Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mshipi Mweusi Ulipofunguliwa

Mshipi Mweusi Ulipofunguliwa

Barua Kutoka Ghana

Mshipi Mweusi Ulipofunguliwa

ANAONEKANA tofauti na jinsi nilivyowazia. Akiwa amevalia nguo ndefu nyeupe ya pamba, na mshipi mweusi wenye upana wa sentimita tano ukiwa umefungwa vizuri kwenye kiuno, anajitayarisha kupigana, mikono ikiwa tayari, miguu isiyo na viatu ikiwa imetengana. Uso wake mkali; na kipaji kinaonyesha amekaza fikira. Macho yake yanatisha, hayana hisia zozote zinazoonyesha udhaifu.

Ghafula anapiga kelele, na kusonga. “Hyaa!” Mkono wake unakata hewa mara moja. Huuu! Mbao kadhaa zinakatika-katika kwa sauti kubwa na kuanguka chini. Anageuka tena, wakati huu akiruka hewani, huku miguu na mikono yake ikisonga haraka na anarusha ngumi na mateke yaliyoelekezwa hasa kumpiga mpinzani bila yeye kutarajia. Je, kweli huyu ndiye mtu aliyeomba funzo la Biblia?

Ninamkaribia nikiwa nimenyoosha mkono. “Nafikiri wewe ni Kojo. Nimesikia kwamba ungependa kujifunza Biblia.” Ananisalimu kwa mkono na kutabasamu sana, uso wake unaonekana mchangamfu na wenye urafiki. Macho yake hayaonekani tena kuwa yenye kutisha, bali anaonekana kuwa mdadisi. “Ndiyo, ningependa sana kujifunza,” anajibu. “Tutaanza lini?”

Tunaketi tukiwa na Biblia na vichapo vyetu kwenye veranda karibu na nyumba yake. Hapa nje hapana joto jingi, ni patulivu, na tunaweza kuwa peke yetu. Tuko watatu hapo nje: mimi, Kojo, na tumbili wake mdogo. Tumbili huyo mdogo ambaye ana urefu wa sentimita 35 tu, na nywele nyekundu kichwani na kidevu chenye nywele nyeupe, anaonekana mwenye kuchekesha na mjanja. Ana sura nzuri, anapenda kucheza, na ni mdadisi sana, anatembea-tembea juu ya karatasi, akichukua kalamu zetu, akiingiza miguu yake midogo ndani ya mifuko ya shati akitafuta kitu kizuri. Kama mzazi aliyezoea kelele za watoto wadogo, Kojo anampuuza na kukazia fikira funzo. Maswali yake mengi yananionyesha kwamba anafikiri na anatamani kujifunza. Huenda karate imemfanya awe mwangalifu kwa kuwa hakubali chochote bila usadikisho na uthibitisho kutoka kwa Maandiko.

Tunaendelea vizuri na funzo letu la Biblia. Hata hivyo, baada ya muda ninaona vita vingine vikianza na mgogoro ndani yake unaoongezeka. “Jambo pekee ninalopenda ulimwenguni ni kupigana,” ananiambia. Ninaona kwamba kupigana kumekolea moyoni mwa mpiganaji huyu, amejitoa kabisa kwa karate. Ingawa ana umri wa miaka 26 tu, anapenda karate naye amekuwa stadi sana hivi kwamba amepewa mshipi mweusi, hatua ya karate ambayo ni watu wachache tu walio nayo au watawahi kuifikia.

Sijui Kojo atafanya nini. Ninahisi anatambua kuwa akiwa mpiganaji wa karate anayewaumiza watu akitumia mikono na miguu yake, hawezi kuwa na sifa za Wakristo wa kweli zinazochochewa na upendo kama vile huruma, wororo na kuwahangaikia watu. Hata hivyo, ninajua kwamba kweli ya Biblia imeyeyusha mioyo ya watu waliokuwa na mioyo migumu zaidi. Ikiwa Kojo ana moyo unaofaa, pole kwa pole moyo wake utayeyushwa na nguvu za Neno la Mungu. Lazima niwe na subira.

Alasiri moja yenye joto, tunapokuwa karibu kumaliza funzo letu, tunasoma Andiko linalomshtua Kojo kama teke lenye nguvu kutoka kwa mpinzani. “Yehova humchunguza mwadilifu na pia mwovu, na mtu yeyote anayependa jeuri nafsi Yake hakika inamchukia,” anasoma. (Zaburi 11:5) “Mtu yeyote anayependa jeuri,” Kojo anarudia kwa sauti ya chini. Macho yake ya rangi ya kahawia ambayo wakati moja hayakuwa tayari kufanya amani, yanaanza kubadilika. Ananiangalia na kuanza kutabasamu. “Nimeamua.”

Sasa mimi na Kojo tunafanya kazi tunayopenda sana, tumejitolea kuwa walimu na kuwafundisha Biblia bila malipo wale watakaosikiliza. Asubuhi ya leo tumepanga kumtembelea kijana anayeitwa Luke.

Tunapoelekea kwake, tunapitia njia nyembamba iliyo na watu wengi katikati ya soko. Mamia ya maduka na wachuuzi wamejaa mitaani wakiuza vitu mbalimbali: pilipili hoho, vikapu vya nyanya zilizokomaa, mbinda, vilevile redio, miavuli, vipande vya sabuni, nywele bandia, vyombo vya upishi, na viatu na nguo zilizotumika. Wasichana wamebeba kwa ustadi mabakuli makubwa ya alumini juu ya vichwa vyao yaliyo na vyakula wanavyouza vyenye vikolezo na pilipili nyingi. Wanapita katikati ya umati wakiwashawishi wanunuzi wenye njaa na supu tamu na vitoweo vya samaki, kaa, na konokono wa kuchomwa. Mbwa, mbuzi, na kuku wanaopiga kelele wanakimbia huku na huku katikati ya miguu ya watu. Kuna kelele za watu na redio, na magari yanapiga honi.

Tunafuata njia ya udongo isiyo na watu wengi kutoka mjini na tunafika kwenye jengo la zamani lililo na ishara inayosema: “Kituo cha Safari Ndefu.” Luke, kijana aliye na umri wa miaka 20 hivi anasimama mlangoni na kutukaribisha ili tujikinge na jua. Chumba chake kimejaa mifuko na masanduku yaliyo na maganda ya miti, majani, na mizizi ya miti-shamba iliyofungwa kwa nyuzi. Vitu hivyo vyote ni vya shangazi yake ambaye ni daktari wa miti-shamba. Ana ujuzi mwingi wa mchanganyiko wa dawa zilizopondwa na kuchemshwa zinazokusudiwa kutibu magonjwa ya aina mbalimbali. Luke amekuwa akitutazamia. Amefagia nyumba na kutayarisha viti vitatu. Tunaketi karibu-karibu na kuanza funzo letu la Biblia.

Kojo ndiye mwalimu wa Luke. Ninaketi na kusikiliza vijana hao wawili wanapozungumzia majibu ya Biblia kuhusu kwa nini watu wanateseka sana duniani. Kojo anapomsaidia Luke kupata andiko katika Biblia, ninatazama mikono yake yenye nguvu ikifungua kwa wororo kurasa nyembamba za Biblia. Kisha ninakumbuka. Juzi tu, mikono hiyo ilikuwa ya mpiganaji. Nguvu za Neno la Mungu zinaondoa sifa mbaya zilizokolea zilizo za kawaida katika ulimwengu huu usio na viwango na kuzigeuza kuwa sifa bora za huruma na upendo. Sidhani kuna mafanikio makubwa kuliko hayo.

Tunapokuwa tukirudi nyumbani, tunazungumza na mwanamume mmoja aliyeketi chini ya mwembe. Anasikiliza kwa makini Kojo anapofungua Biblia na kusoma andiko. Mtu huyo anapotambua kwamba sisi ni Mashahidi wa Yehova anasimama haraka. “Siwapendi ninyi Mashahidi!” anafoka kwa hasira. Kwa muda mfupi, Kojo anapandwa na hasira. Kisha anatulia na kuondoka. Tunaendelea na safari.

Tunapoendelea kutembea Kojo ananiambia kwa sauti ya chini: “Moyo wangu ulikuwa ukipiga kwa nguvu mtu huyo aliponiambia maneno hayo. Unajua ningemfanya nini?” Ninajibu hivi huku nikitabasamu, “Ninajua unachoweza kufanya.” Anatabasamu na tunaendelea na safari.