Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nini Kinachompata Mtu Anapokufa?

Ni Nini Kinachompata Mtu Anapokufa?

Ni Nini Kinachompata Mtu Anapokufa?

“Nafsi zote haziwezi kufa, hata za watu waovu . . . Wanaadhibiwa kwa moto usioweza kuzimwa, na kwa kuwa hawafi, hawawezi [kukomesha] mateso hayo.”—Clement wa Alexandria, mwandishi wa karne ya pili na ya tatu W.K.

KAMA vile Clement, wale wanaounga mkono fundisho la moto wa mateso wanaamini kwamba nafsi za wanadamu haziwezi kufa. Je, Biblia inaunga mkono fundisho hilo? Chunguza jinsi Neno la Mungu linavyojibu maswali yafuatayo.

Je, mwanamume wa kwanza, Adamu, alikuwa na nafsi isiyoweza kufa? Tafsiri ya Union Version inasema hivi kuhusu kuumbwa kwa Adamu: “BWANA Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” (Mwanzo 2:7) Ona kwamba andiko hilo halisemi kwamba Adamu alipewa nafsi.

Ni nini kilichompata Adamu alipofanya dhambi? Mungu hakusema atamwadhibu milele katika moto wa mateso. Badala yake, Biblia Habari Njema inaeleza hivi kuhusu adhabu ambayo Mungu alitoa: “Kwa jasho lako utajipatia chakula, mpaka utakaporudi udongoni ulimotwaliwa; maana wewe ni mavumbi, na mavumbini utarudi.” (Italiki ni zetu; Mwanzo 3:19) Maneno hayo ya Mungu hayaonyeshi kwamba sehemu yoyote ya Adamu ingeendelea kuishi baada ya kifo. Adamu alipokufa, nafsi, yaani, Adamu mwenyewe alikufa.

Je, kuna mwanadamu aliye na nafsi isiyoweza kufa? Mungu alimwambia hivi nabii Ezekieli: “Nafsi inayofanya zambi, itakufa.” (Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible) Mtume Paulo aliandika hivi: “Kwa njia ya mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia ulimwenguni, nayo ikasababisha kifo. Hivyo kifo kimeenea katika jumuiya yote ya binadamu, kwa maana wote wametenda dhambi.” (Waroma 5:12, BHN) Ikiwa wanadamu wote wametenda dhambi, basi nafsi zote zinakufa.

Je, nafsi iliyokufa inajua au kuhisi chochote? Neno la Mungu linasema: “Walio wazima hujua kwamba watakufa; wafu hawajui neno lo lote.” (Mhubiri 9:5, Verbum Bible) Ikifafanua kinachompata mtu anapokufa, Biblia inasema: “Huurudia udongo wake, siku hiyo mawazo yake yapotea.” (Zaburi 146:4, UV) Ikiwa wafu “hawajui neno lo lote” na ‘mawazo yao yanapotea,’ wanaweza kuteseka namna gani katika moto wa mateso?

Yesu Kristo hakusema kwamba mtu aliyekufa ana fahamu, bali alilinganisha kifo na usingizi. * (Yohana 11:11-14) Hata hivyo, huenda watu fulani wakakanusha hilo na kusema kwamba Yesu alifundisha kuna moto wa mateso na kwamba watenda-dhambi watatupwa humo. Acheni tuchunguze Yesu alisema nini hasa kuhusu moto wa mateso.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 8 Ili ujue zaidi kuhusu jambo hilo, ona habari yenye kichwa “Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu—Kuhusu Tumaini la Wafu” kwenye ukurasa wa 16 na 17.