Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuna Wakati wa Kila Kitu

Kuna Wakati wa Kila Kitu

Kuna Wakati wa Kila Kitu

“Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu, hata kuna wakati wa kila jambo chini ya mbingu,” inasema Biblia. Mfalme Sulemani mwenye hekima wa kale, ambaye aliandika maneno hayo, aliendelea kusema kwamba kuna wakati wa kuzaliwa na wakati wa kufa, wakati wa kujenga na wakati wa kubomoa, wakati wa kupenda na wakati wa kuchukia. Mwishowe akasema: “Mtendaji ana faida gani katika jambo analofanyia kazi ngumu?”—Mhubiri 3:1-9.

WATU fulani wanaposoma maneno hayo, wanakata kauli kwamba Biblia inafundisha kwamba kuna wakati ulioamuliwa mapema wa kila kitu; yaani, wanafikiri kwamba Biblia inaunga mkono fundisho la majaliwa. Je, hilo ni kweli? Je, kweli Biblia inaunga mkono wazo la kwamba kila kitu kimepangiwa mapema na Mungu? Kwa kuwa “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu,” basi kile tunachosoma katika sehemu moja ya Biblia lazima kipatane na sehemu nyingine ya Biblia. Kwa hiyo, acheni tuone Neno la Mungu, Biblia, linasema nini kuhusu jambo hilo.—2 Timotheo 3:16.

Wakati na Tukio Lisilotazamiwa

Sulemani aliendelea kuandika hivi katika kitabu cha Mhubiri: “Nilirudi, nikaona chini ya jua kwamba si wenye mbio wanaoshinda katika mbio, wala wenye nguvu wanaoshinda katika pigano, wala pia wenye hekima wanaopata chakula, wala pia wenye uelewaji wanaokuwa na utajiri, wala wenye ujuzi wanaopata kibali.” Kwa nini? Alieleza hivi: “Kwa sababu wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.”—Mhubiri 9:11.

Badala ya kudokeza kwamba kila kitu maishani kimepangiwa mapema, Sulemani alikuwa akionyesha kwamba wanadamu hawawezi kutabiri matokeo ya jambo lolote kwa usahihi “kwa sababu wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” Mara nyingi, mambo yanampata mtu kwa sababu yuko mahali panapofaa wakati unaofaa, au tuseme, yuko mahali pasipofaa wakati usiofaa.

Kwa mfano, fikiria maneno haya: “Si wenye mbio wanaoshinda katika mbio.” Huenda ukakumbuka au ulisoma kuhusu kisa kisicho cha kawaida kilichotukia wakati wa mbio maarufu za mita 3000 za wanawake katika michezo ya Olimpiki iliyofanywa huko Los Angeles, California, Marekani mwaka wa 1984. Wakimbiaji wawili, mmoja kutoka Uingereza na mwingine kutoka Marekani, walikuwa wakitarajia kushinda medali ya dhahabu. Hata hivyo, mbio hizo zilipokuwa zikiendelea waligongana. Mmoja alianguka na kutoka katika mbio; yule mwingine alivunjika moyo sana na akamaliza katika nafasi ya saba.

Je, mambo hayo yalitukia kwa sababu ya majaliwa? Huenda watu fulani wakafikiri hivyo. Lakini ni wazi kwamba kugongana, jambo ambalo hakuna mtu angeweza kutabiri, ndiko kulisababisha wote wawili washindwe. Basi, je, ilipangwa mapema kwamba wagongane? Huenda watu fulani pia wakafikiri hivyo. Hata hivyo, watangazaji walisema aksidenti hiyo ilitukia kwa sababu wakimbiaji hao walikuwa na nguvu na uwezo sawa na kulikuwa na ushindani mkali kati yao. Kama Biblia inavyosema, “wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” Hata mtu awe amejitayarisha vizuri kadiri gani, sikuzote kuna mambo fulani yasiyotazamiwa yanayoweza kuathiri matokeo ya jambo, na hilo halisababishwi na majaliwa.

Basi Biblia inamaanisha nini inaposema: “Kuna wakati uliowekwa wa kila kitu”? Je, kuna jambo lolote tunaloweza kufanya ambalo litaamua jinsi maisha yetu yatakavyokuwa?

Wakati Unaofaa Zaidi kwa Kila Kitu

Mwandikaji wa Biblia hakuwa akizungumza kuhusu yale yatakayompata mtu yeyote, badala yake alikuwa akizungumza kuhusu kusudi la Mungu na matokeo yake juu ya wanadamu. Tunajua jambo hilo jinsi gani? Muktadha unaonyesha hivyo. Baada ya kutaja mambo mengi yanayoonekana kuwa na “wakati uliowekwa,” Sulemani aliandika hivi: “Nimeona shughuli ambayo Mungu amewapa wana wa binadamu wajishughulishe nayo. Amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake.”—Mhubiri 3:10, 11.

Mungu amewapa wanadamu shughuli nyingi, au mambo mengi ya kufanya, naye Sulemani aliorodhesha baadhi ya mambo hayo. Pia, Mungu ametupa uhuru wa kuchagua tunachotaka kufanya. Hata hivyo, kwa kila jambo kuna wakati unaofaa wa kulifanya ili kupata matokeo bora zaidi. Kwa mfano, fikiria maneno ya Sulemani “wakati wa kupanda na wakati wa kung’oa kilichopandwa,” yanayopatikana kwenye Mhubiri 3:2. Wakulima wanajua kwamba kuna wakati unaofaa zaidi wa kupanda kila mmea. Namna gani ikiwa mkulima angepuuza jambo hilo na kupanda mimea wakati au katika majira yasiyofaa? Je, atasema hakupata mazao mazuri kwa sababu ya majaliwa, hata kama amefanya kazi ngumu? La hasha! Hakupanda kwa wakati unaofaa. Mkulima angepata mazao mazuri ikiwa angefuata mpangilio wa mambo uliowekwa na Muumba.

Kwa hiyo, Mungu hajapanga mapema mambo yatakayompata kila mtu au jinsi mambo yote yatakavyotukia, bali ameweka kanuni za kuongoza utendaji wa wanadamu kupatana na kusudi lake. Ili wanadamu wafanikiwe katika shughuli zao, lazima watambue na kutenda kupatana na mapenzi ya Mungu na wakati wake uliowekwa. Kile ambacho kimeamuliwa mapema na ambacho wanadamu hawawezi kubadili si mambo yatakayompata mtu mmojammoja bali kile ambacho Mungu amekusudia kufanya. Kupitia kwa nabii Isaya Yehova alisema: ‘Neno langu linalotoka katika kinywa changu halitarudi kwangu bila matokeo, bali hakika litatenda yale ambayo yamenipendeza, na hakika litafanikiwa katika yale ambayo nimelituma.’—Isaya 55:11.

Basi, ni nini “neno” la Mungu, au kusudi lake kuhusu dunia na wakati ujao wa wanadamu ambalo “hakika litafanikiwa”?

Kuelewa Wakati wa Mungu

Baada ya kusema, “[Mungu] amefanya kila kitu kiwe chenye kupendeza kwa wakati wake,” Sulemani anatusaidia kuelewa maneno hayo kwa kusema, “Tena wakati usio na kipimo ameuweka ndani ya moyo wao, ili mwanadamu asiweze kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho.” Zaire Swahili Bible inasema hivi katika mstari huo: “Ameweka milele vilevile ndani ya mioyo yao, lakini hata mutu asiweze kutambua kazi Mungu aliyofanya tangu mwanzo hata mwisho.”—Mhubiri 3:11.

Mambo mengi yameandikwa kuhusu mstari huo. Lakini ukweli ni kwamba kila mmoja wetu amejiuliza wakati mmoja au mwingine kuhusu kusudi la maisha na wakati wetu ujao. Katika historia yote ya wanadamu, watu wameshindwa kukubali kwamba kusudi pekee la maisha ni kufanya kazi ngumu na kisha kufa. Kati ya viumbe wote, sisi wanadamu ni wa pekee kwa sababu tunafikiri si kuhusu wakati huu tu, bali pia kuhusu wakati wetu ujao. Hata tunatamani kuishi milele. Kwa nini? Kama andiko hilo linavyoonyesha, Mungu “ameweka milele . . . ndani ya mioyo” ya wanadamu.

Ili kutosheleza tamaa hiyo, watu wamejiuliza mara nyingi ikiwa kuna uhai baada ya kifo. Wengine wamekata kauli kwamba kitu fulani ndani yetu kinaendelea kuishi tunapokufa. Wengine wanaamini kwamba tutazaliwa upya tena na tena katika mwili mwingine. Wengine nao wanaamini kwamba kila kitu maishani kimepangiwa mapema au ni mapenzi ya Mungu na kwamba hatuwezi kubadili chochote. Kwa kusikitisha, maelezo yote hayo hayajatoa majibu yenye kuridhisha. Hiyo ni kwa sababu “mwanadamu [hawezi] kugundua kazi ambazo Mungu wa kweli amefanya tangu mwanzo mpaka mwisho,” inasema Biblia.

Ukweli wa kwamba wanadamu wana tamaa ya kujua mambo ya wakati ujao na hawawezi kupata majibu kumewasumbua wanafalsafa kwa muda mrefu sana. Hata hivyo, kwa kuwa Mungu ndiye ameweka tamaa hiyo katika mioyo yetu, je, si jambo linalopatana na akili kutazamia kwamba atatupa kile tunachohitaji ili kutosheleza tamaa hiyo? Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.” (Zaburi 145:16) Kwa kujifunza Neno la Mungu, Biblia, tunaweza kupata maelezo yenye kuridhisha kuhusu uhai na kifo na kuhusu kusudi la milele la Mungu kwa ajili ya dunia na jamii ya wanadamu.—Waefeso 3:11.

[Blabu katika ukurasa wa 5]

“Si wenye mbio wanaoshinda katika mbio.”—Mhubiri 9:11

[Blabu katika ukurasa wa 6]

Ikiwa mkulima hakupanda mimea yake wakati unaofaa, je, atasema hakupata mazao mazuri kwa sababu ya majaliwa?

[Blabu katika ukurasa wa 7]

Tunafikiria kuhusu uhai na kifo kwa sababu Mungu “ameweka milele . . . ndani ya mioyo” ya wanadamu