Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Uhuru wa Kweli kwa Wamaya

Uhuru wa Kweli kwa Wamaya

Uhuru wa Kweli kwa Wamaya

NI NANI ambaye hajawahi kusikia kuhusu Wamaya? Kila mwaka maelfu ya watalii wanatembelea Rasi ya Yucatán huko Mexico ili kujionea piramidi zenye kupendeza, kama zile zilizoko Chichén Itzá na Cobá. Wamaya walikuwa watu wenye ustadi si tu katika kazi zao za ufundi bali pia katika maandishi, hesabu, na elimu ya nyota. Walianzisha mfumo wa hali ya juu wa kuandika kwa kutumia michoro, dhana ya sufuri, na kalenda ya siku 365 ikiwa na masahihisho yanayofanana na mwaka mrefu.

Hata hivyo, mambo ya kidini yalikuwa tofauti kabisa. Wamaya waliabudu miungu mingi; waliabudu miungu ya jua, mwezi, mvua, na mahindi, kati ya vitu vingine vingi. Viongozi wao wa kidini walichunguza nyota kwa makini. Ibada yao ilitia ndani matumizi ya uvumba, mifano, kujikata-kata, na mazoea ya kutoa wanadamu dhabihu, hasa wafungwa, watumwa, na watoto.

Wahispania Wawasili

Huo ndio utamaduni ambao Wahispania walipata mapema katika karne ya 16. Wavumbuzi Wahispania walikuwa na malengo mawili: kupata nchi mpya na utajiri na pia kuwageuza Wamaya wawe Wakatoliki ili kuwaweka huru kutokana na mazoea ya kipagani. Je, ushindi wa Wahispania uliwaletea Wamaya uhuru wa kweli, iwe ni wa kidini au kwa njia nyingine?

Wahispania, kutia ndani viongozi wa Kanisa Katoliki, walichukua ardhi ambayo Wamaya walikuwa wametumia tangu zamani kwa ajili ukulima uliohusisha kufyeka na kuchoma miti na majani ili kupanda mimea. Hilo lilisababisha hali ngumu sana na uhasama. Pia, wakoloni walidhibiti visima ambavyo vilikuwa chanzo pekee cha maji kwenye Rasi ya Yucatán. Hali ngumu hata zaidi zilitokea kanisa lilipoanza kutoza Wamaya kodi kila mwaka ya reale * 12 1/2 kwa kila mwanamume na reale 9 kwa kila mwanamke. Kodi hiyo iliongezwa kwenye ile kodi ya kitaifa ambayo tayari ilikuwa imewalemea. Wahispania waliomiliki nchi walitumia vibaya hali hiyo kwa kuwalipia Wamaya kodi ya kanisa, kisha wakawalipisha deni hilo kwa kuwafanyisha kazi kama watumwa.

Pia, makasisi walitoza watu ada fulani kwa ajili ya huduma za kidini, kama vile ubatizo, ndoa, na mazishi. Kanisa lilijitajirisha huku Wamaya wakizidi kuwa maskini kwa sababu kanisa lilikuwa limenyakua ardhi yao, lilikuwa likiwatoza kodi, na ada. Wamaya walionwa kuwa washirikina na wapumbavu. Hivyo, makasisi na watawala wengine waliona kuwa ni jambo linalofaa kuwachapa Wamaya ili kuwafundisha adabu na kuwasaidia waache ushirikina.

Vita Kati ya Wamaya na Wahispania

Kwanza, Wamaya walijilipizia kisasi kwa kukataa kulipa kodi ya kanisa, kuwatoa watoto wao kutoka shule za makanisa, kutohudhuria mafunzo ya katekisimu, na kukataa kufanya kazi kwenye mashamba. Lakini hilo lilitokeza mateso zaidi. Mnamo 1847, baada ya miaka 300 hivi ya utawala wa Kihispania, hali ikawa mbaya zaidi. Wamaya walipigana na “wazungu.”

Viongozi wa waasi walitumia sanamu iliyoitwa Msalaba Unaozungumza, yaani, msalaba uliotumiwa kueneza ujumbe wa kuwahimiza Wamaya wapigane hadi kifo. Wamaya wengi walikufa katika vita hivyo. Kufikia 1853, wakati ambapo vita hivyo viliisha rasmi, asilimia 40 hivi ya Wamaya wa Yucatán walikuwa wameuawa. Katika miaka 55 iliyofuata, uhasama uliendelea na walipigana mara kwa mara. Mwishowe, Wamaya walifaulu kupata uhuru kutoka kwa Wahispania na ardhi iligawanywa upya. Namna gani kuhusu uhuru wa kidini?

Hakuna Uhuru wa Kweli

Ukatoliki ulioletwa na Wahispania na vile vita kati ya Wahispania na Wamaya havikuleta uhuru wa kweli. Leo, kuna aina fulani ya dini inayounganisha utamaduni wa kabla ya enzi ya Wahispania na itikadi za Wakatoliki.

Kitabu kimoja (The Mayas—3000 Years of Civilization) kinasema hivi kuhusu Wamaya wa siku hizi: “Wamaya wanaabudu miungu yao ya zamani ya nguvu za asili na mababu wa kale kwenye mashamba, mapango, na milimani . . . na wakati uleule wanaabudu watakatifu kanisani.” Hivyo, mungu Quetzalcoatl, au Kukulcán analinganishwa na Yesu, na mungu wa kike wa mwezi analinganishwa na Bikira Maria. Isitoshe, badala ya kuabudu mti mtakatifu wa sufi wanaabudu msalaba na bado watu wanaunyunyizia maji kana kwamba ni mti halisi. Badala ya kuwa na mfano wa Yesu, misalaba ina maua ya msufi.

Hatimaye Uhuru wa Kweli!

Katika miaka ya karibuni, Mashahidi wa Yehova huko Mexico wamekuwa na kampeni ya kuwafundisha Wamaya Biblia. Vichapo vya Biblia, kama vile gazeti hili, vinapatikana katika lugha ya mama ya Wamaya ili kuwasaidia kuwa na uelewaji wa kusudi la Mungu kwa wanadamu. Matokeo yamekuwa nini? Gazeti hili lilipokuwa likiandikwa, kulikuwa na wahubiri 6,600 hivi katika makutaniko 241 ya Mashahidi wa Yehova wanaozungumza lugha ya Wamaya na wanaohubiri habari njema za Ufalme katika eneo hilo. Je, imekuwa rahisi kwa Wamaya kujiweka huru kutokana na imani zao za kitamaduni ili wakubali kweli za Biblia?

Wamaya wengi wamehitaji kufanya jitihada nyingi. Marcelino na mke wake, Margarita, walijiona kuwa Wakatoliki wenye bidii. Kila mwaka, waliabudu msalaba kwa kuubeba kutoka kanisani hadi nyumbani kwao ambako walitoa dhabihu za wanyama na baadaye kula dhabihu hizo pamoja na watu wa ukoo na marafiki. Kisha wakatembelewa na Mashahidi wa Yehova na wakaanza kujifunza Biblia pamoja nao. “Tulitambua kwamba mambo tuliyokuwa tukijifunza ni ya kweli,” wanakumbuka, “lakini tulidhani kwamba ikiwa tungeacha imani tuliyokuwa nayo, tungeshambuliwa na roho waovu.” Hata hivyo, waliendelea na funzo lao la Biblia. “Pole kwa pole, kweli ya Biblia ilitugusa moyo,” anasema Marcelino. “Hiyo ilitupa ujasiri wa kuzungumza na watu wa familia na marafiki kuhusu mambo tuliyojifunza kutoka kwa Biblia. Sasa tunafurahi kuwa huru kutokana na imani za ushirikina tulizofuata. Tunasikitika tu kwamba hatukuanza mapema. Kwa sababu hapo mbeleni hatukumfahamu Yehova, sasa tunataka kufanya mengi zaidi kwa kuwa na bidii ya kuwaambia wengine kuhusu kweli nzuri zinazopatikana katika Biblia.”

Alfonso mwenye umri wa miaka 73, alikuwa Mkatoliki mwenye bidii. Alikuwa akipanga sherehe za kidini mjini ambazo zilitia ndani Misa, kucheza dansi, na kuandaa vyakula na vinywaji kwa ajili ya wahudhuriaji wote. Pia, kulikuwa na mchezo wa kupigana na fahali. “Kwa kawaida, mwishoni mwa sherehe hizo kulikuwa na ugomvi unaotokana na ulevi,” anasema. “Ingawa nilifurahia sherehe hizo, nilihisi kwamba dini yangu ina kasoro fulani.” Mashahidi wa Yehova walipomhubiria Alfonso, alikubali kujifunza Biblia. Ingawa alikuwa na matatizo ya afya, alianza kuhudhuria mikutano katika Jumba la Ufalme. Sasa ameacha mazoea yake ya awali ya kidini na anatumia nafasi zote kuwaeleza wengine wanaomtembelea nyumbani kuhusu imani yake mpya.

Hiyo ni mifano michache tu kati ya Wamaya wengi wanyoofu waliopata uhuru wa kweli wa kidini. Naam, wazao wa wajenzi wa piramidi za Yucatán zenye kupendeza bado wanaishi katika eneo hilo. Bado wanazungumza lugha ileile ya mababu zao. Wengi wao wanaishi kama mababu zao walivyoishi, katika nyumba za udongo zilizilizoezekwa kwa makuti. Wanapanda mahindi na pamba kwa kutumia njia ileile ya ukulima ya kufyeka na kuchoma miti na majani. Lakini sasa kweli za Neno la Mungu zimewaweka Wamaya wengi huru kutokana na uwongo wa kidini na ushirikina. Wanathamini kabisa maneno yenye nguvu ya Yesu: “Mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.”—Yohana 8:32.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Reale ni fedha za zamani za Kihispania.

[Ramani katika ukurasa wa 13]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Eneo lililomilikiwa na Wamaya

Ghuba ya Mexico

MEXICO

Rasi ya Yucatán

Chichén Itzá

Cobá

BELIZE

GUATEMALA

EL SALVADOR

HONDURAS

[Picha katika ukurasa wa 13]

Magofu katika eneo la Wamaya, Chichén Itzá

[Picha katika ukurasa wa 15]

Marcelino na mke wake, Margarita, wakihubiri habari njema huko Yucatán