Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unawaogopa Wafu?

Je, Unawaogopa Wafu?

Je, Unawaogopa Wafu?

HUENDA watu wengi wakajibu swali hilo kwa kusema “La, kwa nini niogope?” Wanaamini kwamba wafu kwa kweli wamekufa. Hata hivyo, mamilioni wanaamini kwamba wafu wanaendelea kuishi wakiwa roho.

Nchini Benin, Afrika Magharibi, watu wengi wanaamini kwamba wafu wanaweza kurudi kuwaua washiriki wengine wa familia zao. Watu wanauza mali au kukopa pesa ili kulipia dhabihu za wanyama na sherehe za kuwatuliza watu wa ukoo waliokufa. Wengine wana mazoea ya kuwasiliana na pepo yanayotia ndani wazo la kwamba roho ya wanadamu inaendelea kuishi na inaweza kuwasiliana na watu walio hai. Wengine wamepitia mambo ya kutisha ambayo wanasema yanasababishwa na roho za wafu.

Mtu mmoja aliyepitia jambo kama hilo ni Agboola anayeishi karibu na mpaka wa Benin na Nigeria. Mwanamume huyo anasema: “Kuwasiliana na pepo ni jambo la kawaida katika eneo letu. Ni kawaida kuosha maiti kidesturi ili kuzitayarisha kwa ajili ya makao ya roho. Mara nyingi nilikusanya sabuni zilizobaki na kuzichanganya na majani fulani. Kisha niliipaka bunduki yangu ya kuwinda mchanganyiko huo na kusema kwa sauti nilitaka kupiga mnyama gani. Mazoea kama hayo ni ya kawaida na yalionekana kuwa na matokeo. Hata hivyo, mambo fulani kuhusu kuwasiliana na pepo yalinitisha sana.

“Wana wangu wawili walipokufa kwa njia zisizoeleweka nilishuku kwamba mtu fulani alikuwa akiniroga. Ili kutambua kama ni kweli nilimwendea mzee fulani aliyejulikana kwa uwezo wake wa kuwasiliana na pepo. Aliniambia kwamba ni kweli nimerogwa. Kwa kuhuzunisha hata zaidi, alieleza kwamba wana wangu sasa walikuwa wakingoja katika ulimwengu wa roho ili wawe watumishi wa mwuaji wao atakapokufa. Mzee huyo aliniambia kwamba mwana wangu wa tatu angekufa. Siku chache baadaye, mwana huyo alikufa.”

Kisha Agboola akakutana na John ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova kutoka Nigeria. Ufafanuzi wa John kuhusu hali ya wafu ulitegemea Biblia. Ufafanuzi huo ulibadili maisha ya Agboola. Unaweza kubadili maisha yako pia.

Je, Wafu Wako Hai?

Ni nani anayeweza kujibu swali hilo kwa njia bora? Si mwanadamu yeyote, hata awe na uwezo kadiri gani. Badala yake, Yehova, Muumba wa kila kitu kilicho hai “mbinguni na duniani, vitu vinavyoonekana na vitu visivyoonekana,” anaweza kujibu. (Wakolosai 1:16) Aliwaumba malaika waishi katika makao ya roho na mwanadamu na wanyama ili waishi duniani. (Zaburi 104:4, 23, 24) Uhai wote unamtegemea Yehova. (Ufunuo 4:11) Basi, hebu chunguza kile ambacho Neno la Mungu mwenyewe, Biblia, linasema kuhusu kifo.

Yehova ndiye aliyekuwa wa kwanza kuzungumza kuhusu kifo. Alionya kwamba Adamu na Hawa wangekufa ikiwa hawangemtii. (Mwanzo 2:17) Hilo lilimaanisha nini? Yehova alieleza: “Wewe ni mavumbi nawe utarudi mavumbini.” (Mwanzo 3:19) Mtu anapokufa, mwili unaoza; unarudi mavumbini. Uhai unakoma.

Adamu na Hawa walikosa kutii kimakusudi, hivyo wakahukumiwa kifo. Hata hivyo, si wao waliokufa kwanza. Abeli mwana wao ndiye aliyekufa kwanza. Kaini, kaka yake, alimwua. (Mwanzo 4:8) Kaini hakuogopa kwamba ndugu yake aliyekufa angelipiza kisasi. Badala yake, Kaini aliogopa vile ambavyo angetendewa na watu waliokuwa hai.—Mwanzo 4:10-16.

Karne nyingi baadaye, Mfalme Herode alikasirika alipoambiwa na wanajimu kwamba “mfalme wa Wayahudi” alikuwa amezaliwa katika eneo alilotawala. Akiwa ameazimia kumwangamiza mfalme huyo, Herode alipanga njama ili wavulana wote huko Bethlehemu kuanzia umri wa miaka miwili kwenda chini wauawe. Lakini malaika alimwonya Yosefu na kumwambia awachukue Yesu na Maria na ‘wakimbie kuingia Misri.’—Mathayo 2:1-16.

Herode alipokufa, malaika alimwambia Yosefu arudi Israeli, “kwa maana wale waliokuwa wakiitafuta nafsi ya mtoto huyo [walikuwa] wamekufa.” (Mathayo 2:19, 20) Malaika huyo ambaye alikuwa kiumbe wa roho, alijua kwamba Herode hangemdhuru Yesu tena. Yosefu hakumwogopa Mfalme Herode aliyekuwa amekufa. Hata hivyo, Yosefu aliogopa kile ambacho mwana wa mkatili wa Herode, Arkelao, angefanya. Kwa hiyo, Yosefu aliishi na familia yake huko Galilaya, nje ya eneo ambalo Arkelao alitawala.—Mathayo 2:22.

Masimulizi hayo yanatusaidia kuona kwamba wafu hawana nguvu zozote. Hivyo basi, tunaweza kueleza jinsi gani kisa cha Agboola na wengine?

“Roho Waovu”

Akiwa mtu mzima, Yesu alikutana na roho waovu. Walimtambua Yesu na kumwita “Mwana wa Mungu.” Yesu pia aliwajua wao ni nani. Hawakuwa roho za wafu. Badala yake Yesu aliwaita “roho waovu,” au pepo wachafu.—Mathayo 8:29-31; 10:8; Marko 5:8.

Biblia inataja viumbe wa roho walio washikamanifu kwa Mungu na wale waliomwasi. Kitabu cha Mwanzo kinasema kwamba Adamu na Hawa walipomwasi, Yehova aliwafukuza kutoka kwa bustani ya Edeni na akaweka makerubi au malaika upande wa mashariki wa bustani hiyo ili kumzuia mtu yeyote asiingie. (Mwanzo 3:24) Inaonekana kwamba hiyo ndiyo mara ya kwanza kwa wanadamu kuona viumbe hao wa roho.

Muda fulani baadaye, malaika kadhaa walikuja duniani na kujivika miili ya kibinadamu. Yehova hakuwa amewatuma wafanye kazi yoyote duniani. Badala yake, ‘waliyaacha makao yao wenyewe yanayofaa’ katika makao ya roho. (Yuda 6) Walikuwa na sababu za ubinafsi. Walijichukulia wake waliozaa majitu yaliyoitwa Wanefili. Wanefili hao na baba zao waasi walijaza dunia jeuri na ubaya mwingine mwingi. (Mwanzo 6:1-5) Yehova alichukua hatua kwa kuleta Gharika ya siku za Noa iliyokuwa ulimwenguni pote. Maji ya mafuriko hayo yaliwaangamiza wanaume na wanawake waovu na pia majitu hayo. Ni nini kilichowapata malaika hao?

Gharika iliwafanya warudi kwenye makao ya roho. Hata hivyo, Yehova aliwazuia kurudi kwa “mahali pao pa kwanza.” (Yuda 6) Biblia inasema: “Mungu hakujizuia kuwaadhibu wale malaika waliofanya dhambi, bali, kwa kuwatupa ndani ya Tartaro, aliwatia ndani ya mashimo yenye giza zito ili wawekwe akiba kwa ajili ya hukumu.”—2 Petro 2:4.

Tartaro si mahali hususa; ni hali ya kushushwa iliyo kama kufungwa ambayo inadhibiti utendaji wa waasi hao. Roho waovu hawawezi tena kujivika miili ya kibinadamu, lakini bado wana nguvu na uvutano mwingi juu ya akili na maisha ya watu. Wanaweza kufanya wanadamu na wanyama wapagawe. (Mathayo 12:43-45; Luka 8:27-33) Pia wanawadanganya wanadamu kwa kujifanya roho za wafu. Kwa nini? Ili kuwazuia watu wasimwabudu Yehova kwa njia inayompendeza na kuwatatanisha kuhusu hali halisi ya wafu.

Jinsi ya Kushinda Woga

Agboola aliona kwamba ufafanuzi wa Biblia kuhusu kifo na utambulisho wa viumbe wa roho unapatana na akili. Alielewa kwamba alihitaji kujifunza mengi zaidi. Alianza kujifunza Biblia na vichapo vinavyotegemea Biblia pamoja na John. Agboola alifarijiwa kwa kujifunza kwamba wana wake walikuwa wamelala kaburini, na si kwamba walikuwa katika makao ya roho wakingoja kuwa watumwa wa mwuaji wao.—Yohana 11:11-13.

Agboola pia alitambua kwamba alihitaji kuacha kabisa mazoea ya kuwasiliana na pepo. Aliteketeza vitu vyote alivyotumia katika uchawi. (Matendo 19:19) Watu fulani katika eneo lake walimwonya kwamba roho waovu wangekasirika. Lakini Agboola hakuogopa. Alifuata shauri linalopatikana katika Andiko la Waefeso 6:11, 12: “Vaeni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu . . . kwa sababu tuna kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho waovu.” Mavazi hayo ya silaha ya kiroho yanatia ndani kweli, uadilifu, habari njema ya amani, imani, na upanga wa roho, yaani, Neno la Mungu. Silaha hizo zinatoka kwa Mungu na ni zenye nguvu!

Baadhi ya marafiki na watu wa ukoo wa Agboola walimtenga kwa sababu alijiepusha na desturi zilizohusisha kuwasiliana na pepo. Hata hivyo, katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova la kwao, alipata marafiki wapya wanaoamini kile ambacho Biblia inafundisha.

Sasa Agboola anajua kwamba hivi karibuni Yehova atasafisha dunia, aondoe uovu, na kuzuia utendaji wote wa roho waovu. Hatimaye, Mungu atawaangamiza. (Ufunuo 20:1, 2, 10) Mungu atawafufua “wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho” hapa duniani. (Yohana 5:28, 29) Watatia ndani Abeli, watoto wasio na hatia ambao Mfalme Herode aliua, na mamilioni ya watu wengine. Agboola ana imani kwamba wana wake watatu watafufuliwa pia. Huenda wapendwa wako waliokufa watafufuliwa pia. Watu wote waliofufuliwa watathibitisha kwamba tangu walipokufa hadi walipofufuliwa hawakuwa na hisia zozote na hawakutambua kwamba kuna sherehe zilizofanywa kwa niaba yao.

Huna sababu ya kuwaogopa wafu. Badala ya hivyo, unaweza kutazamia kuwaona tena wapendwa wako waliokufa. Lakini sasa, kwa nini usijifunze Biblia ili uimarishe imani yako? Shirikiana na wale wanaoamini yale ambayo Biblia inafundisha. Ikiwa unawasiliana na pepo, acha mara moja. Jilinde dhidi ya roho waovu kwa kuvaa “mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu.” (Waefeso 6:11) Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia. Wao wanajifunza na watu Biblia wakitumia kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? *

Agboola hawaogopi wafu tena, na amejifunza jinsi ya kupinga roho waovu. Anasema: “Sijui ni nani aliyesababisha kifo cha wana wangu watatu. Lakini tangu nianze kumtumikia Yehova, nimepata watoto wengine saba. Hakuna yeyote kutoka makao ya roho ambaye amewadhuru.”

[Maelezo ya chini]

^ fu. 25 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 13]

Agboola hawaogopi wafu tena, na amejifunza jinsi ya kupinga roho waovu

[Picha katika ukurasa wa 12]

Kaini hakuogopa kwamba ndugu yake aliyekufa angelipiza kisasi