Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yesu—Mambo Ambayo Watu Wanasema Kumhusu

Yesu—Mambo Ambayo Watu Wanasema Kumhusu

Yesu—Mambo Ambayo Watu Wanasema Kumhusu

“Yesu wa Nazareti . . . bila shaka ndiye mtu mashuhuri zaidi katika historia.”—H. G. Wells, mwanahistoria Mwingereza.

“Kristo . . . hana kifani anapolinganishwa na mashujaa wote katika historia.”—Philip Schaff, mwanatheolojia na mwanahistoria aliyezaliwa Uswisi.

NI NANI anayestahili kuitwa mtu mkuu zaidi aliyepata kuishi duniani? Unaweza kupima ukuu wa mtu jinsi gani? Je, ni kwa ufundi wake wa kivita? Kwa nguvu zake za kimwili? Ustadi wake wa kiakili? Au unapaswa kupimwa kulingana na jinsi maneno yake, matendo, na mfano alioweka umekuwa na uvutano juu ya watu?

Ona mambo ambayo wanahistoria, wanasayansi, wasomi, waandishi, wanasiasa, na wengine, wa kale na wa kisasa, wamesema kuhusu yule mtu aliyetoka Nazareti, Yesu Kristo:

“Ungehitaji kupotosha mambo ya hakika ili kupinga kwamba mtu aliye na uvutano mkubwa zaidi, si katika miaka elfu mbili iliyopita tu, bali katika historia yote ya wanadamu ni Yesu wa Nazareti.”—Reynolds Price, mwandishi na msomi wa Biblia Mmarekani.

“Mtu asiye na hatia kabisa alijitoa kuwa dhabihu kwa faida ya wengine kutia ndani adui zake na kuwa fidia kwa ajili ya ulimwengu. Hilo lilikuwa tendo kamilifu.”—Mohandas K. Gandhi, kiongozi wa kisiasa na wa kidini wa India.

“Nilipokuwa mtoto, nilifundishwa Biblia na Talmud. Mimi ni Myahudi, lakini ninastaajabishwa na yule Mnazareti mwenye kutokeza.”—Albert Einstein, mwanasayansi aliyezaliwa Ujerumani.

“Kwa maoni yangu, Yesu Kristo ndiye mtu mwenye kutokeza zaidi katika historia yote, akiwa Mwana wa Mungu na pia Mwana wa Binadamu. Kila kitu Alichowahi kusema na kufanya kina thamani kwetu leo, na hilo ni jambo ambalo hatuwezi kusema kumhusu mtu mwingine yeyote, aliye hai au aliyekufa.”—Sholem Asch, mwandishi aliyezaliwa Poland kama alivyonukuliwa katika gazeti Christian Herald; italiki ni zao.

“Kwa miaka 35, sikuwa na imani katika jambo lolote. Lakini miaka mitano iliyopita nilianza kuwa na imani. Nilianza kumwamini Yesu Kristo na ghafula maisha yangu yote yakabadilika kabisa.”—Count Leo Tolstoy, mwandishi na mwanafalsafa Mrusi.

“Maisha [ya Yesu] yamekuwa na uvutano mkubwa zaidi katika sayari hii na uvutano wake unaendelea kuongezeka.”—Kenneth Scott Latourette, mwanahistoria na mwandishi Mmarekani.

“Je, tunaweza kusema kwamba historia ya maisha ya Yesu ni hadithi ya kubuniwa? Kwa kweli, rafiki yangu, haionekani kuwa imebuniwa. Badala yake, historia ya Sokratesi, ambayo hakuna mtu aliye na shaka kuihusu, haiwezi kuthibitishwa vizuri kama ile ya Yesu Kristo.”—Jean-Jacques Rousseau, mwanafalsafa Mfaransa.

Ni wazi kwamba Yesu Kristo ndiye mtu anayestahili zaidi kuwa kielelezo chetu maishani. Paulo, mwanamume mwenye elimu wa karne ya kwanza aliyechaguliwa na Yesu kuwa mfuasi Wake ili ayafundishe mataifa kumhusu, anatuhimiza ‘tumtazame Yesu kwa makini.’ (Waebrania 12:2; Matendo 9:3) Yesu anaweza kutufundisha nini juu ya jinsi tunavyopaswa kuishi? Maisha yake yanaweza kukufaidi jinsi gani?