Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mpenda-Haki

Mpenda-Haki

Mkaribie Mungu

Mpenda-Haki

Waebrania 10:26-31

JE, UMEWAHI kutendewa kwa njia isiyo ya haki au kwa ukatili, labda na mtu ambaye inaonekana haadhibiwi na hatubu? Hiyo ni moja kati ya hali ngumu zaidi kushughulika nayo, hasa ikiwa jambo hilo linafanywa na mtu unayetazamia akupende na kukujali. Huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini Mungu anaruhusu mambo kama hayo yatukie?’ * Ukweli ni kwamba Yehova Mungu anachukia ukosefu wa haki. Neno lake, Biblia, linatuhakikishia kwamba Mungu atawaadhibu watenda-dhambi wasiotubu. Acheni tuchunguze maneno yaliyorekodiwa na mtume Paulo kwenye Waebrania 10:26-31.

Paulo anaandika: “Tukizoea kutenda dhambi kimakusudi baada ya kupokea ujuzi sahihi juu ya kweli, hakuna tena dhabihu yoyote iliyobaki kwa ajili ya dhambi.” (Mstari wa 26) Watu wanaotenda dhambi kimakusudi wana hatia. Kwa nini? Kwanza, ni kwa sababu hawafanyi dhambi mara mojamoja tu kwa sababu ya udhaifu, dhambi ambazo nyakati nyingine sisi sote tunafanya kwa sababu hatujakamilika. Wamezoea kutenda dhambi. Pili, dhambi zao ni za kimakusudi. Kama vile Biblia Habari Njema inavyosema ‘wanatenda dhambi makusudi.’ Ubaya uliokita mizizi umejaa katika mioyo yao. Tatu, hawafanyi dhambi kwa sababu ya kutojua. Wana “ujuzi sahihi juu ya kweli” kuhusu mapenzi na njia za Mungu.

Mungu ana maoni gani kuhusu wale wanaotenda dhambi kimakusudi bila kutubu? “Hakuna tena dhabihu yoyote iliyobaki kwa ajili ya dhambi,” akasema Paulo. Dhabihu ya Kristo, zawadi ya Mungu kwa wanadamu, inafunika dhambi tunazofanya kwa sababu ya kutokamilika kwetu. (1 Yohana 2:1, 2) Lakini wale wanaofanya dhambi bila kutubu wanaonyesha kwamba hawathamini zawadi hiyo muhimu. Kwa maoni ya Mungu, ‘wamemkanyagia chini Mwana wa Mungu na kuiona kuwa yenye thamani ya kawaida tu damu ya’ Yesu. (Mstari wa 29) Kwa mwenendo wao, wanamdharau Yesu na kuona damu yake kuwa “kitu ovyo,” kana kwamba haina thamani kubwa kuliko ya mwanadamu asiye mkamilifu. (Union Version) Watu hao wasio na shukrani hawatanufaika kutokana na dhabihu ya Kristo.

Waovu wanaweza kutazamia nini? Mungu wa haki ameahidi hivi: “Kisasi ni changu; mimi nitalipa.” (Mstari wa 30) Acheni wote ambao wana zoea la kutenda dhambi na kuwaumiza wengine wajihadhari. Hakuna mtu anayepuuza kimakusudi sheria za uadilifu za Mungu ambaye hataadhibiwa. Mara nyingi, wanateseka kwa sababu ya dhambi zao. (Wagalatia 6:7) Hata wasipoteseka sasa, hivi karibuni watasimama mbele ya Mungu anapokuja kuondoa ukosefu wote wa haki duniani. (Methali 2:21, 22) Paulo anaonya: “Ni jambo lenye kuogopesha kuanguka mikononi mwa Mungu aliye hai.”—Mstari wa 31.

Kujifunza kwamba Yehova Mungu hakubali dhambi zinazofanywa kimakusudi ni jambo linalofariji na kuwatia moyo, hasa watu ambao wameumizwa na mtenda-dhambi sugu. Tunaweza kumwachia Mungu, anayechukia ukosefu wa haki, daraka la kulipiza kisasi.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 1 Kwa habari zaidi kuhusu sababu ambazo Mungu amewaacha wanadamu wateseke, ona ukurasa wa 106-114 wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.