Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Pontio Pilato alikuwa na sababu ya kumwogopa Kaisari?

Ili wamshinikize Gavana Mroma Pontio Pilato amwue Yesu, viongozi Wayahudi walisema: “Ukimfungua mtu huyu, wewe si rafiki ya Kaisari.” (Yohana 19:12) “Kaisari” anayetajwa hapo ni Maliki Mroma Tiberio. Je, Pilato alikuwa na sababu ya kumwogopa Kaisari huyo?

Kaisari Tiberio alikuwa mtu wa aina gani? Miaka mingi kabla ya kesi ya Yesu, tayari Tiberio alikuwa “mtu aliyeonekana kuwa anapendezwa na kujitosheleza tu na alitumia njia zilizopotoka kufanya hivyo,” kinasema kitabu kimoja (The New Encyclopædia Britannica). Woga ulimfanya awatese na kuwaua hata watu walioshukiwa kuwa wahaini. “Ikiwa wanahistoria walioishi kipindi chake wanaweza kuaminiwa,” kinaripoti kitabu hicho, “alipenda hasa burudani chafu na zenye ukatili. Hata maelezo yanayoeleza mambo kwa kumpendelea yanaonyesha kwamba aliua kwa ukatili mtu yeyote aliyetaka wakati wowote.”

Hivyo basi huenda ikawa kwamba mambo yaliyojulikana kumhusu Tiberio yalimfanya Pilato akubaliane na viongozi Wayahudi na kuagiza Yesu auawe.—Yohana 19:13-16.

Kwa nini Yesu aliosha miguu ya mitume wake?

Katika Israeli la kale, watu wengi wa kawaida walifanya shughuli zao za kila siku bila viatu. Na wale waliovaa viatu walivaa sapatu, viatu ambavyo vilikuwa na soli na kamba za kufungia kwenye kifundo cha mguu. Kwa kuwa barabara na mashamba yalikuwa yenye vumbi au matope, miguu ya watu ilichafuka.

Hivyo, ilikuwa desturi kwa mtu kuvua sapatu zake kabla ya kuingia katika nyumba. Mwenye nyumba alimwonyesha mgeni ukarimu kwa kumwosha miguu. Kazi hiyo ingefanywa na mwenye nyumba mwenyewe au mtumishi wake. Biblia inasema mara kadhaa kuhusu desturi hiyo. Kwa mfano, Abrahamu aliwaambia hivi wageni katika hema lake: “Tafadhali, acha maji kidogo yachukuliwe, nanyi mwoshwe miguu yenu. Kisha mketi chini ya mti. Nanyi acheni nichukue kipande cha mkate, niburudishe mioyo yenu.”—Mwanzo 18:4, 5; 24:32; 1 Samweli 25:41; Luka 7:37, 38, 44.

Habari hiyo inatusaidia kuelewa jinsi Yesu alivyowaosha wanafunzi wake miguu katika Pasaka ya mwisho pamoja nao. Wakati huo, hakukuwa na mwenye nyumba au mtumishi wa kufanya kazi hiyo, na inaonekana kwamba hakuna mwanafunzi aliyejitolea kuifanya. Hivyo kwa kuchukua beseni la maji na kitambaa ili aoshe na kukausha miguu ya mitume wake, Yesu aliwafundisha wanaume hao upendo na unyenyekevu.—Yohana 13:5-17.