Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu Alifundisha Nini Kuhusu Moto wa Mateso?

Yesu Alifundisha Nini Kuhusu Moto wa Mateso?

Yesu Alifundisha Nini Kuhusu Moto wa Mateso?

“Jicho lako likikukosesha,” akasema Yesu, “ling’oe, ulitupe; ni afadhali kuingia katika ufalme wa Mungu, una chongo, kuliko kuwa na macho mawili, na kutupwa katika jehanum; ambamo humo funza wao hafi, wala moto hauzimiki.”—MARKO 9:47, 48, Union Version.

Wakati mwingine, Yesu alitaja kuhusu kipindi cha hukumu wakati ambapo angewaambia hivi waovu: “Ondokeni mbele yangu enyi mliolaaniwa! Nendeni katika moto wa milele aliotayarishiwa Ibilisi na malaika wake.” Pia alisema kwamba hao “watakwenda kwenye adhabu ya milele.”—MATHAYO 25:41, 46, Biblia Habari Njema.

MTU anaposoma maneno hayo ya Yesu kwa mara ya kwanza huenda akaona ni kana kwamba yanaunga mkono fundisho la moto wa mateso. Bila shaka, Yesu hakutaka kupinga Neno la Mungu ambalo linasema hivi waziwazi: “Wafu hawajui neno lo lote.”—Mhubiri 9:5, Verbum Bible.

Basi, Yesu alimaanisha nini aliposema mtu anatupwa “katika Jehanam”? Je, Yesu alionya kuhusu “moto wa milele” ulio halisi au wa mfano? Ni katika njia gani waovu “watakwenda kwenye adhabu ya milele”? Acheni tuchunguze maswali hayo moja baada ya lingine.

Yesu alimaanisha nini aliposema mtu anatupwa “katika jehanum”? Neno la awali la Kigiriki linalotafsiriwa “jehanum” katika Marko 9:47 ni Geʹen·na. Neno la Kiebrania Geh Hin·nomʹ, linamaanisha “Bonde la Hinomu.” Bonde la Hinomu lilikuwa nje tu ya kuta za Yerusalemu la kale. Katika siku za wafalme Waisraeli, lilitumiwa kuwadhabihu watoto, zoea lenye kuchukiza ambalo Mungu alishutumu. Mungu alisema kwamba angewaharibu wote walioshiriki katika matendo kama hayo ya ibada ya uwongo. Wakati huo, Bonde la Hinomu lingeitwa “bonde la Machinjo,” ambapo “maiti za watu hawa” zingetapakaa bila kuzikwa. (Yeremia 7:30-34, Zaire Swahili Bible) Hivyo, Yehova alitabiri kwamba Bonde la Hinomu halingekuwa mahali pa kutesa watu walio hai, bali lingekuwa mahali pa kutupa maiti nyingi sana.

Katika siku za Yesu, wakaaji wa Yerusalemu walitupa takataka zao katika Bonde la Hinomu. Walitupa miili ya wahalifu sugu na kuhakikisha kwamba moto ulikuwa ukiwaka kila wakati ili uchome takataka na miili hiyo.

Yesu aliposema kuhusu funza wasiokufa na moto usiozimika, inaelekea alikuwa akirejelea andiko la Isaya 66:24. Kuhusu ‘mizoga ya watu waliomwasi Mungu,’ Isaya alisema kwamba “funza wao hatakufa, wala moto wao hautazimika.” (UV) Yesu na wasikilizaji wake walijua kwamba maneno hayo ya Isaya yalihusu mizoga ya watu wasiostahili kuzikwa.

Hivyo, Yesu alitumia Bonde la Hinomu, au Gehena, kuwa mfano unaofaa wa kifo kisicho na tumaini la ufufuo. Alikazia jambo hilo alipoonya kwamba Mungu ndiye “anayeweza kuharibu nafsi na mwili vilevile katika Gehena.” (Mathayo 10:28, ZSB) Gehena inawakilisha kifo cha milele, si mateso ya milele.

Je, Yesu alionya kuhusu “moto wa milele” ulio halisi au wa mfano? Ona kwamba “moto wa milele” unaotajwa na Yesu na kurekodiwa katika Mathayo 25:41 ulitayarishiwa “Ibilisi na malaika wake.” Je, unafikiri kwamba moto halisi unaweza kuwachoma viumbe wa roho? Au je, Yesu alikuwa akitumia neno “moto” kwa njia ya mfano? Kwa kweli, “kondoo” na “mbuzi” wanaotajwa katika mazungumzo hayo si halisi; ni mifano tu inayowakilisha aina mbili za watu. (Mathayo 25:32, 33) Moto wa milele ambao Yesu alitaja unateketeza kabisa waovu kwa njia ya mfano.

Ni katika njia gani waovu “watakwenda kwenye adhabu ya milele”? Ingawa tafsiri nyingi zinatumia neno “adhabu” katika Mathayo 25:46, maana ya msingi ya neno la Kigiriki koʹla·sin ni “kudhibiti ukuzi wa miti,” au kupogoa, kukata matawi yasiyohitajiwa. Kwa hiyo, watu wenye mfano wa kondoo wanapopokea uzima wa milele, watu wenye mfano wa mbuzi wasiotubu wanapatwa na “adhabu ya milele,” kukatiliwa mbali milele.

Una Maoni Gani?

Yesu hakufundisha kwamba wanadamu wana nafsi isiyoweza kufa. Hata hivyo, mara nyingi alifundisha kwamba wafu watafufuliwa. (Luka 14:13, 14; Yohana 5:25-29; 11:25) Kwa nini Yesu afundishe kwamba wafu watafufuliwa ikiwa aliamini kwamba nafsi zao hazijakufa?

Yesu hakufundisha kwamba Mungu angewatesa waovu kwa ukatili milele. Badala ya hivyo, Yesu alisema: “Maana Mungu aliupenda ulimwengu hivi hata akamtoa Mwana wake wa pekee, ili kila amwaminiye asipotee, bali awe na uhai wa milele.” (Yohana 3:16, BHN) Kwa nini Yesu alidokeza kwamba wale wasiomwamini wangekufa? Ikiwa alimaanisha kwamba wangeishi milele wakiteseka katika moto wa mateso, je, hangesema hivyo?

Fundisho la kwamba moto wa mateso ni mahali pa kuwatesa watu halitegemei Biblia. Badala yake, ni fundisho la kipagani linalodaiwa kuwa la Kikristo. (Ona sanduku  “Historia Fupi ya Moto wa Mateso,” kwenye ukurasa wa 6.) La hasha, Mungu hawatesi watu milele katika moto wa mateso. Kujifunza ukweli kuhusu moto wa mateso kutakuwa na matokeo gani kwa maoni yako kumwelekea Mungu?

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

  HISTORIA FUPI YA MOTO WA MATESO

CHANZO CHA KIPAGANI: Wamisri wa kale waliamini kwamba kuna moto wa mateso. Kitabu kimoja (The Book Ȧm-Ṭuat) kinachokadiriwa kuwa cha 1375 K.W.K., kinasema kuhusu wale ambao “watatupwa kichwa chini ndani ya mashimo ya moto; na . . . hawatatoka humo, na . . . hawataweza kuepuka miale ya moto.” Mwanafalsafa Mgiriki Plutarch (karibu 46-120 W.K.) aliandika hivi kuhusu wale walio katika ulimwengu huo wa chini: “Walilia kwa sauti huku wakipatwa na mateso yenye kutisha na adhabu yenye kuaibisha na kuumiza sana.”

LAENEA KATIKA MADHEHEBU YA KIYAHUDI: Mwanahistoria Yosefo (37-karibu 100 W.K.) aliripoti kwamba madhehebu ya Kiyahudi iliyoitwa Waesene, iliamini kwamba “nafsi haziwezi kufa na zitaendelea milele.” Aliongeza hivi: “Hayo yanafanana na maoni ya Wagiriki . . . Wao wanafikiri kwamba nafsi mbaya zinafungwa ndani ya eneo lenye giza, linaloogopesha lililo na adhabu zisizokwisha.”

LAINGIZWA KATIKA “UKRISTO”: Katika karne ya pili W.K., kitabu cha kiapokrifa (Apocalypse of Peter) kilisema hivi kuhusu waovu: “Wametayarishiwa moto usioweza kuzimwa.” Pia kilisema: “Ezrael, malaika wa ghadhabu, anawaleta wanaume na wanawake huku nusu ya miili yao ikiungua na kuwatupa katika eneo la giza, moto wa mateso wa wanadamu; na roho wa ghadhabu anawaadhibu.” Wakati huohuo, mwandishi Theofilo wa Antiokia anamnukuu nabii Mgiriki wa kike Sibyl akitabiri adhabu ya waovu: “Juu yenu moto unaowaka utakuja, nanyi mtateketea kila siku daima dawamu.” Hayo ni baadhi ya maneno ambayo Theofilo anasema ni “ya kweli na yenye manufaa, ya haki, na yenye faida kwa wanadamu wote.”

LATUMIWA KUTETEA JEURI KATIKA ENZI ZA KATI: Inaripotiwa kwamba Malkia wa Uingereza Mary wa Kwanza (1553-1558), anayeitwa pia “Mary Mwuaji” kwa sababu ya kuwateketeza Waprotestanti karibu 300, alisema hivi: “Kwa kuwa baada ya hapa nafsi za wazushi zitakuwa zikiteketea milele katika moto wa mateso, hakuna jambo linalofaa zaidi kwangu kuliko kuiga kisasi cha Mungu kwa kuwateketeza duniani.”

UFAFANUZI WA KISASA: Katika miaka ya karibuni, dini fulani zimebadili msimamo wao kuhusu fundisho la moto wa mateso. Kwa mfano, mnamo 1995 Tume ya Mafundisho ya Kanisa la Anglikana ilisema hivi: “Moto wa mateso si mateso ya milele, bali ni kuchaguliwa kwa mwisho kusikoweza kubadilishwa kwa kile kinachompinga Mungu kabisa hivi kwamba mwisho wake ni kuharibiwa kabisa.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

“ZIWA LA MOTO” NI NINI?

Ufunuo 20:10 inasema kwamba Ibilisi atatupwa ndani ya “ziwa la moto” na ‘kuteswa mchana na usiku hata milele na milele.’ (Union Version) Ikiwa Ibilisi angeteswa milele, Mungu angehitaji kumhifadhi hai, lakini Biblia inasema kwamba Yesu ‘atamharibu.’ (Waebrania 2:14, UV) Ziwa la mfano linalowaka moto linamaanisha “kifo cha pili.” (Ufunuo 21:8) Hiki si kifo kinachotajwa kwanza katika Biblia, yaani, kifo kinachosababishwa na dhambi ya Adamu, kifo ambacho mtu anaweza kufufuliwa. (1 Wakorintho 15:21, 22) Kwa kuwa Biblia haisemi kwamba “ziwa la moto” litawaachilia waliomo ndani yake, basi lazima “kifo cha pili” kiwe kinamaanisha kifo cha aina nyingine, kisicho na tumaini la ufufuo.

Ni katika njia gani wale waliomo katika “ziwa la moto” watateswa milele? Nyakati nyingine, “kutesa” kunaweza kumaanisha “kuzuia” mtu. Wakati fulani Yesu alipowakabili roho waovu, wao walipaaza sauti hivi: “Wewe umekuja hapa kututesa [kutuzuia katika abiso] mbele ya wakati?” (Mathayo 8:29; Luka 8:30, 31; Zaire Swahili Bible) Kwa hiyo, wote waliomo katika “ziwa” hilo watapata ‘mateso’ ya kuzuiwa milele, au “kifo cha pili.”