Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu—Kielelezo Kikamilifu cha Kufuata

Yesu—Kielelezo Kikamilifu cha Kufuata

Yesu—Kielelezo Kikamilifu cha Kufuata

JE, UNGEPENDA kuwa mtu bora na mwenye furaha zaidi? Mtume Petro anaeleza jinsi tunavyoweza kufanya hivyo. Anaandika hivi: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Kwa kweli, tunaweza kujifunza mengi kutoka kwa Yesu Kristo kwa kuwa aliishi maisha yasiyo ya kawaida. Tunapojifunza kumhusu Yesu na kufuata kielelezo chake maishani mwetu, tunaweza kuwa watu bora na wenye furaha zaidi. Acheni tuchunguze kwa ukaribu baadhi ya sifa za mtu huyo mkuu na kuona jinsi mfano wake unavyoweza kutufaidi.

Yesu alikuwa na usawaziko. Ingawa Yesu alisema kwamba “hana mahali popote pa kulaza kichwa chake,” hakuishi wala kupendekeza maisha yasiyo na furaha. (Mathayo 8:20) Alihudhuria karamu mbalimbali. (Luka 5:29) Muujiza wake wa kwanza uliorekodiwa, kugeuza maji kuwa divai safi katika karamu ya arusi, unaonyesha kwamba hakujitenga au kuishi maisha yasiyo na furaha. (Yohana 2:1-11) Hata hivyo, Yesu alionyesha waziwazi ni nini kilichokuwa cha maana zaidi kwake. Alisema: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.”—Yohana 4:34.

Je, umechanganua maisha yako ili uone jinsi unavyoweza kusawazisha mambo ya kimwili unayofuatia na utendaji wako wa kiroho?

Yesu alikuwa mwenye kufikika. Biblia inamfafanua Yesu kuwa mtu mchangamfu na mwenye urafiki. Hakukasirishwa watu walipomwendea wakiwa na matatizo na maswali yenye kutatanisha. Pindi moja umati ulipomzunguka, mwanamke ambaye alikuwa ameteseka kwa miaka 12 aligusa vazi lake, akitazamia kupata msaada. Yesu hakumkemea kwa sababu alifanya tendo ambalo wengine walifikiri kuwa ni la kimbelembele lakini alimwambia hivi kwa fadhili: “Binti yangu, imani yako imekuponya.” (Marko 5:25-34) Watoto pia walijihisi huru kuwa pamoja naye, na hawakuogopa kwamba atawapuuza. (Marko 10:13-16) Mazungumzo yake na wanafunzi wake yalikuwa ya wazi na yenye furaha. Hawakusita kumkaribia.—Marko 6:30-32.

Je, watu wanahisi huru kukukaribia?

Alikuwa na hisia-mwenzi na huruma. Moja kati ya sifa nzuri zaidi za Yesu ilikuwa uwezo wake wa kujitia katika hali za wengine, kuhisi jinsi walivyohisi, na kuwasaidia. Mtume Yohana anasema kwamba Yesu alipomwona Maria akilia kwa sababu ya kifo cha ndugu yake Lazaro, Yesu ‘aliugua rohoni na kutaabika’ na “akatokwa na machozi.” Watazamaji wangeweza kuona jinsi Yesu alivyoipenda familia hiyo, upendo ambao hakuaibika kuonyesha waziwazi. Naye alionyesha huruma nyingi kama nini alipomfufua rafiki yake!—Yohana 11:33-44.

Pindi nyingine, mtu aliyekuwa na ukoma, ugonjwa mbaya uliomfanya atengwe, alimsihi Yesu hivi: “Bwana, ikiwa tu unataka, unaweza kunitakasa.” Yesu aliitikia kwa njia yenye kugusa moyo sana: “Akaunyoosha mkono wake, akamgusa, na kusema: ‘Ninataka. Takasika.’” (Mathayo 8:2, 3) Yesu hakuwaponya watu ili tu atimize unabii. Alitaka kupangusa machozi yao. Kila kitu alichofanya kilipatana na maneno yake ambayo mara nyingi yanakumbukwa zaidi: “Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni wao vivyo hivyo.”—Luka 6:31.

Je, watu wengine wanaweza kuona jinsi unavyowahurumia wengine kupitia matendo yako?

Yesu alikuwa mwenye uelewaji na utambuzi. Ingawa hakufanya makosa yoyote, Yesu hakutazamia ukamilifu kutoka kwa wengine, hakujionyesha kuwa bora kuliko wengine; wala hakutenda bila uelewaji. Wakati mmoja, mwanamke “aliyejulikana jijini kuwa mtenda-dhambi” alionyesha imani na uthamini kwa kuosha miguu ya Yesu kwa machozi yake. Yesu alimruhusu afanye hivyo, naye mwenye nyumba alishangazwa sana na tendo hilo na kumhukumu kwa ukali. Akielewa unyoofu wake, Yesu hakumshtumu mwanamke huyo kwa dhambi zake. Badala yake, alisema: “Imani yako imekuokoa; nenda zako kwa amani.” Kwa sababu ya itikio la Yesu lenye uchangamfu, huenda mwanamke huyo alichochewa kuacha maisha yake ya zamani.—Luka 7:37-50.

Je, watu wanakujua kuwa mtu aliye tayari kupongeza na asiyehukumu haraka?

Hakupendelea na aliwaheshimu watu. Yesu alimpenda sana mwanafunzi Yohana, labda kwa sababu nyutu zao zilipatana au kwa sababu ya mahusiano ya kifamilia. * Hata hivyo, hakumwonyesha upendeleo huku akiwabagua wanafunzi wengine. (Yohana 13:23) Hata Yohana na ndugu yake Yakobo walipoomba mapendeleo katika Ufalme wa Mungu, Yesu alijibu: “Kuketi kwenye mkono wangu wa kuume au kwenye mkono wangu wa kushoto sina haki kutoa.”—Marko 10:35-40.

Sikuzote Yesu aliwaheshimu watu. Hakujihusisha katika ubaguzi ambao watu walikuwa nao katika siku zake. Kwa mfano, wanawake walitendewa kama watu wa hali ya chini kuliko wanaume. Hata hivyo, Yesu aliwaheshimu wanawake. Mara ya kwanza alipojitangaza kuwa Masihi, hakumwambia Myahudi bali alimwambia mwanamke Msamaria. Wasamaria walikuwa watu ambao Wayahudi kwa ujumla waliwadharau na hata hawangewasalimu. (Yohana 4:7-26) Pia, Yesu aliwapa wanawake pendeleo la kuwa mashahidi wa kwanza wa ufufuo wake.—Mathayo 28:9, 10.

Je, unawatendea bila ubaguzi watu wa rangi, jinsia, lugha, au taifa lingine?

Alitimiza wajibu wake akiwa mwana na ndugu. Inaonekana kwamba Yosefu, baba aliyemlea Yesu, alikufa Yesu alipokuwa kijana. Inaelekea kwamba Yesu alimtegemeza mama yake na ndugu na dada zake kwa kufanya kazi ya useremala. (Marko 6:3) Katika saa za mwisho za maisha yake, alimwambia mwanafunzi wake Yohana amtunze mama yake.—Yohana 19:26, 27.

Je, unaweza kumwiga Yesu kwa kutunza madaraka yako ya familia kama alivyofanya?

Yesu alikuwa rafiki wa kweli. Yesu alikuwa rafiki wa pekee. Kwa njia gani? Hakuwakana rafiki zake kwa sababu tu walikosea, hata walipofanya makosa yaleyale kwa kurudia. Wanafunzi wake hakutenda nyakati zote kama alivyotaka. Lakini alithibitika kuwa rafiki yao kwa kukazia fikira sifa zao nzuri badala ya kudhani kwamba wana nia mbaya. (Marko 9:33-35; Luka 22:24-27) Ingawa hakuwalazimisha wakubaliane na maoni yake, aliwaruhusu wajieleze kwa uhuru.—Mathayo 16:13-15.

Zaidi ya yote, Yesu aliwapenda rafiki zake. (Yohana 13:1) Kwa kadiri gani? Alisema: “Hakuna aliye na upendo mkuu kuliko huu, kwamba mtu aitoe nafsi yake kwa ajili ya rafiki zake.” (Yohana 15:13) Je, kuna mtu yeyote anayeweza kuwapa rafiki zake kitu chenye thamani kuliko uhai wake?

Je, wewe unaendelea kuwa rafiki hata wengine wanapokuudhi au kukukasirisha?

Alikuwa jasiri na alitenda kama mwanamume. Yesu alikuwa tofauti sana na picha fulani zinazomwonyesha kuwa mtu dhaifu. Vitabu vya Injili vinasema alikuwa mtu mwenye nguvu na bidii. Mara mbili, Yesu aliwafukuza wafanyabiashara na kuwafanya waondoe bidhaa zao kutoka hekaluni. (Marko 11:15-17; Yohana 2:14-17) Umati ulipokuja kumkamata “Yesu Mnazareti,” kwa ujasiri alijitambulisha na kuwalinda wanafunzi wake, akisema hivi kwa uthabiti: “Mimi ndiye. Kwa hiyo, ikiwa ni mimi mnayetafuta, acheni hawa waende.” (Yohana 18:4-9) Hivyo haishangazi kwamba Pontio Pilato alipoona ujasiri wa Yesu alipokuwa ameshikwa na kutendewa vibaya, alisema: “Tazameni! Mwanamume!”—Yohana 19:4, 5.

Je, wewe unatenda kwa ujasiri unapotambua unachopaswa kufanya?

Sifa hizo na nyingine zenye kutokeza zinamfanya Yesu kuwa kielelezo kikamilifu kwetu. Tutakuwa watu bora na wenye furaha zaidi tukiiga mwenendo wake. Hiyo ndiyo sababu mtume Petro aliwahimiza Wakristo wafuate hatua za Yesu kwa ukaribu. Je, unajaribu kufuata hatua za Yesu kwa ukaribu kadiri unavyoweza?

Si Kielelezo tu cha Kufuata

Hata hivyo, Yesu hakuwa tu kielelezo cha kufuata. Alisema: “Mimi ndiye njia na kweli na uzima. Hakuna anayekuja kwa Baba ila kupitia kwangu.” (Yohana 14:6) Zaidi ya kujulisha ukweli kumhusu Mungu na hivyo kufungua njia ya kumkaribia Mungu, Yesu aliandaa njia ya kuwawezesha watu waaminifu kupata uzima.—Yohana 3:16.

Kuhusu jambo hilo lililomfanya aje duniani, Yesu alisema: ‘Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Kwa kuutoa uhai wake kuwa dhabihu, Yesu aliandaa msingi kwa ajili ya wanadamu kufurahia uzima wa milele. Tunapaswa kufanya nini kibinafsi ili tufaidike na maandalizi hayo? Yesu alieleza: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Ndiyo, kuwa na ujuzi kumhusu Yesu, kuiga maisha yake, na kuwa na imani katika kifo cha kidhabihu ni matakwa ya kupata uzima wa milele. Tunakualika utumie wakati wako kujifunza chanzo cha ujuzi huo, Biblia, na kujitahidi kufuata yale inayosema, kama Yesu alivyofanya. *

Maisha ya Yesu yanatufundisha tunapaswa kuwa watu wa aina gani. Kifo cha kidhabihu kinaweza kutuweka huru kutokana na dhambi na mshahara wake, kifo. (Waroma 6:23) Hali yetu ingesikitisha kama nini bila uvutano wenye nguvu wa Yesu Kristo! Usiruhusu kamwe shughuli na mahangaiko ya maisha yakufanye usiwe na wakati wa kuchunguza na kufuata kwa ukaribu mfano uliowekwa na mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi duniani, Yesu Kristo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Inawezekana kwamba mama ya Yohana, Salome, alikuwa dada ya Maria, mama ya Yesu. Linganisha Mathayo 27:55, 56 na Marko 15:40 na Yohana 19:25.

^ fu. 26 Kwa masimulizi ya kina kuhusu maisha ya Yesu duniani, ona kitabu Yule Mtu Mkuu Zaidi Aliyepata Kuishi, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 7]

▪ Yesu hakupendelea na aliwaheshimu watu wote

▪ Alikuwa rafiki wa kweli

▪ Alikuwa jasiri

Je, unajaribu kufuata hatua za Yesu kwa ukaribu kadiri unavyoweza?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Yesu alikuwa na usawaziko . . .

mwenye kufikika . . .

mwenye huruma