Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Yesu alifanya kazi gani akiwa seremala?

Baba aliyemlea Yesu alikuwa seremala. Yesu alijifunza kazi hiyo pia. Alipoanza huduma yake akiwa na umri wa “karibu miaka 30,” hakuonwa tu kuwa ‘mwana wa seremala’ lakini yeye mwenyewe alikuwa seremala.—Luka 3:23; Mathayo 13:55; Marko 6:3.

Katika mji wa nyumbani wa Yesu, kungekuwa na uhitaji wa vifaa vya kulima kama vile plau na nira, ambavyo kwa kawaida vilitengenezwa kwa mbao. Vitu vingine ambavyo seremala angetengeneza ni meza, viti, na kabati, vilevile milango, madirisha, na maboriti. Pia, kazi ya seremala ilitia ndani ujenzi.

Katika mfano mmoja, Yohana Mbatizaji alitaja shoka, kifaa ambacho huenda Yesu na maseremala wengine walitumia kukata miti. Baada ya hapo, wangechonga mbao kuwa boriti papo hapo au wangezisafirisha hadi kwenye karakana. Bila shaka, sehemu hiyo ya kazi yao ilihitaji nguvu nyingi. (Mathayo 3:10) Isaya anaorodhesha vifaa vingine vilivyotumiwa na maseremala wa siku zake: “Naye mchongaji wa mti, ameinyoosha kamba ya kupimia; huinakili kwa chokaa nyekundu; huitengeneza kwa chombo kinachoparuza mbao; naye huendelea kuinakili kwa bikari.” (Isaya 44:13) Vitu vya kale vimethibitisha kwamba misumeno ya chuma, nyundo za mawe, na misumari ya shaba ilitumiwa katika nyakati za Biblia. (Kutoka 21:6; Isaya 10:15; Yeremia 10:4) Inapatana na akili kuamini kwamba Yesu alitumia vitu kama hivyo.

“Wenye kutunza akiba” ambao Yesu alitaja katika mojawapo ya mifano yake walikuwa nani, na walifanya kazi jinsi gani?

Yesu alizungumza kuhusu bwana aliyemkemea mtumwa ambaye hakuleta faida yoyote, akisema: “Ulipaswa kuwa umeweka fedha zangu kwa wenye kutunza akiba, na wakati wa kufika kwangu ningekuwa nikipokea kilicho changu pamoja na faida.”—Mathayo 25:27.

Katika siku za Yesu hakukuwa na benki kubwa kama zile zilizopo leo. Hata hivyo, watu waliokopesha pesa walikuwa wakiwalipa faida watu waliowaachia pesa na waliwakopesha watu pesa kwa faida kubwa hata zaidi. Kulingana na kamusi moja (The Anchor Bible Dictionary), mikopo yenye kutozwa faida ilikuwa jambo la kawaida huko Ugiriki kufikia karne ya nne K.W.K. Na katika kipindi cha amani kilichoanzishwa na Waroma, faida ya mwaka mzima katika Milki ya Roma ilikuwa kati ya asilimia 4 hadi 6.

Sheria ya Musa iliwakataza watu kukopesha Waisraeli wenye uhitaji pesa kwa faida. (Kutoka 22:25) Inaonekana kwamba sheria hiyo ilitumika hasa kuhusiana na mikopo kwa maskini. Hata hivyo, kama ilivyoonyeshwa na mfano wa Yesu, ilikuwa kawaida kwa watu walioweka pesa kwa watoaji wa mikopo au “wenye kutunza akiba” kupata faida. Hivyo, kama kawaida, Yesu alitumia mfano uliojulikana na wasikilizaji wake.