Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nayajua Vizuri Maumivu Waliyo Nayo”

“Nayajua Vizuri Maumivu Waliyo Nayo”

Mkaribie Mungu

“Nayajua Vizuri Maumivu Waliyo Nayo”

Kutoka 3:1-10

“MTAKATIFU, mtakatifu, mtakatifu ni Yehova.” (Isaya 6:3) Maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu yanaonyesha kwamba Yehova Mungu ni safi na ametakata kwa njia isiyo na kifani. Huenda ukauliza, ‘Je, utakatifu huo unamfanya asijali na asiweze kufikika? Je, Mungu mtakatifu kama huyo anaweza kweli kumjali mwanadamu mwenye dhambi na asiye mkamilifu kama mimi?’ Acheni tuchunguze maneno yenye kutia moyo ambayo Mungu alimwambia Musa, yaliyorekodiwa katika Kutoka 3:1-10.

Siku moja alipokuwa akichunga kondoo, Musa aliona jambo lisilo la kawaida, mti fulani wa miiba ulikuwa ukiwaka moto lakini “haukuwa ukiteketea.” (Mstari wa 2) Akitaka kujua kilichokuwa kikifanyika, aliukaribia. Akitumia malaika, Yehova alizungumza na Musa kutoka katikati ya moto: “Usikaribie hapa. Vua viatu vyako kutoka miguuni, kwa sababu mahali ambapo umesimama ni udongo mtakatifu.” (Mstari wa 5) Fikiria hilo, kwa kuwa mti huo wa miiba uliwakilisha kuwapo kwa Mungu, mahali hapo pakawa patakatifu!

Mungu mtakatifu alikuwa na sababu ya kuzungumza na Musa. Mungu alisema: “Pasipo shaka nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; kwa sababu nayajua vizuri maumivu waliyo nayo.” (Mstari wa 7) Mungu aliyaona mateso ya watu wake, na alisikia vilio vyao vya kuomba msaada. Alifanya huzuni yao iwe yake. Ona kwamba Mungu alisema: “Nayajua vizuri maumivu waliyo nayo.” Kuhusu maneno hayo “nayajua vizuri,” kitabu kimoja kinasema: “Maneno hayo yanaonyesha hisia za kibinafsi, wororo, na huruma.” Maneno ambayo Yehova alimwambia Musa yanaonyesha kwamba yeye ni Mungu anayejali sana.

Mungu angefanya nini? Hakuwasikitikia tu au kuwasikiliza tu kwa huruma. Alichochewa kutenda. Alikusudia kuwakomboa watu wake kutoka Misri na kuwaleta katika “nchi inayotiririka maziwa na asali.” (Mstari wa 8) Ili afanye hivyo, Yehova alimwagiza Musa hivi: “Uwatoe watu wangu . . . kutoka Misri.” (Mstari wa 10) Akitii agizo hilo, Musa aliwatoa Waisraeli kutoka Misri mnamo 1513 K.W.K.

Yehova hajabadilika. Waabudu wake leo wanaweza kuwa na uhakika kwamba anaona taabu zao na anasikia vilio vyao vya kuomba msaada. Anajua vizuri maumivu yao. Lakini Yehova hawahurumii tu watumishi wake waliojitoa. Mungu mwenye wororo anachochewa kutenda kwa ajili yao kwa sababu “anawajali.”—1 Petro 5:7.

Huruma za Mungu zinatupa sababu ya kuwa na tumaini. Kwa msaada wake, sisi wanadamu wasio wakamilifu tunaweza kuwa watakatifu kwa kadiri fulani na kupata kibali chake. (1 Petro 1:15, 16) Mwanamke mmoja Mkristo ambaye amekabiliana na mshuko wa moyo na kuvunjika moyo alifarijiwa na simulizi la Musa kwenye mti wa miiba. Anasema: “Ikiwa Yehova anaweza kufanya ardhi iwe takatifu, basi huenda nina tumaini. Wazo hilo limenisaidia sana.”

Je, unachochewa kujifunza mengi zaidi kumhusu Mungu mtakatifu, Yehova? Unaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye, kwa kuwa Yehova “analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.”—Zaburi 103:14.