Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usafi—Kwa Nini Ni Muhimu?

Usafi—Kwa Nini Ni Muhimu?

Usafi—Kwa Nini Ni Muhimu?

Kwa maelfu ya miaka, magonjwa ya kuambukiza na yale yasiyo na tiba yamewaathiri wanadamu. Watu fulani walifikiri kwamba magonjwa hayo yalionyesha kwamba Mungu amekasirika na yalitumwa kuwaadhibu wakosaji. Uchunguzi wa kina uliofanywa kwa karne nyingi umeonyesha kwamba chanzo cha magonjwa hayo ni viumbe wadogo wanaoishi kando yetu.

Watafiti wa kitiba waligundua kwamba panya, mende, nzi, na mbu wanaweza kueneza magonjwa. Pia, waligundua kwamba mara nyingi watu wanafanya iwe rahisi kuambukizwa magonjwa kwa kutodumisha usafi. Inaonekana kwamba uhai wa mtu unategemea kadiri anavyodumisha usafi.

Ni wazi kwamba viwango vya usafi vinatofautiana kwa kutegemea tamaduni na hali za watu. Katika maeneo ambako hakuna maji au mifumo mizuri ya kuondoa maji-taka, ni vigumu kudumisha usafi. Hata hivyo, Waisraeli wa kale walipewa maagizo na Mungu kuhusu usafi walipokuwa wakisafiri jangwani. Hilo lilikuwa eneo gumu sana la kudumisha usafi!

Kwa nini Mungu anapenda usafi? Ni maoni gani yanayofaa kuhusu usafi? Wewe na familia yako mnaweza kufanya nini ili kupunguza magonjwa?

ANAPOTOKA shuleni, mvulana mdogo anayeitwa Max * ambaye anaishi nchini Kamerun anarudi nyumbani. Anaingia nyumbani, akiwa na njaa na kiu, anamkumbatia mbwa wake, anaweka mfuko wake juu ya meza, anaketi chini, na kungoja chakula kwa hamu.

Mama yake akiwa jikoni, anamsikia Max akiingia na anamletea sahani ya wali moto na maharagwe. Lakini anakunja uso anapoona mfuko juu ya meza safi. Anamwangalia mwana wake na kusema, “Maaaax!” Mwana wake anaelewa, anaondoa mfuko huo, na anakimbia kunawa mikono yake. Muda si muda, anarudi kula mlo ambao amekuwa akingoja kwa hamu. “Pole Mama. Nilisahau,” anasema.

Mama anayejali anaweza kufanya mengi katika kudumisha afya na usafi, ingawa anahitaji ushirikiano kutoka kwa familia yote. Kama kisa cha Max kinavyoonyesha, mazoezi ya muda mrefu yanahitajika kwa sababu usafi unahitaji jitihada nyingi na watoto wanahitaji kukumbushwa mara nyingi.

Mama ya Max anatambua kwamba chakula kinaweza kupata uchafu kwa njia nyingi. Hivyo, ananawa mikono kwa uangalifu kabla ya kushika chakula na pia anafunika chakula ili kuzuia kisichafuliwe na wadudu. Kwa kuhakikisha kwamba chakula kinahifadhiwa vizuri na nyumba ni safi na nadhifu, hasumbuliwi sana na panya au mende.

Sababu moja inayomfanya mama ya Max awe mwangalifu sana ni kwamba anataka kumpendeza Mungu. “Biblia inasema kwamba ni lazima watu wa Mungu wawe watakatifu kwa sababu Mungu ni mtakatifu,” anaeleza mama ya Max. (1 Petro 1:16) “Utakatifu ni sawa na usafi,” anaongeza. “Hivyo ninataka nyumba yangu iwe safi, na ninataka familia yangu iwe safi. Bila shaka, hilo linawezekana tu kwa sababu kila mtu katika familia anasaidia.”

Ushirikiano Katika Familia Ni Muhimu

Kulingana na mama ya Max, familia nzima inahusika katika kudumisha usafi. Mara kwa mara, familia fulani zinaketi na kuzungumzia mahitaji yao na marekebisho wanayohitaji kufanya, ndani na nje ya nyumba. Jambo hilo pia linaleta umoja katika familia na linamkumbusha kila mmoja jambo analopaswa kufanya ili kuwatunza wengine katika familia. Kwa mfano, Mama anaweza kuwaeleza watoto wakubwa kwa nini wanapaswa kunawa mikono baada ya kutumia choo, kugusa pesa, na kabla ya kula. Watoto hao wanaweza kuhakikisha kwamba watoto wadogo wanachukua jambo hilo kwa uzito.

Wote katika familia wanaweza kugawiwa majukumu mbalimbali. Huenda familia ikaamua kusafisha nyumba kila juma na kuwa na ratiba ya kuisafisha kabisa mara moja au mbili kwa mwaka. Namna gani nje ya nyumba? Mhifadhi wa mazingira Stewart L. Udall, alisema hivi kuhusu Marekani: “Tunaishi katika nchi inayopoteza umaridadi wake, inayozidi kuwa na sura mbaya, isiyo na maeneo mengi yaliyo wazi, na mazingira yanayozorota kila siku kwa sababu ya uchafuzi na kelele.”

Je, hali za kwenu zinafanana na ufafanuzi huo? Zamani na hata leo katika miji fulani ya Afrika ya Kati, mpiga-mbiu wa mji anapiga kengele ili watu wamsikilize. Kwa sauti kubwa anawakumbusha raia wasafishe mji, wafagie mitaro, wakate matawi ya miti, wang’oe magugu, na washughulikie takataka.

Mifumo ya kuondoa takataka ni tatizo la ulimwenguni pote linalohangaisha serikali nyingi. Manispaa fulani zinachelewa kuokota takataka na hivyo zinarundamana mitaani. Raia wanaweza kuombwa wasaidie. Kwa kuwa Wakristo ni raia wazuri, wao huwa kati ya wale wanaoongoza kutii sheria za Kaisari bila kulalamika. (Waroma 13:3, 5-7) Wakristo wa kweli wako tayari kufanya mengi zaidi ili wasaidie katika jambo hilo. Wanapendezwa na mazingira safi nao wanachukua hatua ya kwanza kufanya usafi, bila kukumbushwa na mpiga-mbiu wa mji. Wanatambua kwamba usafi unaonyesha wamezoezwa vizuri na wana tabia nzuri. Jambo hilo linaanza na kila mtu na kila familia. Kudumisha usafi nyumbani kutachangia afya nzuri na vilevile kuboresha mazingira ya eneo ambalo mtu anaishi.

Usafi wa Kibinafsi Unamtukuza Mungu Tunayemwabudu

Miili yetu inapokuwa safi na tunapovalia kwa njia ya heshima tunaonyesha jinsi tunavyoiona ibada yetu na mara nyingi tunawavutia watu. Kikundi cha vijana 15 hivi wa kiume na kike kiliingia kwenye mkahawa fulani baada ya kuhudhuria kusanyiko la Mashahidi wa Yehova huko Toulouse, Ufaransa. Wenzi fulani wa ndoa waliozeeka waliokuwa wameketi kwenye meza iliyokuwa kando ya vijana hao walitarajia kungekuwa na kelele na wangesumbuliwa. Hata hivyo, walipendezwa na mwenendo mzuri na mazungumzo yenye kupendeza ya vijana hao waliokuwa wamevalia vizuri. Vijana hao walipokuwa wakiondoka, wenzi hao waliwapongeza kwa sababu ya mwenendo wao mzuri na wakamwambia kijana mmoja kwamba si rahisi kuona mwenendo mzuri kama huo siku hizi.

Wageni wanapotembelea ofisi za tawi, ofisi zinazofanya uchapishaji, na makao ya wafanyakazi wa ofisi hizo za Mashahidi wa Yehova mara nyingi wanavutiwa na usafi wanaoona huko. Ni matakwa kwa wajitoleaji wanaofanya kazi na kuishi katika ofisi hizo kuvaa mavazi safi na kuoga kwa ukawaida. Marashi hayawezi kuchukua mahali pa usafi wa kimwili. Wajitoleaji hao ambao ni wahudumu wa wakati wote, wanapowahubiria majirani wao jioni au kwenye miisho ya juma, usafi wao pia unafanya watu wavutiwe na ujumbe wao.

“Iweni Waigaji wa Mungu”

Wakristo wanahimizwa ‘wawe waigaji wa Mungu.’ (Waefeso 5:1) Nabii Isaya aliona maono ya malaika waliosema kuwa Muumba alikuwa “Mtakatifu, mtakatifu, mtakatifu.” (Isaya 6:3) Ufafanuzi huo unakazia usafi wa hali ya juu wa Mungu. Kwa sababu hiyo, Mungu anataka watumishi wake wote wawe safi. Anawaambia hivi: “Muwe watakatifu, kwa sababu mimi ni mtakatifu.”—1 Petro 1:16.

Biblia inawatia moyo Wakristo “wavae mavazi ya heshima.” (1 Timotheo 2:9, Verbum Bible) Haishangazi kwamba katika kitabu cha Ufunuo, “kitani bora, changavu, safi” kinawakilisha matendo ya uadilifu ya wale ambao Mungu anawaona kuwa watakatifu. (Ufunuo 19:8) Kwa upande mwingine, mara nyingi katika Maandiko dhambi inawakilishwa na uchafu au doa.—Methali 15:26; Isaya 1:16; Yakobo 1:27.

Leo, mamilioni ya watu wanaishi katika maeneo ambako ni vigumu kudumisha usafi wa kimwili, kiadili, na kiroho. Suluhisho kamili la tatizo hilo litapatikana wakati Mungu ‘atafanya vitu vyote kuwa vipya.’ (Ufunuo 21:5) Ahadi hiyo itakapotimizwa, uchafu wa aina zote utatoweka milele.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 6 Jina limebadilishwa.

[Sanduku katika ukurasa wa 10]

Mungu Anatazamia Watu Wawe Safi

Walipokuwa jangwani Waisraeli waliagizwa wawe waangalifu kuhusu kuondoa kinyesi cha wanadamu. (Kumbukumbu la Torati 23:12-14) Lazima hilo liwe lilikuwa jambo la kuchosha kwa sababu kambi ilikuwa kubwa, lakini bila shaka lilisaidia kuwaepusha na magonjwa kama vile homa ya matumbo na kipindupindu.

Watu waliamriwa wasafishe au kuharibu kitu chochote kilichogusa wanyama waliokufa. Ingawa huenda hawakuelewa kusudi la sheria hiyo, Waisraeli walisaidiwa kuepuka kuambukizwa magonjwa.—Mambo ya Walawi 11:32-38.

Makuhani walipaswa kusafisha mikono na miguu yao kabla ya kufanya kazi katika maskani. Haikuwa rahisi kujaza beseni la maji lililotengenezwa kwa shaba walilotumia kunawia, lakini ilikuwa lazima kunawa.—Kutoka 30:17-21.

[Sanduku katika ukurasa wa 11]

Vikumbusho Kutoka kwa Daktari

Maji ni muhimu kwa uhai, lakini maji machafu yanaweza kuwa chanzo cha magonjwa na kifo. Dakt. J. Mbangue Lobe, mkuu katika idara ya matibabu katika bandari ya Douala, Kamerun, alitaja mambo fulani muhimu katika mahojiano.

“Chemsha maji ya kunywa ikiwa huna hakika kuwa maji hayo ni safi.” Lakini alionya hivi: “Kutumia kemikali za kuua viini ni sawa lakini kunaweza kutokeza madhara zisipotumiwa vizuri. Nawa mikono yako kwa sabuni na maji kabla ya kula na baada ya kutumia choo. Kipande cha sabuni si bei ghali, hivyo hata maskini wanaweza kununua. Fua nguo zako kwa ukawaida, tumia maji moto ikiwa una matatizo ya ngozi au magonjwa mengine.”

“Usafi ndani na nje ya nyumba unapaswa kuchukuliwa kwa uzito na washiriki wote wa familia,” anaendelea daktari huyo. “Mara nyingi vyoo vinapuuzwa na vinakuwa makao ya mende na nzi.” Akiongezea jambo moja muhimu kuhusu watoto, alionya hivi: “Jihadharini msiogee katika mitaro katika ujirani wenu. Vijito hivyo vina viini hatari. Oga usiku kabla ya kwenda kulala, piga mswaki vizuri usiku, na ujifunike kwa neti ya mbu unapolala.” Wazo kuu ni kwamba unapaswa kufikiria mapema, kuchukua hatua, na kuepuka matatizo.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Kusafisha nguo zako kunasaidia kuzuia matatizo ya ngozi na magonjwa mengine

[Picha katika ukurasa wa 10]

Wakristo wanachukua hatua ya kwanza kusafisha mazingira yao

[Picha katika ukurasa wa 10]

Mama anayejali anaweza kufanya mengi katika kudumisha usafi wa familia yake