Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Uponyaji wa Kimuujiza’ Leo—Je, Unatoka kwa Mungu?

‘Uponyaji wa Kimuujiza’ Leo—Je, Unatoka kwa Mungu?

‘Uponyaji wa Kimuujiza’ Leo—Je, Unatoka kwa Mungu?

KATIKA nchi fulani, ni jambo la kawaida kuwaona watu wakisafiri hadi kwenye sehemu wanazoona kuwa takatifu ambako wengi wanadai kuna nguvu za kuponya magonjwa “yasiyoweza kupona.” Katika nchi nyingine, waganga wanadai kuwaponya watu kwa kutumia nguvu zinazozidi zile za kawaida. Katika maeneo mengine, mikutano ya kidini inafanywa ambapo watu walio katika viti vya magurudumu wanaruka kutoka kwenye viti vyao au kutupa mikongojo yao na kudai kwamba wameponywa.

Kwa kawaida, wale ambao wanafanya uponyaji huo ni watu wa dini tofauti-tofauti na mara nyingi wao wanawashtaki wenzao kuwa waasi-sheria, waongo, au wapagani. Basi, huenda swali hili likaulizwa, Je, Mungu anafanya miujiza kupitia mashirika mengi ya kidini yanayopingana? Biblia inasema: “Mungu si Mungu wa machafuko, bali ni wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Kwa hiyo, je, ‘uponyaji wa kimuujiza’ unatoka kwa Mungu? Waponyaji wanadai kuwaponya watu katika nguvu za Yesu. Acheni tuchunguze jinsi Yesu alivyoponya.

Jinsi Yesu Alivyoponya

Yesu aliwaponya wagonjwa katika njia tofauti sana na zile zinazotumiwa na waponyaji wa leo. Kwa mfano, Yesu aliwaponya watu wote waliomwendea ili awasaidie. Hakuwaponya tu watu fulani aliochagua katika umati na kuwaambia wengine warudi nyumbani bila kuponywa. Pia, Yesu aliwaponya watu kabisa na mara nyingi alifanya hivyo papo hapo. Biblia inasema: “Umati wote ulikuwa ukitafuta kumgusa, kwa sababu nguvu zilikuwa zikimtoka na kuwaponya wote.”Luka 6:19.

Tofauti na waponyaji wa kimuujiza wa leo ambao mara nyingi wanawalaumu wagonjwa kwa kukosa imani wanapokosa kupona, Yesu aliwaponya watu wengine ambao hata hawakuwa wamemwamini. Kwa mfano, pindi moja Yesu alimkaribia kipofu ambaye hakuwa amemwita na kumponya. Baadaye, Yesu alimwuliza: “Je, unamwamini Mwana wa binadamu?” Mtu huyo akajibu: “Huyo ni nani, bwana, ili nipate kumwamini?” Yesu akamwambia: “Yule anayesema na wewe ndiye huyo.”—Yohana 9:1-7, 35-38.

Huenda ukajiuliza, ‘Ikiwa haikuwa lazima mtu awe na imani ili aponywe na Yesu, kwa nini mara nyingi Yesu aliwaambia watu aliowaponya: “Imani yako imekuponya”?’ (Luka 8:48; 17:19; 18:42) Aliposema hivyo, Yesu alikuwa akionyesha kwamba watu waliochochewa na imani kumtafuta waliponywa, huku watu ambao hawakumtafuta wakipoteza nafasi hiyo. Wale walioponywa hawakuponywa na imani yao; bali waliponywa na nguvu za Mungu. Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Mungu [alimtia] mafuta kwa roho takatifu na nguvu, naye akaenda akipita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote waliokandamizwa na Ibilisi; kwa sababu Mungu alikuwa pamoja naye.”—Matendo 10:38.

Mara nyingi, inaonekana kwamba pesa ndilo jambo kuu katika uponyaji wa kimuujiza wa leo. Waponyaji hao wanajulikana kwa sababu ya kujua kuchangisha pesa nyingi. Iliripotiwa kwamba mponyaji mmoja alichangisha dola milioni 89 (za Marekani) katika mwaka mmoja kupitia kazi yake ya ulimwenguni pote. Mashirika ya kidini pia yanapata pesa kutoka kwa watu wanaotembelea maeneo matakatifu wakitumaini kuponywa. Tofauti na hilo, Yesu hakuwahi kukusanya pesa kutoka kwa watu aliowaponya. Pindi nyingine, hata aliwalisha watu. (Mathayo 15:30-38) Yesu alipowatuma wanafunzi wake wakahubiri, aliwaambia hivi: “Ponyeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, fukuzeni roho waovu. Mlipokea bure, toeni bure.” (Mathayo 10:8) Kwa nini mazoea ya waponyaji wa leo ni tofauti sana na uponyaji wa Yesu?

“Uponyaji” Kutoka kwa Chanzo Gani?

Kwa miaka mingi, wataalamu fulani katika nyanja za matibabu wamechunguza madai ya waponyaji wa kidini. Wamegundua nini? Kulingana na gazeti moja la London (Daily Telegraph), daktari mmoja huko Uingereza aliyefanya uchunguzi kuhusu jambo hilo kwa miaka 20, alisema hivi: “Ripoti zinazoelezewa kwa msisimko mwingi za uponyaji wa kimuujiza haziwezi kuthibitishwa kitiba.” Hata hivyo, watu wengi wanaamini kwa unyoofu kwamba wameponywa na nguvu za mifano, mahali patakatifu, au waponyaji wa kidini. Je, walidanganywa?

Katika Mahubiri ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu alisema kwamba walaghai wa kidini wangemwambia: ‘Bwana, Bwana, hatukufanya matendo mengi yenye nguvu katika jina lako?’ Lakini angewajibu: “Sikuwajua ninyi kamwe! Ondokeni kwangu, ninyi wenye matendo ya uasi-sheria.” (Mathayo 7:22, 23) Mtume Paulo alionya hivi kuhusu chanzo cha nguvu wanazodai kuwa nazo: “Kuwapo kwa huyo mwasi-sheria ni kulingana na utendaji wa Shetani pamoja na kila tendo lenye nguvu na ishara za uwongo na mambo ya ajabu na pamoja na kila udanganyifu usio wa uadilifu.”—2 Wathesalonike 2:9, 10.

Isitoshe, “uponyaji” unaohusianishwa na sanamu na mifano ya kidini hauwezi kutokana na Mungu. Kwa nini? Kwa sababu Neno la Mungu linaamuru hivi waziwazi: “Ikimbieni ibada ya sanamu,” na “Jilindeni na sanamu.” (1 Wakorintho 10:14; 1 Yohana 5:21) “Uponyaji” kama huo ni sehemu ya mbinu za Ibilisi za kuwaondoa watu kutoka kwa ibada ya kweli. Biblia inasema: “Shetani mwenyewe huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.”—2 Wakorintho 11:14.

Kwa Nini Yesu na Mitume Waliwaponya Watu?

Uponyaji wa kweli wa kimuujiza uliorekodiwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ulitambulisha waziwazi kwamba Yesu na mitume walimwakilisha Mungu. (Yohana 3:2; Waebrania 2:3, 4) Pia, uponyaji wa kimuujiza wa Yesu ulitegemeza ujumbe aliohubiri: “Akaenda akizunguka katika Galilaya yote, akifundisha katika masinagogi yao na kuhubiri habari njema ya ufalme na kuponya kila namna ya ugonjwa.” (Mathayo 4:23) Matendo yenye nguvu ya Yesu yalitia ndani kuponya wagonjwa, kulisha umati, kudhibiti nguvu za asili, na hata kufufua wafu. Na yalionyesha kile ambacho atawafanyia wanadamu watiifu chini ya utawala wake wa Ufalme. Hizo zilikuwa habari njema kwelikweli!

Matendo kama hayo yenye nguvu, au zawadi za roho, yalikwisha Yesu na mitume na watu wengine ambao walipokea nguvu hizo kupitia kwao walipokufa. Mtume Paulo aliandika: “Kama kuna zawadi za kutoa unabii, zitaondolewa mbali; kama kuna lugha [zinazozungumzwa kimuujiza], zitakoma; kama kuna ujuzi [uliofunuliwa na Mungu], utaondolewa mbali.” (1 Wakorintho 13:8) Kwa nini? Yakiwa yametimiza kusudi la kumtambulisha Yesu kuwa Masihi aliyeahidiwa na kuonyesha kwamba kutaniko la Kikristo limekubaliwa na Mungu, matendo hayo yenye nguvu, yaliyotia ndani uponyaji, hayakuhitajiwa tena; ‘yaliondolewa mbali.’

Lakini bado miujiza ya Yesu ya uponyaji ina ujumbe muhimu kwetu leo. Tukikazia fikira na kuamini mafundisho ya Yesu kuhusu Ufalme wa Mungu, tunaweza kutazamia wakati unabii huu ulioongozwa na roho ya Mungu utatimizwa kiroho na kimwili: “Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24; 35:5, 6; Ufunuo 21:4.