Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mashahidi wa Yehova Wanaamini Kwamba Ni Wao Tu Watakaookolewa?

Je, Mashahidi wa Yehova Wanaamini Kwamba Ni Wao Tu Watakaookolewa?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Je, Mashahidi wa Yehova Wanaamini Kwamba Ni Wao Tu Watakaookolewa?

Mashahidi wa Yehova wanafikiri kwamba wana dini ya kweli. Ikiwa hawangefikiri hivyo, wangebadili imani zao. Kama tu waumini wa dini nyingi, Mashahidi wa Yehova wanatumaini kuokolewa. Hata hivyo, pia wanaamini kwamba si kazi yao kuamua ni nani atakayeokolewa. Mungu ndiye Hakimu. Yeye ndiye anayeamua.—Isaya 33:22.

Neno la Mungu linafunua kwamba wale watakaookolewa ni lazima watake kuokolewa na washirikiane na Mwokozi. Kwa mfano: Tuseme kwamba mtu amepotea jangwani. Anataka sana kufika anakoenda. Je, atakufa, au ataokoka? Matokeo yatategemea ikiwa atakubali msaada. Kwa kiburi, anaweza kukataa msaada wa mwokoaji, au kwa unyenyekevu anaweza kukubali msaada unaotolewa na kufika anakoenda akiwa salama.

Vivyo hivyo, wale wanaoshirikiana na Mwokoaji wa wanadamu Yehova Mungu, ndio watakaookolewa. Wokovu ni zawadi kutoka kwa Mungu, hata hivyo si wote watakaoupata. Mwana wa Mungu, Yesu, alisema: “Si kila mtu anayeniambia, ‘Bwana, Bwana,’ atakayeingia katika ufalme wa mbinguni, bali yule anayefanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia.”—Mathayo 7:21.

Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba Mungu anawaokoa wale tu wanaoonyesha imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu na wanaofuata kwa ukaribu mafundisho ya Yesu. (Matendo 4:10-12) Fikiria matakwa matatu muhimu yanayohitajiwa ili mtu aokolewe yanayoonyeshwa na Neno la Mungu.

(1) Yesu aliwaambia waandamani wake hivi: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Mfano wa Yesu wa kutoa uhai wake kwa ajili ya wengine ulionyesha umuhimu wa upendo. Wale wanaowapenda wengine wanaonyesha sifa muhimu kwa ajili ya wokovu.

(2) Yesu alisali hivi kwa Baba yake: “Nimewajulisha jina lako.” (Yohana 17:26) Yesu alijua jinsi jina la Mungu la kibinafsi, Yehova, lilivyo muhimu kwa Baba yake. Yesu alisali kwamba jina la Baba yake “litakaswe.” (Mathayo 6:9) Kutakasa jina hilo kunatia ndani kulijua na kuliona kuwa muhimu na takatifu. Kwa kumwiga Yesu, watu wanaotaka kuokolewa wanahitaji kutumia jina la Mungu. Pia, wanahitaji kuwafundisha wengine kuhusu jina la Mungu na sifa zake. (Mathayo 28:19, 20) Kwa kweli, ni wale tu wanaoliitia jina la Mungu watakaookolewa.—Waroma 10:13.

(3) Yesu alimwambia Pontio Pilato: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu.” (Yohana 18:36) Ni watu wachache sana leo wanaoamini Ufalme wa Mungu au serikali ambayo Mfalme wake ni Yesu. Badala yake wanatumaini mashirika ya kibinadamu. Tofauti na hilo, wale watakaookolewa wanaunga mkono Ufalme wa Mungu kwa ushikamanifu na kuwafundisha wengine jinsi utakavyowakomboa wanadamu wote waaminifu.—Mathayo 4:17.

Baada ya kujifunza baadhi ya matakwa ya wokovu, wanafunzi wa Yesu waliuliza: “Ni nani anayeweza kuokolewa?” Yesu akajibu: “Mambo yasiyowezekana kwa wanadamu yanawezekana kwa Mungu.” (Luka 18:18-30) Mashahidi wa Yehova wanajitahidi kutimiza matakwa hayo ya wokovu. Pia, wanajitahidi kuwasaidia wengine waokolewe.