundisho hakika la Biblia.”

Imani Yako Ni Muhimu Kadiri Gani?

Ikiwa kweli kuna moto wa mateso, unapaswa kuogopa moto huo. Hata hivyo, ikiwa fundisho hilo si la kweli, viongozi wa kidini ambao wanalifundisha wanaleta mvurugo na kuwafanya watu waogope bila sababu. Pia wanalichafua jina la Mungu.

Biblia, Neno la Mungu, linasema nini kuhusu jambo hilo? Katika habari zinazofuata tutatumia Biblia za Kikatoliki na za Kiprotestanti kujibu maswali haya matatu: (1) Ni nini kinachompata mtu anapokufa? (2) Yesu alifundisha nini kuhusu moto wa mateso? (3) Kujifunza ukweli kuhusu moto wa mateso kunaweza kuwa na matokeo gani kwako?