Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Muumba Anayestahili Sifa Zetu

Muumba Anayestahili Sifa Zetu

Mkaribie Mungu

Muumba Anayestahili Sifa Zetu

Ufunuo 4:11

JE, UMEWAHI kujiuliza, ‘Ni nini kusudi la uhai?’ Wale wanaoamini kwamba uhai unatokana na mageuzi bila kuwa na mbuni mwenye akili wanatafuta jibu la swali hilo bila kufanikiwa. Lakini wale wanaokubali ukweli wa kwamba Yehova Mungu ndiye Chanzo cha uhai wanafaulu kupata jibu hilo. (Zaburi 36:9) Wanajua kwamba alikuwa na kusudi alipotuumba. Kusudi hilo limetajwa katika Ufunuo 4:11. Acheni tuone jinsi maneno hayo yaliyoandikwa na mtume Yohana yanavyoeleza kwa nini tupo hapa.

Yohana anaonyesha umati mbinguni ukimsifu Mungu hivi: “Unastahili, Ee Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako navyo vikaumbwa.” Ni Yehova pekee anayestahili kusifiwa hivyo. Kwa nini? Kwa sababu ‘aliumba vitu vyote.’ Basi, viumbe wake wenye akili wanapaswa kuchochewa kufanya nini?

Yehova anasemekana kuwa anastahili “kupokea” utukufu, heshima, na nguvu. Bila kupingwa, yeye ndiye Mtu mtukufu, mwenye kuheshimika, na mwenye nguvu zaidi ulimwenguni. Hata hivyo, wanadamu wengi hawatambui kwamba yeye ndiye Muumba. Lakini, kuna wale ambao wanaona “sifa zake [Mungu] ambazo hazionekani” kupitia vitu alivyoumba. (Waroma 1:20) Wakiwa na mioyo iliyojaa shukrani, wanachochewa kumpa Yehova utukufu na heshima. Wanawatangazia wote watakaosikiliza uthibitisho wa kwamba Yehova ndiye aliyefanya vitu vyote kwa njia ya ajabu na hivyo anastahili kuheshimiwa sana.—Zaburi 19:1, 2; 139:14.

Lakini Yehova anapokea nguvu kutoka kwa waabudu wake jinsi gani? Bila shaka, hakuna kiumbe kinachoweza kumpa nguvu Muumba mweza-yote. (Isaya 40:25, 26) Hata hivyo, kwa sababu tumeumbwa kwa mfano wa Mungu, tuna kiasi fulani cha sifa za Mungu, na sifa yake moja ni nguvu. (Mwanzo 1:27) Ikiwa kweli tunathamini yale ambayo Muumba wetu ametufanyia, tutachochewa kutumia nguvu zetu kumheshimu na kumtukuza. Badala ya kutumia nguvu zetu kuendeleza mapendezi yetu, tunahisi kwamba Yehova Mungu anastahili kupokea nguvu zetu zote tunapomtumikia.—Marko 12:30.

Basi kwa nini tupo hapa? Sehemu ya mwisho ya Ufunuo 4:11 inajibu: “Kwa sababu ya mapenzi yako [viumbe vyote] vilikuwako navyo vikaumbwa.” Hatukujiumba wenyewe. Tupo hapa kwa sababu ya mapenzi ya Mungu. Kwa sababu hiyo, maisha yanayotumiwa tu kwa ajili ya faida za kibinafsi ni matupu na hayaridhishi. Ili kupata amani ya ndani, shangwe, na uradhi, tunahitaji kujifunza kusudi la Mungu ni nini na kupatanisha maisha yetu na kusudi hilo. Hapo tu ndipo tutakapojua kwa nini tuliumbwa.—Zaburi 40:8.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 31]

NASA, ESA, and A. Nota (STScI)