Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mashahidi wa Yehova Wanakubali Agano la Kale?

Je, Mashahidi wa Yehova Wanakubali Agano la Kale?

Wasomaji Wetu Wanauliza

Je, Mashahidi wa Yehova Wanakubali Agano la Kale?

Mashahidi wa Yehova wanaiona Biblia kuwa Neno la Mungu na wanakubali Agano la Kale na Agano Jipya kuwa sehemu muhimu. Hata hivyo, wanapendelea kuita sehemu hizo kwa majina yanayofaa zaidi, yaani, “Maandiko ya Kiebrania” na “Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo,” kwa sababu vitabu vya Agano la Kale na Agano Jipya viliandikwa hasa katika lugha za Kiebrania na Kigiriki.

Ingawa hivyo, baadhi ya watu wanaodai kuwa Wakristo hawapendi kukubali vitabu vya Agano la Kale. Wanadai kwamba vinamwonyesha Mungu kuwa mwenye hasira aliyekubali watu wapigane, wauane, na kufanya matendo ambayo hayapatani na Mungu mwenye upendo na mwenye viwango vya maadili anayefunuliwa katika Agano Jipya. Au wanasema kwamba kwa kuwa Agano la Kale linahusu hasa dini ya Kiyahudi, haliwahusu Wakristo hata kidogo. Hata hivyo, kwa kupatana na amri ya Mungu kwenye Kumbukumbu la Torati 12:32 kwamba mtu yeyote asiongeze wala kuondoa chochote kutoka katika Neno lake, je, hizo ni sababu zinazofaa za kutokubaliana na asilimia 75 hivi ya Biblia?

Katika mwaka wa 50 W.K. mtume Mkristo Paulo alipowatembelea wakaaji wa Thesalonike, huko Ugiriki, ‘alijadiliana nao kwa kutumia Maandiko, akieleza na kuthibitisha kwa marejeo kwamba ilikuwa lazima Kristo ateseke na kufufuliwa kutoka kwa wafu.’ (Matendo 17:1-3) Baadhi ya wasikilizaji wake walikubali kuwa Wakristo na baadaye Paulo akawapongeza kwa kusema: “Mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.” (1 Wathesalonike 2:13) Wakati wa ziara hiyo, huenda ni Injili ya Mathayo pekee iliyokuwa imeandikwa kati ya vitabu 27 vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kwa hiyo, bila shaka “Maandiko” ambayo Paulo alitumia kuthibitisha “kwa marejeo” yalikuwa Maandiko ya Kiebrania.

Kwa kweli, waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo walinukuu moja kwa moja kutoka kwa Maandiko ya Kiebrania mara 320 hivi na kwa njia isiyo ya moja kwa moja mara mia kadhaa. Kwa nini? “Kwa maana mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” (Waroma 15:4) Hilo linaonyesha wazi kwamba wale ambao leo wanakubali Biblia nzima wananufaika sana kwa kufanya hivyo.

Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, yanayotegemea msingi uliowekwa na Maandiko ya Kiebrania, ni mwendelezo unaopatana na akili wa Neno la Mungu unaotokezwa na kufunuliwa hatua kwa hatua kwa makusudi ya Mungu. Hayapunguzi umuhimu wa Maandiko ya Kiebrania kwa njia yoyote. Herbert H. Farmer, profesa wa elimu ya kidini katika Chuo Kikuu cha Cambridge anasema kwamba vitabu vya Injili “haviwezi kueleweka bila kuchunguza historia ya watu wa Agano la Kale kama ilivyoandikwa katika Agano hilo.”

Neno la Mungu halihitaji kufanyiwa mabadiliko yoyote. Hata hivyo, “njia ya waadilifu ni kama nuru inayong’aa, inayozidi kuongezeka mpaka mchana mkamilifu.” (Methali 4:18) Kwa kuongeza Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo katika Biblia, Mungu alifunua zaidi jinsi kusudi lake lingetimizwa bila kupunguza thamani ya Maandiko ya Kiebrania. Maandiko yote ni sehemu ya “neno la Yehova [ambalo] linadumu milele.”—1 Petro 1:24, 25.