Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siku ya Wageni Yenye Kusudi

Siku ya Wageni Yenye Kusudi

Siku ya Wageni Yenye Kusudi

“WANAFANYA nini humo?” Watu wengi ambao wanapita majengo makubwa ya Mashahidi wa Yehova huko Mogale City (Krugersdorp), karibu na Johannesburg, Afrika Kusini, wanauliza swali hilo. Kwa hiyo, Mashahidi waliamua kuwa na siku ya wageni katika ofisi ya tawi Oktoba (Mwezi wa 10) 12 na 13, 2007. Walikusudia kutimiza mambo mawili. Walitaka kukomesha maneno ya uwongo na vilevile kuonyesha umma kile ambacho ofisi hiyo ya tawi inafanya kutegemeza kazi ambayo Yesu Kristo aliamuru.—Mathayo 28:19, 20.

Wale wanaofanya kazi katika ofisi ya tawi waliweka mabango makubwa langoni kuwakaribisha watu wote, na waligawa mialiko ya pekee kwa majirani. Wafanyabiashara wenye mapatano na ofisi ya tawi pamoja na familia zao walikaribishwa. Waliitikia jinsi gani? Zaidi ya wageni 500 ambao si Mashahidi walitembelea ofisi hiyo.

Watu wengi walipendezwa na mashini ya uchapishaji inayoitwa MAN Roland Lithoman inayoweza kuchapisha magazeti 90,000 kwa saa. Pia wageni walivutiwa na eneo kubwa la upakiaji na usafirishaji linaloshughulikia vichapo zaidi ya tani 14 kila siku na vilevile wakavutiwa na eneo la kujalidi vitabu. Mashahidi katika idara mbalimbali walitayarisha vibao vya maonyesho, kutia ndani kimoja kilichoonyesha kwa ufupi historia ya uchapishaji, kuanzia na mashini za Gutenberg hadi zile za kisasa. Ubao mwingine ulionyesha jinsi ofisi ya tawi inavyotunza mazingira. Kwa mfano, sehemu fulani ya pekee inaondoa gesi zenye sumu na harufu kutoka kwenye mashini za uchapishaji, na vichujio vinakusanya vumbi linalotoka kwenye karatasi.

Gazeti la eneo hilo lilikuwa na habari iliyosema kwamba wajitoleaji 700 wanaoishi katika ofisi hiyo “ni wahudumu waliowekwa rasmi ambao wamejitoa kwa Yehova.” Pia gazeti hilo lilitaja kuhusu “usafi wa hali ya juu na jinsi mambo yanavyofanywa kwa wakati kabisa” katika idara ya uchapishaji. Mtu fulani aliyekuwa akiwapinga Mashahidi wa Yehova alikuja kutembea. Baadaye aliandika barua iliyosema: “Pongezi. Si jambo la kawaida kuona mambo yakifanywa kwa njia bora hivyo.”

Wageni wengi walithamini sana kutembelea ofisi hiyo na walishangaa kwamba ofisi hiyo ina vichapo vinavyotegemea Biblia katika lugha 151 na inachapisha vichapo kwa ajili ya nchi 18 kusini mwa Afrika na Afrika ya kati. Mtu anaweza kutembelea ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote saa za kazi. Mbona usiulize ni wakati gani unaweza kutembelea ofisi ya tawi katika eneo lenu?

[Picha katika ukurasa wa 14]

Watu wakija kutembelea ofisi ya tawi

[Picha katika ukurasa wa 14]

Mwaliko

[Picha katika ukurasa wa 15]

Ofisi ya tawi ya Afrika Kusini huko Mogale City, Afrika Kusini

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mashini ya MAN Roland Lithoman

[Picha katika ukurasa wa 15]

Mashini ya kujalidi vitabu

[Picha katika ukurasa wa 15]

Idara ya upakiaji na usafirishaji