Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Thamini Mvua

Thamini Mvua

Thamini Mvua

MAISHA yangekuwa namna gani bila mvua? Ni kweli kwamba nyakati nyingine mvua nyingi inaweza kusababisha mafuriko yenye madhara. Pia, huenda watu wanaoishi katika maeneo baridi, yenye mvua au yenye majira kama hayo hawafurahii mvua pindi fulani. (Ezra 10:9) Lakini vipi kuhusu mamilioni wanaolazimika kuvumilia majira marefu ya joto kali? Mwishowe, mvua inaponyesha, inaburudisha kama nini!

Hali ilikuwa hivyo katika maeneo yanayotajwa katika Biblia, kama vile Asia Ndogo, eneo ambalo mtume Paulo alihubiri akiwa mmishonari. Akiwa huko, Paulo aliwaambia hivi Walikaonia wa wakati huo: “[Mungu] hakujiacha mwenyewe bila ushahidi kwa kuwa alitenda mema, akiwapa ninyi mvua kutoka mbinguni na majira yenye kuzaa matunda, akijaza mioyo yenu kikamili kwa chakula na uchangamfu.” (Matendo 14:17) Ona kwamba Paulo anataja mvua kwanza, kwa sababu pasipo mvua mimea haiwezi kukua na hivyo hakutakuwa na “majira yenye kuzaa matunda.”

Biblia inasema mengi kuhusu mvua. Maneno ya Kiebrania na Kigiriki yanayotafsiriwa mvua yanapatikana katika Biblia zaidi ya mara 100. Je, ungependa kujifunza zaidi kuhusu zawadi yenye kustaajabisha ya mvua? Wakati huohuo, je, ungependa kuimarisha imani yako katika usahihi wa kisayansi wa Biblia?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Mvua?

Yesu Kristo alikazia fikira maandalizi muhimu ambayo yanawezesha kuwe na mvua. “Baba yenu,” Yesu alisema, “hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mathayo 5:45) Je, umeona kwamba Yesu alitaja jua kabla ya kutaja mvua? Hilo linafaa kwa sababu jua linaandaa nishati ili mimea ikue na pia linachochea mzunguko wa maji duniani. Ndiyo, joto kutoka kwa jua linafanya maji mengi sana baharini yavukizwe na kuwa mvuke wa maji baridi kila mwaka. Kwa sababu Yehova Mungu aliumba jua, kwa kufaa anaitwa yule anayeteka maji na kuyafanya yawe mvua.

Biblia inaufafanua mzunguko wa maji hivi: “Mungu . . . huyateka matone ya maji; yanajichuja kama mvua yawe ukungu wake, hivi kwamba mawingu yanadondoka, yanadondoka kwa wingi juu ya wanadamu.” (Ayubu 36:26-28) Kwa maelfu ya miaka tangu maneno hayo yaliyo sahihi kisayansi yalipoandikwa, mwanadamu amekuwa na muda mrefu wa kujaribu kuelewa mzunguko wa maji. “Kufikia sasa,” kinasema kitabu fulani cha mwaka wa 2003 (Water Science and Engineering), “haijulikani kwa uhakika jinsi matone ya mvua yanavyofanyizwa.”

Wanasayansi wanajua kwamba matone ya mvua yanafanyizwa kwa chembechembe ambazo zinakuja kuwa matone madogo sana katika mawingu. Kila tone dogo lazima liongezeke mara milioni moja au zaidi ili lifanyize tone moja la mvua. Hiyo ni mbinu tata inayoweza kuchukua saa kadhaa. Kitabu kimoja cha kisayansi (Hydrology in Practice) kinasema: “Kuna nadharia kadhaa juu ya jinsi matone madogo ya mawingu yanavyokuwa matone ya mvua, na wachunguzi wanatumia muda mwingi kuchunguza njia hususa ambazo zinahusika.”

Muumba wa mifumo ya kutokeza mvua alimwuliza mtumishi wake Ayubu maswali haya yenye kunyenyekeza: “Je, mvua ina baba, au ni nani aliyezaa matone ya umande? Ni nani aliyetia hekima katika tabaka za mawingu? . . . Ni nani anayeweza kuhesabu kwa ukamili mawingu kwa hekima, au mitungi ya maji ya mbingu—ni nani anayeweza kuipindua?” (Ayubu 38:28, 36, 37) Miaka 3,500 hivi baadaye, wanasayansi bado wanatafuta majibu ya maswali hayo magumu.

Mzunguko wa Maji Unafuata Njia Gani?

Wanafalsafa Wagiriki walifundisha kwamba chanzo cha maji ya mto si mvua bali ni maji ya bahari ambayo kwa njia fulani yanapitia chini ya ardhi na kupanda juu milimani, kisha yanakuwa chemchemi ya maji baridi. Kitabu kimoja kinachotoa maelezo kuhusu Biblia kinadai kwamba Sulemani alikubaliana na wazo hilo. Fikiria maneno haya ya Sulemani yaliyoongozwa na roho ya Mungu: “Mito yote ya wakati wa majira ya baridi kali inaenda baharini, hata hivyo bahari haijai. Mahali inapoenda mito hiyo ya majira ya baridi kali, hapo ndipo inarudi ili iende tena.” (Mhubiri 1:7) Je, kweli Sulemani alimaanisha kwamba maji ya bahari yalielekezwa juu ya milima ili yawe chanzo cha maji ya mito? Ili kujibu swali hilo, acheni tuone jinsi watu walioishi nyakati za Sulemani walivyoamini kuhusu mzunguko wa maji. Je, waliamini mawazo hayo ya uwongo?

Miaka isiyozidi 100 baada ya siku za Sulemani, nabii wa Mungu, Eliya alionyesha maoni yake kuhusu upande ambao mvua inatoka. Katika siku zake, nchi ilikumbwa na ukame mbaya sana kwa zaidi ya miaka mitatu. (Yakobo 5:17) Yehova Mungu alikuwa ameleta msiba huo juu ya watu wake kwa sababu walimkataa na kuanza kuabudu mungu wa mvua wa Kanaani aliyeitwa Baali. Lakini Eliya aliwasaidia Waisraeli kutubu, na hivyo sasa alikuwa tayari kusali ili wapate mvua. Alipokuwa akisali, Eliya alimwambia mtumishi wake atazame “upande wa bahari.” Alipoambiwa kwamba kuna “wingu dogo kama kiganja cha mkono wa mwanadamu linalopanda kutoka baharini,” Eliya alijua sala yake imejibiwa. Punde si punde, “mbingu zikatiwa giza kwa mawingu na upepo na mvua kubwa sana ikaanza kunyesha.” (1 Wafalme 18:43-45) Kwa hiyo, Eliya alionyesha kwamba alijua kuhusu mzunguko wa maji. Alijua mawingu yanafanyizwa juu ya bahari na kupeperushwa upande wa mashariki wa Nchi ya Ahadi. Hadi leo, nchi hiyo inapata mvua kwa njia nchi hiyo.

Miaka 100 hivi baada ya Eliya kusali kwa ajili ya mvua, mkulima anayeitwa Amosi alikazia jambo muhimu kuhusu chanzo cha mzunguko wa maji. Amosi alitumiwa na Mungu kutoa unabii dhidi ya Waisraeli kwa sababu ya kuwanyanyasa maskini na kuabudu miungu ya uwongo. Ili wasiangamizwe na Mungu, Amosi aliwahimiza ‘wamtafute Yehova ili waendelee kuishi.’ Kisha Amosi akaeleza kwamba ni Yehova peke yake anayepaswa kuabudiwa kwa sababu yeye ndiye Muumba, “Yeye ambaye anaita maji ya bahari, ili ayamwage kwenye uso wa dunia.” (Amosi 5:6, 8) Baadaye Amosi alirudia jambo hilo kuhusu mzunguko wa maji na upande ambao unaelekea. (Amosi 9:6) Hivyo, Amosi alionyesha kwamba chanzo kikuu cha mvua inayonyesha duniani ni bahari.

Jambo hilo lilithibitishwa kisayansi na Edmond Halley mnamo 1687. Hata hivyo, ilichukua muda kwa wengine kukubali uthibitisho wa Halley. Kitabu kimoja cha marejeo (Encyclopædia Britannica Online) kinasema hivi: “Wazo la kwamba kuna mzunguko wa maji katika Dunia, ambao unasafirisha maji ya bahari juu milimani na kuyamwaga, liliendelea hadi mwanzoni mwa karne ya 18.” Leo, kila mtu anajua upande ambao mzunguko wa maji unaelekea. Kitabu hichohicho kinaeleza: “Maji ya bahari yanavukizwa, yanagandishwa angani, yanamwagika Duniani kama mvua, na mwishowe yanatiririka hadi kwenye mito na kurudi baharini.” Hivyo basi ni wazi kwamba maneno ya Sulemani kuhusu mzunguko wa mvua yaliyorekodiwa katika Mhubiri 1:7, yanarejelea mfumo uleule unaohusu mawingu na mvua.

Hilo Linapaswa Kukuchochea Ufanye Nini?

Mzunguko wa maji uliofafanuliwa kwa usahihi sana na waandikaji kadhaa wa Biblia, ni mojawapo ya uthibitisho wa kwamba Biblia iliongozwa na roho ya Muumba wa wanadamu, Yehova Mungu. (2 Timotheo 3:16) Ni kweli kwamba mwanadamu ametumia dunia vibaya, na hivyo hali ya hewa imebadilika na kutokeza mafuriko makubwa katika sehemu fulani na ukame katika maeneo mengine. Lakini Yehova Mungu, Muumba wa mzunguko wa maji, aliahidi zamani kwamba mwishowe ataingilia kati na “kuwaharibu wale wanaoiharibu dunia.”—Ufunuo 11:18.

Lakini sasa, unaweza jinsi gani kuonyesha uthamini wako kwa zawadi za Mungu, kama vile mvua? Unaweza kufanya hivyo kwa kujifunza Neno lake, Biblia, na kufuata mambo unayojifunza maishani. Kisha utakuwa na tumaini la kuokoka na kuingia ndani ya ulimwengu mpya wa Mungu ambako utaweza kufurahia zawadi zote za Mungu milele. Kwa kweli, “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu” inatoka kwa Chanzo cha mvua, Yehova Mungu.—Yakobo 1:17.

[Mchoro/Picha katika ukurasa wa 16, 17]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

KUGANDA

MVUA

MAJI KUTOKA KWA MIMEA

UVUKIZAJI

MAJI YA MVUA

MAJI ARDHINI

[Picha katika ukurasa wa 16]

Eliya alipokuwa akisali, mtumishi wake alitazama “upande wa bahari”