Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Neno Alikuwa “Mungu” au “mungu”?

Je, Neno Alikuwa “Mungu” au “mungu”?

SWALI hilo linahitaji kuchunguzwa watafsiri wa Biblia wanapotafsiri mstari wa kwanza wa Injili ya Yohana. Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatafsiri hivi mstari huo: “Hapo mwanzo Neno alikuwako, na Neno alikuwa pamoja na Mungu, na Neno alikuwa mungu.” (Yohana 1:1) Biblia nyingine zinapotafsiri sehemu ya mwisho ya mstari huo zinatoa wazo la kwamba Neno alikuwa “wa kimungu” au wazo kama hilo. (A New Translation of the Bible, ya James Moffatt; The New English Bible) Hata hivyo, tafsiri nyingi zinatafsiri sehemu ya Yohana 1:1 hivi: “Na Neno alikuwa Mungu.”—Zaire Swahili Bible.

Sarufi ya Kigiriki na muktadha unatoa uthibitisho wenye nguvu kwamba Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ni sahihi na kwamba “Neno” hapaswi kutambuliwa kuwa “Mungu” anayetajwa mwanzoni mwa mstari huo. Lakini kwa kuwa Kigiriki hakikutumia maneno hususa kuonyesha aina ya kitu au mtu, watu fulani wana maoni yanayotofautiana kuhusu mstari huo. Hii ndiyo sababu tafsiri fulani ya Biblia ya lugha ambayo ilizungumzwa katika karne za kwanza za Wakati wa Kawaida inapendeza sana.

Lugha hiyo ni lahaja ya Kikoptiki inayoitwa Kisahidi. Lugha ya Kikoptiki ilizungumzwa nchini Misri katika karne chache baada ya huduma Yesu duniani, na kati ya lahaja zote za Kikoptiki, lahaja ya Kisahidi ndiyo iliyokuwa lugha ya mapema zaidi kuandikwa. Kamusi moja (The Anchor Bible Dictionary) inasema hivi kuhusu tafsiri za Biblia za mapema zaidi za Kikoptiki: “Kwa kuwa [Septuajinti] na [Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo] yalikuwa yakitafsiriwa katika Kikoptiki katika karne ya tatu W.K., tafsiri ya Kikoptiki ilitegemea [hati za Kigiriki] ambazo ni za kale zaidi kuliko ushahidi mwingi uliopo.”

Maandishi ya Kikoptiki cha Kisahidi yanapendeza kwa njia mbili. Kwanza, kama ilivyoonyeshwa hapo juu maandishi hayo yanaonyesha jinsi Wakristo walivyoelewa mafundisho ya Biblia kabla ya karne ya nne, Utatu ulipoanza kuwa fundisho rasmi. Pili, sarufi ya Kikoptiki inafanana na sarufi ya Kiingereza katika njia moja muhimu. Tafsiri za mapema za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zilikuwa katika Kisiria, Kilatini, na Kikoptiki. Kama vile Kigiriki cha wakati huo, lugha za Kisiria na Kilatini hazitumii maneno hususa kuonyesha aina ya kitu au mtu. Hata hivyo, Kikoptiki kinatumia maneno ya aina hiyo. Zaidi ya hayo, katika maandishi yake (Introduction to Sahidic Coptic), msomi Thomas O. Lambdin, anasema hivi: “Maneno ya Kikoptiki yanayotumiwa kuonyesha maneno hususa na yasiyo hususa ya aina ya mtu au kitu yanafanana sana na matumizi ya maneno kama hayo katika Kiingereza.”

Hivyo, tafsiri ya Kikoptiki inatoa uthibitisho wenye kupendeza wa jinsi andiko la Yohana 1:1 lilivyopaswa kueleweka wakati huo. Tunapata uthibitisho gani? Tafsiri ya Kikoptiki cha Kisahidi inatumia neno lisilo hususa kabla ya neno “mungu” katika sehemu ya mwisho ya Yohana 1:1. Ni wazi kwamba watafsiri hao wa kale walitambua kwamba maneno hayo ya Yohana kwenye Yohana 1:1 hayakumaanisha Yesu ni Mungu Mweza-Yote. Neno alikuwa mungu, lakini si Mungu Mweza-Yote.