Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jukumu la Maria Katika Kusudi la Mungu

Jukumu la Maria Katika Kusudi la Mungu

Jukumu la Maria Katika Kusudi la Mungu

WAKATI wa huduma ya Yesu, mwanamke aliinua sauti yake katika umati na kusema: “Lenye furaha ni tumbo la uzazi lililokuchukua wewe na maziwa uliyonyonya!” Ikiwa Yesu alitaka mama yake aabudiwe, alikuwa amepata nafasi nzuri ya kupendekeza jambo hilo. Lakini alijibu: “Hapana, badala yake, Wenye furaha ni wale wanaolisikia neno la Mungu na kulishika!”—Luka 11:27, 28.

Yesu hakumpendelea mama yake; wala hakuwaambia wafuasi wake wafanye hivyo. Jambo hili linapatana jinsi gani na vile waamini wengi wanyoofu wanavyomwabudu Maria? Acheni tuchunguze baadhi ya mafundisho yaliyoenea sana kuhusu mama ya Yesu na kuyalinganisha na Maandiko Matakatifu.

“Umejaa Neema,” “Mbarikiwa Kati ya Wanawake”

Malaika Gabrieli alimweleza Maria jukumu lake katika kusudi la Mungu. Katika pindi hiyo, alimsalimu Maria akisema hivi: “Siku njema, uliyependelewa sana, Yehova yuko pamoja nawe.” (Luka 1:28) Tafsiri nyingine ya salamu hizo ni: “Salamu, umejaa neema, Bwana yu nawe.” Muda mfupi baada ya hapo, Elisabeti alimsalimia Maria akisema: “Wewe ni mbarikiwa kati ya wanawake, na uzao wa tumbo lako la uzazi umebarikiwa!” (Luka 1:42) Je, maneno hayo hayaonyeshi kwamba Maria anapaswa kuabudiwa?

Hapana. Ingawa maneno haya yanapatikana katika sala ambayo Wakatoliki wanamtolea Maria, Biblia haionyeshi kwamba watu wanapaswa kusali kwake. Gabrieli na Elisabeti walitambua kwamba Maria alikuwa na pendeleo kubwa la kumzaa Masihi, lakini wazo la kusali kwake halipatikani katika Maandiko. Kinyume na hilo, wanafunzi wa Yesu walipomwuliza awafundishe kusali, alionyesha kwamba sala zinapaswa kuelekezwa kwa Baba yake. Kwa kweli, sala ya Yesu inayojulikana sana inaanza kwa maneno haya: “Baba yetu uliye mbinguni.”—Mathayo 6:9.

Ni Mmoja wa Watawala

Fundisho lingine linalojulikana sana kumhusu Maria ni kwamba sasa yeye ni “Malkia wa mbinguni.” Biblia haimpi cheo kama hicho. Hata hivyo, inaonyesha kwamba ana sehemu ya pekee katika mpango wa kimbingu wa Mungu. Ni sehemu gani hiyo?

Yesu alionyesha kwamba baadhi ya wanafunzi wake waaminifu wangetawala pamoja naye katika Ufalme wake. (Luka 22:28-30) Yesu atawapa hao waliochaguliwa mamlaka ya kuwa “makuhani kwa Mungu wetu, nao watatawala wakiwa wafalme juu ya dunia.” (Ufunuo 5:10) Biblia inatusaidia kuona kwamba Maria ni kati ya wale ambao wamepewa pendeleo hilo kuu. Kwa nini tunasema hivyo?

Utakumbuka kwamba baada ya kifo cha Yesu, Maria alikuwa ‘akidumu katika sala’ pamoja na wanafunzi wa Yesu na ndugu zake. Watu 120 hivi walikutana kwa kusudi hilo kutia ndani “wanawake fulani.” (Matendo 1:12-15) “Sherehe ya Pentekoste ilipokuwa ikiendelea,” inasema Biblia, “walikuwa wote pamoja mahali pale pale” wakati roho takatifu ya Mungu ilipomiminwa juu yao na kuwapa uwezo wa kuzungumza katika lugha za kigeni.—Matendo 2:1-4.

Kwa vile Maria alikuwa kati ya wale waliobarikiwa kwa njia hiyo, hilo linaonyesha kwamba yeye na wanawake waliopokea roho takatifu walichaguliwa kuwa sehemu ya Ufalme wa Yesu wa mbinguni. Kwa hiyo, tuna kila sababu kuamini kwamba sasa Maria ameketi pamoja na Yesu katika utukufu wa kimbingu. (Waroma 8:14-17) Fikiria baadhi ya mapendeleo ambayo yeye pamoja na wengine watakaotawala pamoja na Yesu watakuwa nayo katika kutimizwa kwa makusudi ya Mungu.

Kuandaa Baraka za Ajabu

Kitabu cha Biblia cha Ufunuo kinasema kwamba watu 144,000 watafufuliwa kwenye utukufu wa kimbingu ili watumikie pamoja na Yesu wakiwa makuhani, mahakimu, na wafalme. (Ufunuo 14:1, 4; 20:4, 6) Wakiwa makuhani, watashiriki katika kutoa faida za dhabihu ya Yesu kwa wanadamu wote watiifu na kuwainua kufikia ukamilifu wa kiroho, kiadili, na kimwili. (Ufunuo 21:1-4) Litakuwa pendeleo kama nini kwa waabudu wote washikamanifu wa Yehova kuona wakati huo mzuri ajabu! *

Maria alikuwa na jukumu na bado ana jukumu katika kutimizwa kwa makusudi ya Yehova. Anastahili kuigwa kwa sababu ya unyenyekevu, imani, utii, na bidii yake akiwa mama, bila kusahau uvumilivu wake alipokabili majaribu. Kwa sababu ya kutimiza jukumu la kumzaa Masihi na kuandaa baraka za milele kwa wanadamu, anastahili kuheshimiwa kabisa.

Hata hivyo, jambo muhimu zaidi tunalojifunza kutoka kwa Maria ni kwamba yeye pamoja na watumishi wengine wote waaminifu wa Mungu wanamwabudu Yehova peke yake na wala si mungu mwingine. Maria pamoja na wengine wanaotawala pamoja na Kristo mbinguni, anasema kwa sauti kubwa: “Kwake Yule [Yehova Mungu] anayeketi juu ya kile kiti cha ufalme na kwa Mwana-Kondoo [Yesu Kristo] kuwe na baraka na heshima na utukufu na nguvu milele na milele.”—Ufunuo 5:13; 19:10.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 13 Kwa habari zaidi kuhusu baraka hizo, ona sura ya 8 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 10]

Maria anastahili kuigwa kwa sababu ya unyenyekevu, imani, na utii wake