Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wakristo wa Mapema na Utamaduni wa Wagiriki

Wakristo wa Mapema na Utamaduni wa Wagiriki

Wakristo wa Mapema na Utamaduni wa Wagiriki

WATU wengi ambao walihubiriwa na Wakristo wa karne ya kwanza walizungumza Kigiriki. Maandiko waliyotumia kutoa uthibitisho kuhusu Yesu yaliandikwa katika Kigiriki. Wengi wa waandikaji walioongozwa na roho ya Mungu kuandika maandishi yaliyokuja kuwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, waliandika katika Kigiriki wakitumia maneno na mifano ambayo watu walioishi katika utamaduni wa Wagiriki walielewa. Hata hivyo, Yesu, mitume wake, na hata waandikaji wa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo hawakuwa Wagiriki. Wote walikuwa Wayahudi.—Waroma 3:1, 2.

Kigiriki kilipata umashuhuri huo jinsi gani katika kueneza Ukristo? Waandikaji Wakristo na wamishonari wa karne ya kwanza walihubiri jinsi gani hivi kwamba ujumbe wao ukawapendeza wasikilizaji waliozungumza Kigiriki? Na kwa nini tupendezwe na sehemu hiyo ya historia yao?

Kuenea kwa Utamaduni wa Wagiriki

Katika karne ya nne K.W.K., Aleksanda Mkuu alishinda Milki ya Uajemi na akashinda sehemu nyingine za ulimwengu. Ili kuwaunganisha watu mbalimbali aliowashinda, yeye na wafalme waliomfuata walitia moyo watu wazungumze Kigiriki na kufuata njia ya Wagiriki ya maisha.

Hata baada ya Roma kushinda Ugiriki na kuiondolea mamlaka yote ya kisiasa, utamaduni wa Wagiriki uliendelea kuwa na uvutano mkubwa juu ya watu katika nchi jirani. Katika karne ya pili na ya kwanza K.W.K., wasomi Waroma walipendezwa na vitu vyote vya Kigiriki, yaani, sanaa, majengo, vichapo, na falsafa, na hivyo kufanya mshairi Horace aseme hivi: “Ugiriki iliyotekwa iliwateka washindi wake.”

Chini ya utawala wa Roma, majiji muhimu kotekote katika Asia Ndogo, Siria, na Misri yalikuwa vituo muhimu vya utamaduni wa Wagiriki. Utamaduni wa Wagiriki ulipenya katika kila sehemu ya maisha, kutia ndani mambo ya serikali, sheria, biashara, viwanda, na hata mitindo ya mavazi. Kwa kawaida, katika majiji mengi ya Kigiriki kulikuwa na ukumbi wa michezo ambako vijana walifanya mazoezi, na pia kulikuwa na ukumbi wa maonyesho wa kuigiza michezo ya Kigiriki.

Mwanahistoria Emil Schürer anasema hivi: “Ingawa walisitasita, baadaye Wayahudi walianza kufuata utamaduni wa Wagiriki pole kwa pole.” Mwanzoni, bidii ya Wayahudi katika ibada yao iliwawezesha kupinga uvutano wowote wa kipagani ulioletwa na utamaduni wa Wagiriki, lakini hatimaye sehemu nyingi za maisha ya Wayahudi ziliathiriwa. Schürer anaendelea kusema kwamba “eneo ndogo lililomilikiwa na Wayahudi lilizungukwa karibu pande zote na maeneo yaliyofuata utamaduni wa Wagiriki na walikutana mara kwa mara kwa sababu za kibiashara.”

Fungu Lililotimizwa na Septuajinti

Wayahudi wengi walipohama na kuishi katika eneo la Mediterania, walijipata wakiishi katika majiji yaliyofuata utamaduni wa Wagiriki ambako lugha ya Kigiriki ilizungumzwa. Wayahudi hao waliendelea na dini ya Kiyahudi na wangesafiri hadi Yerusalemu kwa ajili ya sikukuu za kila mwaka za Kiyahudi. Hata hivyo, baada ya muda, wengi wao walisahau lugha ya Kiebrania. * Hivyo kukawa na uhitaji wa kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika lugha ya Kigiriki iliyozungumzwa na wengi wakati huo. Wasomi Wayahudi, yaelekea walioishi huko Aleksandria, Misri, mji uliokuwa kituo muhimu cha utamaduni wa Wagiriki, walianza kazi ya kutafsiri karibu mwaka wa 280 K.W.K. Hivyo, wakatokeza Septuajinti.

Maandishi ya Septuajinti yamekuwa muhimu sana. Ndiyo yaliyotumiwa kuwasilisha Maandiko ya Kiebrania kwa mataifa ya Magharibi. Bila maandishi hayo, matendo ya Mungu kwa Waisraeli hayangejulikana ikiwa yangebaki katika lugha ambayo haikutumiwa na watu wengi, na maandiko ya Kiebrania hayangesaidia katika kueneza habari njema ulimwenguni pote. Kwa kweli, Septuajinti iliandaa muktadha, mawazo, na lugha iliyowezesha kuwasilisha ujuzi wa Yehova Mungu kwa watu wa malezi mbalimbali. Kwa sababu watu wengi walizungumza Kigiriki, hiyo ikawa lugha bora zaidi ya kueneza kweli kumhusu Mungu ulimwenguni.

Wageuzwa-Imani na Watu Waliomwogopa Mungu

Kufikia karne ya pili K.W.K., Wayahudi walikuwa wametafsiri maandishi yao mengi katika Kigiriki na walikuwa wakiandika maandishi mapya katika lugha hiyo. Hilo lilisaidia sana katika kufanya Watu wa Mataifa wajue historia na dini ya Waisraeli. Wanahistoria wanaripoti kwamba wengi kati ya Watu wa Mataifa “walijihusisha kwa kadiri fulani na jamii za Wayahudi, walishiriki katika ibada za Kiyahudi, na wakafuata sheria za Wayahudi, nyakati nyingine kwa kiwango kikubwa au kwa kiwango kidogo.”—The History of the Jewish People in the Age of Jesus Christ.

Baadhi ya Watu wa Mataifa walifanya maendeleo na kuwa wafuasi wa dini ya Kiyahudi, wakakubali tohara, na wakageuzwa imani. Wengine walifuata sheria fulani za Kiyahudi lakini wakasita kugeuzwa imani. Mara nyingi katika vichapo vya Kigiriki, watu kama hao waliitwa “watu wanaomwogopa Mungu.” Kornelio anaitwa “mtu mwenye kuheshimu na kumwogopa Mungu.” Mtume Paulo alikutana na watu wengi waliomwogopa Mungu walioshirikiana na Wayahudi kotekote katika Asia Ndogo na Ugiriki. Kwa mfano, katika Antiokia ya Pisidia akizungumza na watu waliokuwa wamekusanyika katika sinagogi aliwaita “wanaume, Waisraeli na ninyi wengine ambao mnamwogopa Mungu.”—Matendo 10:2; 13:16, 26; 17:4; 18:4.

Kwa hiyo, wanafunzi wa Yesu walipoanza kuhubiri habari njema katika jamii za Kiyahudi nje ya Yudea, wengi waliosikiliza ujumbe huo walikuwa Wagiriki. Jamii kama hizo ziliwezesha Ukristo kuenea. Ilipokuwa wazi kwamba Mungu aliwapa Watu wa Mataifa tumaini kwa ajili ya wokovu, wanafunzi hao walitambua kwamba machoni pa Mungu “hakuna Myahudi wala Mgiriki.”—Wagalatia 3:28.

Kuwahubiria Wagiriki

Kwa sababu ya dini na viwango vya watu wa mataifa, Wakristo fulani Wayahudi wa mapema walisitasita mwanzoni kuwageuza Watu wa Mataifa waingie katika kutaniko la Kikristo. Hivyo, ilipokuwa wazi kwamba Mungu alikuwa tayari kuwakubali Watu wa Mataifa, mitume na wanaume wazee huko Yerusalemu walisema waziwazi kwamba watu waliogeuzwa imani walihitaji kujiepusha na damu, uasherati, na ibada ya sanamu. (Matendo 15:29) Ilikuwa muhimu kwa watu wote waliofuata njia ya maisha ya Wagiriki watii mwongozo huo kwa sababu jamii ya Wagiriki na Waroma ilijawa na “hamu za ngono yenye kufedhehesha” na ngono za watu wa jinsia moja. Wakristo hawakupaswa kujihusisha katika mazoea kama hayo.—Waroma 1:26, 27; 1 Wakorintho 6:9, 10.

Mtume Paulo ndiye aliyekuwa mashuhuri zaidi kati ya wamishonari wote Wakristo wa karne ya kwanza waliowahubiria watu katika maeneo yaliyotumia lugha ya Kigiriki. Hadi leo, wasafiri huko Athene, Ugiriki, wanaweza kuona bamba la shaba kwenye Areopago ambalo linawakumbusha watu hotuba maarufu ya Paulo katika jiji hilo. Simulizi hilo limerekodiwa katika sura ya 17 katika kitabu cha Biblia cha Matendo ya Mitume. Maneno yake ya kwanza, “Wanaume wa Athene,” yalitumiwa kwa kawaida na wasemaji Wagiriki na yaliwatuliza wasikilizaji wake waliotia ndani wanafalsafa Waepikurea na Wastoiki. Badala ya kuonyesha kwamba ameudhika au kuchambua imani ya wasikilizaji wake, Paulo alitambua kwamba walikuwa na imani ya kidini yenye nguvu. Alizungumza kuhusu madhabahu yao iliyokuwa imeandikwa “Kwa Mungu Asiyejulikana” na kusema kwamba alitaka kuzungumza kuhusu Mungu huyo.—Matendo 17:16-23.

Paulo aliwagusa moyo wasikilizaji wake kwa kutumia mawazo ambayo wangeweza kukubali. Wastoiki walikubaliana naye kwamba Mungu ni Chanzo cha uhai wa wanadamu, kwamba watu wote ni wa jamii moja, kwamba Mungu hayuko mbali nasi, na kwamba uhai wa wanadamu unamtegemea Mungu. Paulo alithibitisha wazo hilo la mwisho kwa kutaja marejeo ya washairi Wastoiki Arato (Phaenomena) na Kleanthe (Wimbo kwa Zeu). Pia, Waepikurea waligundua kwamba walikubaliana na Paulo katika mambo mengi, kutia ndani wazo la kwamba Mungu yuko hai na anaweza kujulikana. Anajitegemea, hahitaji chochote kutoka kwa wanadamu, na haishi katika mahekalu yaliyofanywa kwa mikono.

Wasikilizaji wa Paulo walifahamiana na maneno aliyotumia. Kulingana na chanzo kimoja, “ulimwengu (kosmos),” “uzao,” na “Mungu” ni maneno yaliyotumiwa mara nyingi na wanafalsafa Wagiriki. (Matendo 17:24-29) Paulo hakuwa tayari kuridhiana ili awasaidie. Badala yake, maneno yake ya kumalizia kuhusu ufufuo na hukumu yalipingana na imani zao. Hata hivyo, alibadili ujumbe wake ili uwapendeze wasikilizaji wake walioamini hasa falsafa za wakati huo.

Barua nyingi za Paulo zilielekezwa kwa makutaniko katika majiji ya Wagiriki na koloni za Waroma zilizokuwa zikifuata utamaduni wa Wagiriki. Alitumia mawazo na mifano ambayo ilikuwa ya kawaida katika utamaduni wa Wagiriki katika maandishi hayo yaliyoandikwa katika Kigiriki kizuri. Paulo alitaja michezo, tuzo la mshindi, mtunzaji aliyempeleka mvulana shuleni, na mifano mingine mingi kutokana na maisha ya Wagiriki. (1 Wakorintho 9:24-27; Wagalatia 3:24, 25) Ingawa Paulo alikuwa tayari kutumia maneno ya Kigiriki, alikataa katakata viwango vya maadili vya Wagiriki na mafundisho yao ya kidini.

Kuwa Mambo Yote kwa Watu wa Namna Zote

Mtume Paulo alitambua kwamba ili awahubirie wengine habari njema, alihitaji kuwa “mambo yote kwa watu wa namna zote.” “Kwa Wayahudi nilikuwa kama Myahudi, ili niwapate Wayahudi,” aliandika, na kwa Wagiriki akawa kama Mgiriki ili awasaidie kuelewa makusudi ya Mungu. Bila shaka, Paulo alistahili kufanya hivyo, kwa kuwa alikuwa raia Myahudi kutoka jiji lililofuata utamaduni wa Wagiriki. Wakristo wote leo wanahitaji kufanya jambo kama hilo.—1 Wakorintho 9:20-23.

Mamilioni ya watu leo wanahama kutoka nchi moja hadi nyingine, kutoka utamaduni mmoja hadi mwingine. Hilo linawaletea Wakristo kipingamizi kikubwa kwani wanajitahidi kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu na kutimiza amri ya Yesu ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mathayo 24:14; 28:19) Mara kwa mara, wamegundua kwamba watu wanaposikiliza habari njema katika lugha ya mama, mioyo yao inaguswa na wanaitikia vizuri.

Kwa sababu hiyo, gazeti hili, Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova, linachapishwa kila mwezi katika lugha 169, na gazeti Amkeni! linalotolewa pamoja na hili katika lugha 81. Isitoshe, ili kuwahubiria habari njema watu ambao wamehamia eneo lao, wengi wa Mashahidi wa Yehova wamejitahidi kujifunza lugha mpya, kutia ndani lugha ngumu kama vile Kiarabu, Kichina, na Kirusi. Kusudi ni sawa na lile la karne ya kwanza. Mtume Paulo alieleza jambo hilo vizuri aliposema: “Nimekuwa mambo yote kwa watu wa namna zote, ili kwa vyovyote niwaokoe wengine.”—1 Wakorintho 9:22.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Wayahudi wengi walioishi Yerusalemu walizungumza Kigiriki. Kwa mfano, kulikuwa na wanaume “katika lile lililoitwa Sinagogi la Watu Waliowekwa Huru, na kati ya Wakirene na Waaleksandria na kati ya wale wa kutoka Kilikia na Asia,” ambao huenda walizungumza Kigiriki.—Matendo 6:1, 9.

[Ramani katika ukurasa wa 18]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

Roma

UGIRIKI

Athene

ASIA

Antiokia (ya Pisidia)

KILIKIA

SIRIA

YUDEA

Yerusalemu

MISRI

Aleksandria

Kirene

BAHARI YA MEDITERANIA

[Picha katika ukurasa wa 19]

“Septuajinti” ilisaidia kueneza ujuzi kumhusu Yehova katika karne ya kwanza

[Hisani]

Israel Antiquities Authority

[Picha katika ukurasa wa 20]

Bamba katika Areopago ambalo linawakumbusha watu hotuba maarufu ya Paulo