Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wafundishe Watoto Wako

Daudi—Kwa Nini Hakuogopa

Daudi—Kwa Nini Hakuogopa

JE, UMEWAHI kuogopa?— * Wengi wetu tunaogopa mara kwa mara. Unaweza kufanya nini unapoogopa?— Unaweza kumwomba msaada mtu mkubwa na mwenye nguvu kuliko wewe. Labda baba au mama yako anaweza kukusaidia. Tunaweza kujifunza mengi kutoka kwa Daudi kuhusu mahali tunapoweza kupata msaada. Alimwimbia Mungu hivi: “Mimi nitakutegemea wewe. . . . Nimeliweka tegemeo langu kwa Mungu; sitaogopa.”—Zaburi 56:3, 4.

Unafikiri Daudi alijifunza kutokuwa mwoga kutoka kwa nani? Kutoka kwa wazazi wake?— Bila shaka alijifunza hilo kutoka kwao. Baba yake, Yese, alikuwa mzee mwaminifu wa ukoo wa Yesu Kristo, “Mkuu wa Amani” aliyeahidiwa wa Mungu. (Isaya 9:6; 11:1-3, 10) Baba ya Yese, yaani, babu ya Daudi, alikuwa Obedi. Kitabu kimoja cha Biblia kina jina la mama ya Obedi. Je, unajua jina lake?— Ni Ruthu, mwanamke mshikamanifu aliyekuwa mke wa Boazi.—Ruthu 4:21, 22.

Bila shaka, Ruthu na Boazi walikufa muda mrefu kabla ya Daudi kuzaliwa. Huenda unajua jina la mama ya Boazi, yaani, nyanya ya nyanya ya Daudi. Aliishi Yeriko na alisaidia kuwaokoa wapelelezi fulani Waisraeli. Kuta za Yeriko zilipoanguka, alilindwa pamoja na familia yake kwa kuning’iniza kamba nyekundu katika dirisha lake. Jina lake ni nani?— Ni Rahabu ambaye alikuja kuwa mwabudu wa Yehova, na ni mfano wa ujasiri unaopaswa kuigwa na Wakristo.—Yoshua 2:1-21; 6:22-25; Waebrania 11:30, 31.

Tunaweza kuwa na hakika kwamba baba na mama ya Daudi walimfundisha kuhusu watumishi hao waaminifu wa Yehova kwa kuwa wazazi waliamriwa wawafundishe watoto wao mambo kama hayo. (Kumbukumbu la Torati 6:4-9) Wakati ulifika ambapo Samweli nabii wa Mungu aliambiwa amchague Daudi, mwana mchanga zaidi wa Yese, kuwa mfalme wa wakati ujao wa Israeli.—1 Samweli 16:4-13.

Siku moja, Yese alimtuma Daudi awapelekee chakula kaka zake watatu waliokuwa wakipigana na adui za Mungu, Wafilisti. Daudi anapofika, anakimbia kwenda kwenye uwanja wa mapigano na anasikia jitu linaloitwa Goliathi likivitukana “vikosi vya Mungu aliye hai.” Watu wote wanaogopa kupigana na Goliathi. Mfalme Sauli anasikia kwamba Daudi yuko tayari kupigana na jitu hilo, hivyo anamwita. Lakini Sauli anapomwona Daudi, anamwambia: “Wewe ni mvulana tu.”

Daudi anamweleza Sauli kwamba alimwua simba na dubu waliojaribu kuchukua kondoo wa familia yake. Goliathi “atakuwa kama mmoja wa hao,” Daudi anasema. “Nenda, na Yehova awe pamoja nawe,” Sauli anajibu. Daudi anajichagulia mawe matano yaliyo laini kabisa, anayatia katika mfuko wake wa mchungaji, anachukua kombeo lake, na kwenda kupigana na jitu hilo. Goliathi anapomwona mvulana huyo akija, anasema hivi kwa sauti: “Wewe nikaribie tu, nyama yako nitawapa ndege.” Daudi anajibu: “Naja kwako nikiwa na jina la Yehova,” na kisha akasema hivi kwa sauti: “Hakika nitakupiga.”

Baada ya hapo, Daudi anakimbia kumwelekea Goliathi, anachukua jiwe kutoka kwenye mfuko wake, analiweka kwenye kombeo lake, na kulitupa moja kwa moja ndani ya kichwa cha Goliathi. Wafilisti wanapoona kwamba jitu limekufa, wanaogopa na kukimbia. Waisraeli wanawafuatilia na kushinda vita hivyo. Tafadhali soma pamoja na familia yako simulizi hilo lote katika 1 Samweli 17:12-54.

Ukiwa kijana, huenda nyakati fulani ukaogopa kufuata amri za Mungu. Yeremia alikuwa kijana na aliogopa mwanzoni, lakini Mungu alimwambia: “Usiogope . . . kwa maana ‘mimi niko pamoja nawe.’” Yeremia alipata ujasiri na kuhubiri kama Mungu alivyomwagiza afanye. Kama Daudi na Yeremia, ukimtegemea Yehova, wewe pia unaweza kujifunza kuwa jasiri.—Yeremia 1:6-8.

^ fu. 3 Kama unasoma sehemu hii pamoja na watoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na uwaruhusu watoe maoni yao.