Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nilitafuta Makosa Nikapata Kweli

Nilitafuta Makosa Nikapata Kweli

Nilitafuta Makosa Nikapata Kweli

Limesimuliwa na R. Stuart Marshall

“Hatuzungumzi na Mashahidi wa Yehova,” alisema kasisi Mjesuti. “Wanatumia Biblia.” Jibu lake lilinishangaza kwani nilikuwa nimemwomba amsaidie mke wangu kwa kumwonyesha mafundisho yanayopingana ya Mashahidi wa Yehova. Niliamua kujifunza Biblia na Mashahidi ili nimwonyeshe tofauti hizo.

NI WAKATI huo, nilipokuwa na umri wa miaka 43, nilipotaka kupinga mafundisho ya Mashahidi wa Yehova kwa kutumia ujuzi wangu wa mambo yanayopatana na akili na theolojia. Tangu shule ya nasari hadi chuo nilisomea katika shule za Wakatoliki. Ingawa nilipata digrii ya mambo ya uchumi mnamo 1969 na kujifunza falsafa na theolojia kwa sababu ilikuwa lazima, masomo yangu ya Kikatoliki hayakutia ndani kujifunza Biblia.

Baada ya kuhitimu, nilimwoa Patricia McGinn ambaye alikuwa Mkatoliki pia. Kisha sote wawili tulipata digrii katika Chuo Kikuu cha Stanford. Mwana wetu Stuart, alizaliwa mnamo 1977, na hatimaye tukahamia Sacramento, California, huko Marekani. Kwa miaka 23 iliyofuata, nilifanya kazi ya jimbo la California katika Ofisi ya Mchunguzi wa Mambo ya Kisheria (LAO), nikichunguza kiasi cha pesa kilichohitajika katika masomo yaliyogharimiwa na jimbo hilo. Nilifanya kazi kwa bidii na kufurahia maisha mazuri. Nilifurahia kuwa baba mzuri mwana wetu alipokuwa akikua. Mke wangu mpendwa alinitegemeza sana, nami nilimtegemeza pia.

Jibu la Senti 25

Mwana wetu alipokuwa na umri wa miaka miwili, Patricia alipata Biblia kutoka kwa Mashahidi wa Yehova na akaanza kujifunza nao. Alibatizwa miaka mitatu baadaye. Nilifikiri kwamba Mashahidi wa Yehova walikuwa na maoni yasiyofaa kuhusu sikukuu na kutiwa damu mishipani, hata hivyo, nilifurahia jinsi walivyotoa sababu zenye kusadikisha kuhusu mambo fulani. Siku moja mnamo 1987, nilishangaa kujikuta nikieleza hisia zangu nilipoombwa nitoe ushahidi mbele ya kamati ya bunge inayosimamia elimu katika jimbo letu kuhusu pendekezo fulani nililotoa.

Chuo Kikuu cha California kilihitaji pesa za kushindana na majimbo mengine ili kiruhusiwe kusimamia mradi ambao ungegharimu dola bilioni sita. Mradi huo ungehusisha kujenga kifaa kikubwa sana kwa ajili ya uchunguzi wa kisayansi. Nilikuwa nimependekeza wasipewe pesa hizo, na kusema kwamba mradi huo haungesaidia sana uchumi wa nchi yetu. Chuo kikuu kilinipinga na kikaleta washindi wawili wa Tuzo ya Nobeli katika fizikia watoe ushuhuda mbele ya kamati hiyo. Kila mmoja wao alieleza jinsi mradi huo ungetusaidia kupata ujuzi muhimu. Mmoja alisema kwamba mradi huo ungejibu maswali kuhusu chanzo cha ulimwengu. Mwingine alisema ungesaidia kujua jinsi uhai ulivyoanza duniani.

Mwenyekiti alinigeukia.

“Unafikiri dola bilioni sita ni pesa nyingi sana ili mtu apate majibu ya maswali hayo?” aliuliza.

“Ninakubali kwamba hayo ni maswali muhimu,” nikajibu. “Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova wanakuja kwangu kila Jumamosi (Siku ya Posho) asubuhi na kunipa gazeti kwa mchango wa senti 25 [za Marekani] na magazeti hayo yanajibu maswali hayo. Huenda jibu lao la senti 25 ni bora kuliko majibu tutakayopata kwa dola bilioni sita.”

Kila mtu chumbani aliangua kicheko, kutia ndani washindi wa Tuzo ya Nobeli. Ingawa kamati hiyo ilitoa pesa za kugharimia mradi huo, hakuna mtu aliyekataa hoja yangu.

Kadiri wakati ulivyopita, nilianza kuona uhitaji wa kushughulikia hali fulani nyumbani. Baada ya miaka sita ya kuwa na mazungumzo na Patricia kuhusu Biblia na Mashahidi wa Yehova, nilivunjika moyo aliposema anataka kutumia wakati mwingi zaidi katika huduma. Hilo lilihusisha kupunguza wakati aliotumia katika chuo kikuu. Nilikatishwa tamaa na wazo la kwamba mtu anaweza kujiwekea mradi kama huo, lakini ilionekana kwamba hakuna jambo ambalo ningesema au kufanya ili kubadili nia yake.

Nilijaribu kupata msaada kutoka kwa mtaalamu mmoja, mtu ambaye alikuwa na ujuzi zaidi kuhusu Biblia kuliko mimi, mtu ambaye nilifikiri angeweza kuonyesha tofauti zilizopo kati ya mafundisho ya Mashahidi wa Yehova na yale ya Biblia. Ikiwa angethibitisha fundisho moja tu kuwa kosa basi mengine yote yangetiliwa shaka. Hilo tu ndilo ningehitaji ili kubadili akili ya mke wangu. Niliwasiliana na kasisi Mjesuti wa kanisa ambalo mimi na Patricia tulikuwa tumehudhuria. Mazungumzo yetu yalikwisha kwa maneno yaliyotajwa mwanzoni mwa simulizi hili. Kasisi huyo alipokataa kuzungumza na mke wangu, nilijua kwamba ingawa ingenichukua muda mrefu zaidi, mimi mwenyewe ningepata tofauti hizo katika mafundisho na kumwonyesha Patricia.

Natafuta Makosa

Nilipojifunza Biblia na Mashahidi nilipendezwa hasa na unabii wa Biblia. Nilisoma habari hususa kuhusu kuanguka kwa Babiloni katika unabii wa Isaya ulioandikwa karibu miaka 200 kabla ya tukio hilo, na kumtaja Koreshi kwa jina kuwa mshindi na kufafanua mbinu ya kubadili mkondo wa Mto Efrati ili kushinda Babiloni. (Isaya 44:27–45:4) Miaka mingi mapema, nilikuwa nimejifunza kuhusu kuanguka kwa Babiloni katika darasa la mbinu za kijeshi. Pia, nilijifunza kwamba nabii Danieli alikuwa ametabiri zaidi ya miaka 200 mapema habari hususa kuhusu mfalme mwenye nguvu wa Ugiriki ambaye ufalme wake ungegawanywa katika falme nne zisizo na nguvu kama zake baada ya kifo chake. (Danieli 8:21, 22) Nilikumbuka jambo hilo kumhusu Aleksanda Mkuu kutokana na masomo yangu ya historia. Kupitia utafiti wa kibinafsi katika vitabu vya marejeo, nilijithibitishia kwamba vitabu vya Biblia viliandikwa kabla ya matukio hayo yaliyotabiriwa.

Kadiri nilivyojifunza na Mashahidi ndivyo nilivyosadikishwa kwamba Biblia ni Neno la Mungu, jambo ambalo masomo yangu ya miaka mingi ya theolojia ya Kikatoliki hayakuwa yamethibitisha. Ningetumia ujuzi huo jinsi gani? Niliamua kuweka maisha yangu wakfu kwa Yehova na kuwa mmoja wa Mashahidi wake. (Isaya 43:10) Nilibatizwa mnamo 1991, miaka miwili tu baada ya mazungumzo yangu na kasisi. Mwana wetu alibatizwa mwaka uliofuata.

Tukiwa tumebadili mtazamo wetu, tulibadili miradi ya familia pia. Mojawapo ya mambo ya kwanza niliyofanya baada ya kubatizwa ni kumwekea mke wangu mradi wa kuacha kazi ya kufundisha katika chuo kikuu baada ya miaka mitano alipotimia umri wa miaka 50. Alitaka kuwa painia, yaani, mhudumu ambaye wakati huo alitumia saa 1,000 kwa mwaka, au karibu saa 83 kwa mwezi, ili kuwasaidia wengine kujifunza kweli za Biblia. Kufikia mwaka wa 1994, alikuwa amepunguza muda aliofanya kazi hivi kwamba angeweza kuwa painia. Miradi yangu ya mwanzoni ilitia ndani kuboresha utumishi wangu, kusaidia mahali popote ambapo ningeweza katika kutaniko letu, na kujitolea kufanya kazi ya hesabu kwa ajili ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme katika eneo letu.

Mara kwa mara, nilipata nafasi ya kuzungumzia Biblia nilipokuwa kazini. Mchanganuzi mpya wa bajeti kwenye LAO alikuwa Shahidi ambaye hakuwa akifuatilia imani yake kwa bidii. Imani yake ilififia kwa sababu ya kutilia shaka mafundisho ya Biblia. Nilifurahi sana kumsaidia kiroho. Alirudi kwenye jimbo la nyumbani kwao na akaanza kufanya upainia.

Mnamo 1995, nilikuwa nikihudhuria mkutano wa pekee wa kamati ya bunge inayosimamia elimu kuhusu utafiti wa kiserikali. Msimamizi wa kamati hiyo aliuliza mwakilishi wa serikali kuhusu mradi ule wa kifaa kikubwa sana cha uchunguzi wa kisayansi. Mwakilishi huyo alijibu kwamba jimbo la Texas ndilo lilipewa jukumu la kusimamia mradi huo lakini haukuwahi kumalizwa kwa sababu tatu. Kwanza, hata kabla ya mradi huo kuanza, gharama zake ziliongezeka kutoka dola bilioni sita hadi bilioni tisa. Pili, serikali ilitaka pesa zitumiwe kwenye mradi mwingine, hasa kwenye vita vya 1991 vya Iraki. Tatu, waligundua kwamba wanaweza kupata majibu kuhusu maswali ya maisha kutoka kwa Mashahidi wa Yehova kwa senti 25 tu! Inaonekana kwamba maneno yangu yalikuwa yamezunguka na mwishowe yakanirudia.

Huku kila mtu akicheka, washiriki fulani wa kamati hiyo walinitazama. Niliwaambia hivi ili niwapashe habari za karibuni zaidi, “Sasa mnaweza kupata majibu hayo bila malipo mkisoma vichapo vyao.”

Maisha Kamili na Yenye Kusudi

Mke wangu alipostaafu, tulifanya mipango ya miaka mitano kwa ajili yangu. Nilichunguza ni mashirika gani yanayoweza kunipa kazi ya muda kwa sababu sasa nilitaka kutumia wakati mwingi zaidi kuwafundisha wengine kweli za Biblia. Bila kutarajia, LAO ilinipa kazi ya muda. Hivyo, mnamo 1998, nikawa painia.

Asubuhi moja mimi na mke wangu tulipokuwa tukijitayarisha kwenda kuhubiri, nilipigiwa simu kutoka kwa ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Brooklyn, New York, Marekani. Kutokana na uchunguzi uliokuwa umefanywa mapema, ndugu aliyepiga simu aliniuliza ikiwa ningependa kusaidia katika mradi fulani huko Brooklyn. Nilijibu ndiyo. Kwa sababu hiyo tukafanya kazi kwa miezi 18 katika makao makuu. Ilinibidi nistaafu mapema kutoka kazi ya serikali ya jimbo la California ili nimalize mradi huo. Baada ya hapo, tulijitolea kusaidia ujenzi wa Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Fairfield, California. Tuliuza nyumba yetu huko Sacramento na kuhamia nyumba ndogo huko Palo Alto. Kustaafu huko kwa mapema kulifungua njia ya kupata baraka zaidi. Tangu wakati huo tumeshiriki katika miradi mbalimbali ya ofisi za tawi za Mashahidi wa Yehova huko Nigeria, Afrika Kusini, Kanada, Uingereza, na Ujerumani.

Kama Mashahidi waliotusaidia, mimi na mke wangu sasa tunafurahia kuwasaidia wengine wajifunze kweli za Biblia. Kwa unyoofu ninahisi kwamba elimu ambayo nimepata kutoka kwa Yehova ndiyo elimu bora zaidi ya juu ambayo nimewahi kupata. Haiwezi kulinganishwa na elimu nyingine duniani kwa sababu ina habari nyingi sana zinazofundishwa kwa undani. Yehova amewazoeza Mashahidi wake kufundisha kweli za Biblia katika njia inayogusa akili na mioyo. Hilo ndilo linalonichochea niendelee kujifunza. Mimi na mke wangu tunathamini sana uhai tulio nao sasa na pendeleo la kutumia elimu yetu kumtumikia Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu, Yehova Mungu.

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Nilipojifunza Biblia na Mashahidi nilipendezwa hasa na unabii wa Biblia

[Picha katika ukurasa wa 27]

Nikiwa na Patricia siku ya arusi yetu

[Picha katika ukurasa wa 29]

Tunafurahia kuwasaidia wengine wajifunze kweli za Biblia