Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mti “Ambao Majani Yake Hayanyauki”

Mti “Ambao Majani Yake Hayanyauki”

Mti “Ambao Majani Yake Hayanyauki”

JE, UMEWAHI kuona eneo lenye miti mingi yenye majani mengi ya kijani? Huenda utakubali kwamba hiyo ni mandhari yenye kupendeza sana. Ukiona miti yenye majani makubwa, je, ungewazia kwamba kuna ukame katika eneo hilo? Bila shaka, unajua kwamba lazima kuwe na maji mengi ambayo yanafanya miti hiyo iwe hai na yenye afya.

Kwa kufaa, Biblia inalinganisha wale walio na afya nzuri kiroho na miti mikubwa na yenye majani mengi. Kwa mfano, ona simulizi hili lenye kupendeza lililo katika mistari mitatu ya kwanza ya Zaburi ya kwanza:

“Mwenye furaha ni mtu ambaye hakutembea katika shauri la waovu, na katika njia ya watenda-dhambi hakusimama, na katika kiti cha wenye dhihaka hakuketi. Bali mapendezi yake ni katika sheria ya Yehova, naye huisoma sheria yake kwa sauti ya chini mchana na usiku. Naye hakika atakuwa kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.”

Vivyo hivyo, katika Yeremia 17:7, 8, tunasoma hivi: “Amebarikiwa yule mtu hodari anayemtegemea Yehova, na ambaye Yehova amekuwa uhakika wake. Na hakika yeye atakuwa kama mti uliopandwa kando ya maji, unaopeleka mizizi yake kando ya mto; naye hataona joto linapoingia, bali kwa kweli majani yake yatakuwa mengi. Na katika mwaka wa ukame hatahangaika, wala hataacha kuzaa matunda.”

Katika maandiko hayo mawili, miti inatumiwa kuonyesha jinsi mtu anayefanya lililo sawa, anayefurahia sheria ya Mungu, na kumtegemea kikamili anavyokuwa. Hilo linatufanya tuulize, ni katika njia gani mtu anakuwa kama mti wenye majani mengi, kwa njia ya kiroho? Acheni tuchunguze mistari hiyo kwa makini.

“Uliopandwa Kando ya Vijito vya Maji”

Miti inayotajwa inafafanuliwa kuwa imepandwa “kando ya vijito vya maji” au “kando ya maji,” si kando ya mto au kijito kimoja tu. Maneno kama hayo yanapatikana katika Isaya 44:3, 4, ambapo Yehova Mungu alizungumzia jinsi ambavyo angewatunza Wayahudi waliotubu walitoka utekwani huko Babiloni. Kupitia nabii Isaya, Yehova alisema: “Nitamimina maji juu ya mwenye kiu, na vijito vinavyotiririka juu ya mahali pakavu. . . . Nao watachipuka kama katikati ya majani mabichi, kama mierebi kando ya mitaro ya maji.” Katika mistari hiyo, inasemwa kuwa “vijito” na “mitaro ya maji” inawafanya waliobarikiwa wasitawi kama mierebi yenye majani.

Hata leo katika maeneo ya mashambani, unaweza kuona mitaro ya maji na vijito vikitiririka kutoka kwenye chanzo kikubwa cha maji kama vile kisima chenye kina, mto, ziwa, au bwawa. Kwa kawaida, mitaro ya maji na vijito vinatumiwa kunyunyizia mashamba maji. Nyakati nyingine vinaelekeza maji kwenye shamba la miti ya matunda. Katika visa fulani, vijito vinanyunyizia mashamba kwenye upande mmoja na upande ule mwingine vinanyunyizia miti yenye majani mengi ambayo inaonyesha mpaka wa shamba.

Miti iliyopandwa kando ya vijito kama hivyo inakua jinsi gani? Zaburi 1:3 inaeleza kuhusu mti “ambao hutoa matunda yake katika majira yake.” Katika nchi zinazotajwa katika Biblia, kuna mitini, mikomamanga, mitofaa, mitende, na mizeituni. Ingawa mtini unaweza kukua kufikia kimo cha mita 9 na uwe na matawi yaliyoenea, miti mingine mingi ya matunda haikui kufikia kimo kirefu sana. Lakini inaweza kuwa na matawi mengi na yenye afya na kutokeza matunda mengi wakati unaofaa.

Katika nyakati za kale, mierebi mikubwa ilikua kando ya mito na vijito vya Siria na Palestina. Kwa kawaida, mierebi inapotajwa katika Biblia inahusianishwa na mito au ‘mabonde ya mito.’ (Mambo ya Walawi 23:40) Mivinje, ambayo ni ya jamii moja na mierebi, ingepatikana pia ikikua mahali penye maji mengi. (Ezekieli 17:5) Miti hiyo mikubwa na yenye matawi mengi inakazia wazo ambalo mtunga-zaburi na Yeremia walitaka kupitisha: Wale wanaojitahidi kufuata sheria ya Mungu na kumtegemea kikamili wataendelea kuwa na afya kiroho, ‘na kila jambo wanalofanya litafanikiwa.’ Bila shaka sisi sote tunataka kufanikiwa maishani, sivyo?

Kupendezwa na Sheria ya Yehova

Leo watu wanajaribu kupata mafanikio kwa njia nyingi. Wao wanajaribu kufuatilia vitu vinavyoweza kuwaletea umaarufu na utajiri, ambavyo mara nyingi haviwezi kupatikana na vinakatisha tamaa. Hata hivyo, ni nini kinachoweza kuleta uradhi wa kweli na furaha yenye kudumu maishani? Maneno ya Yesu kwenye Mahubiri ya Mlimani yanatupa jibu. Alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mathayo 5:3) Kwa kweli, furaha ya kweli inapatikana, si kwa kuwa na mali nyingi, bali kwa kutambua na kutosheleza mahitaji yetu ya kiroho ili tuwe na afya ya kiroho, kama miti yenye majani mengi inayotoa matunda katika majira yanayofaa. Tunaweza kusitawi kiroho namna gani?

Kulingana na mtunga-zaburi, kwanza kuna mambo fulani tunayopaswa kuepuka. Alitaja kuhusu “shauri la waovu,” “njia ya watenda-dhambi,” na “kiti cha wenye dhihaka.” Ili tuwe na furaha tunapaswa kuwaepuka wale wanaodhihaki au kupuuza sheria za Mungu.

Kisha tunapaswa kupendezwa na sheria ya Yehova. Tunapopendezwa na kitu au utendaji fulani, tunatafuta nafasi zote za kushiriki kuufanya, sivyo? Kwa hiyo, kupendezwa na sheria ya Mungu kunamaanisha kwamba tunapaswa kulithamini sana Neno la Mungu, tutamani kujifunza zaidi kuhusu neno hilo na kulielewa zaidi.

Mwishowe, tunapaswa kulisoma “kwa sauti ya chini mchana na usiku.” Hilo linamaanisha kwamba tunapaswa kusoma Biblia kwa ukawaida na kutafakari mambo tunayosoma. Kuhusu Neno la Mungu, tunapaswa kuhisi kama mtunga-zaburi alivyoimba: “Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia mchana kutwa.”—Zaburi 119:97.

Naam, tunapopata ujuzi sahihi na uelewaji wa Yehova Mungu na kumtegemea kikamili na ahadi zake, bila shaka tutakuwa na afya ya kiroho. Kwa kufanya hivyo, tutakuwa kama yule mtu mwenye furaha aliyefafanuliwa na mtunga-zaburi—“kila jambo analofanya litafanikiwa.”