Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutokea na Kuanguka kwa “Merikebu za Tarshishi”

Kutokea na Kuanguka kwa “Merikebu za Tarshishi”

Kutokea na Kuanguka kwa “Merikebu za Tarshishi”

“Merikebu za Tarshishi ndizo zilikusafirishia bidhaa zako.”—EZEKIELI 27:25, BIBLIA HABARI NJEMA

MERIKEBU, au meli za Tarshishi zilisaidia kumtajirisha Mfalme Sulemani. Watu waliozitengeneza walichangia kuanzishwa kwa alfabeti za Kigiriki na Kiroma. Pia, walianzisha jiji lililoitwa Byblos, na jina hilo likaja kuwa jina la Biblia katika lugha nyingi.

Ni nani waliotengeneza na kuabiri meli za Tarshishi? Kwa nini meli hizo ziliitwa hivyo? Na matukio yanayohusu watu hao na meli zao yanathibitisha usahihi wa Biblia kwa njia gani?

Mabwana wa Mediterania

Wafoinike walitengeneza meli zilizokuja kuitwa meli za Tarshishi. Tayari Wafoinike walikuwa mabaharia stadi miaka elfu moja hivi kabla ya wakati wa Kristo. Eneo lao lilikuwa pwani nyembamba inayofanana na Lebanoni ya kisasa. Mataifa mengine yaliishi upande wa kaskazini, mashariki, na kusini. Upande wa magharibi, walipakana na Bahari ya Mediterania. Ili kupata utajiri, Wafoinike walitazamia kufanya biashara na mataifa yaliyokuwa kando ya bahari hiyo.

Hatua kwa hatua, mabaharia Wafoinike walitengeneza meli nyingi za kibiashara. Kadiri walivyopata faida na kufanya maendeleo katika tekinolojia yao, walitengeneza meli kubwa zaidi ambazo zingeweza kusafiri mbali zaidi. Baada ya kufika kwenye Visiwa vya Balearic, Kipro, na Sardinia, Wafoinike walipitia kando ya pwani ya Afrika Kaskazini wakielekea upande wa magharibi hadi Hispania. (Ona ramani.)

Watengenezaji wa meli Wafoinike walitengeneza meli ndefu sana. Inaonekana meli hizo ziliitwa “meli za Tarshishi” kwa kuwa zingeweza kusafiri umbali wa kilomita 4,000 kutoka Foinike hadi Hispania kusini ambako huenda Tarshishi ilikuwa. *

Huenda Wafoinike hawakutaka kutawala ulimwengu bali walitaka kujitajirisha kutokana nao. Walifanya hivyo kwa kuanzisha vituo vya kibiashara. Hata hivyo, wafanyabiashara hao walikuja kuwa mabwana wa Mediterania.

Mbele ya Mediterania

Katika jitihada zao za kujitajirisha, Wafoinike walisafiri kwenye Bahari ya Atlantiki. Meli zao ziliendelea kupitia pwani ya kusini ya Hispania hadi zikawasili kwenye eneo linaloitwa Tartessus. Mnamo 1100 K.W.K., walianzisha jiji ambalo waliliita Gadir. Bandari hiyo, ambayo sasa inaitwa Cádiz, nchini Hispania, ikawa moja kati ya majiji ya kwanza makubwa ya Ulaya Magharibi.

Wafoinike waliuza chumvi, divai, samaki waliokaushwa, mierezi, misonobari, vyombo vya chuma, glasi, mapambo, kitani safi, na vitambaa vilivyotiwa rangi maarufu ya zambarau ya Tiro. Hispania ingewapa utajiri gani?

Kati ya maeneo yote ya Mediterania, eneo la Hispania Kusini ndilo lililokuwa na fedha na vyuma vingine vingi vyenye thamani. Nabii Ezekieli alisema hivi kuhusu Tiro iliyokuwa bandari kuu ya Wafoinike: “Watu wa Tarshishi [Hispania] walifanya biashara nawe kwa sababu ya utajiri wako mwingi na wa kila namna. Walitoa fedha, chuma, bati, na risasi kupata bidhaa zako.”—Ezekieli 27:12, BHN.

Wafoinike waligundua madini mengi sana karibu na Mto Guadalquivir, ulio karibu na Cádiz. Bado madini hayo yanachimbwa katika eneo hilo ambalo sasa linaitwa Río Tinto. Migodi hiyo imetokeza madini yenye thamani kwa miaka elfu tatu hivi.

Kwa kuwa njia ya usafiri kati ya Wahispania na Wafoinike ilikuwa imeimarishwa, Wafoinike walidhibiti biashara ya fedha ya Hispania. Fedha ilifurika katika Foinike na hata katika Israeli iliyokuwa jirani. Mfalme Sulemani wa Israeli alifanya mapatano ya kibiashara na Mfalme Hiramu wa Foinike. Kwa sababu hiyo, katika siku za Sulemani, fedha “haikuhesabiwa kuwa kitu.”—1 Wafalme 10:21. *

Ingawa Wafoinike walikuwa wafanyabiashara wenye mafanikio, walikuwa pia wakatili. Inasemekana kwamba nyakati nyingine waliwashawishi watu waingie melini ili wawaonyeshe bidhaa lakini wakawafanya kuwa watumwa. Baada ya muda, waliwasaliti Waisraeli ambao walikuwa wafanyabiashara wenzi na kuwauza utumwani. Hivyo, manabii Waebrania walitabiri kuharibiwa kwa jiji la Wafoinike la Tiro. Unabii huo ulitimizwa na Aleksanda Mkuu mnamo 332 K.W.K. (Yoeli 3:6; Amosi 1:9, 10) Uharibifu huo ulitia alama mwisho wa enzi ya Wafoinike.

Tunafaidika Jinsi Gani Kutokana na Wafoinike?

Kama tu wafanyabiashara wote wenye mafanikio, Wafoinike waliandika mapatano yao. Walitumia mfumo wa alfabeti unaofanana na ule wa Kiebrania cha kale. Mataifa mengine yaliona faida za kutumia alfabeti za Kifoinike. Baada ya kufanyiwa mabadiliko fulani, ikawa msingi wa alfabeti ya Kigiriki ambayo ilikuja kutumiwa katika maandishi ya Kiroma. Alfabeti ya Kiroma inatumiwa sana leo.

Isitoshe, jiji muhimu la Foinike linaloitwa Byblos lilikuwa kituo cha kugawa mafunjo ambayo yalitumiwa kabla ya karatasi kutengenezwa. Kutumiwa kwa mafunjo kulisaidia kutokezwa kwa vitabu. Kwa kweli, neno la Kiswahili, Biblia, ambacho ni kitabu kilichosambazwa zaidi duniani, linatokana na jina la jiji hilo, Byblos. Bila shaka, historia ya Wafoinike na meli zao inatuhakikishia kwamba Biblia inategemea mambo hakika.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Baada ya muda, usemi “meli za Tarshishi” ulitumiwa kumaanisha aina ya meli ambayo ingeweza kusafiri mbali sana.

^ fu. 15 “Kundi la meli za Tarshishi” za Sulemani zilifanya kazi pamoja na kundi la meli za Hiramu, na huenda zilitoka Esion-geberi na kufanya biashara kwenye Bahari Nyekundu au hata mbali zaidi.—1 Wafalme 10:22.

[Ramani katika ukurasa wa 27]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

NJIA ZA WAFOINIKE ZA BIASHARA

HISPANIA

TARTESSUS

Mto Guadalquivir

Gadir

Corsica

Visiwa vya Balearic

Sardinia

Sisili

Krete

Kipro

Byblos

Tiro

BAHARI YA MEDITERANIA

Esion-geberi

Bahari Nyekundu

AFRIKA

[Picha katika ukurasa wa 27]

Sarafu ya karne ya tatu hadi ya nne K.W.K. inayoonyesha meli ya Wafoinike

[Picha katika ukurasa wa 27]

Magofu ya makao ya Wafoinike, Cádiz, Hispania

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 26]

Museo Naval, Madrid

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 27]

Coin: Museo Arqueológico Municipal. Puerto de Sta. María, Cádiz; remains: Yacimiento Arqueológico de Doña Blanca, Pto. de Sta. María, Cádiz, España