Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Waathiriwa wa Tufani wa Myanmar Wapata Msaada

Waathiriwa wa Tufani wa Myanmar Wapata Msaada

Waathiriwa wa Tufani wa Myanmar Wapata Msaada

MEI 2, 2008, (2/5/2008) Tufani Nargis ilipiga nchi ya Myanmar kwa nguvu sana na upesi tukio hilo likaripotiwa katika vyombo vya habari vya kimataifa. Iliripotiwa kwamba karibu watu 140,000 walikufa au wakatoweka baada ya mawimbi makubwa kupiga Delta ya Irrawaddy.

Kwa kushangaza, hakuna Shahidi yeyote wa Yehova katika eneo hilo aliyeumizwa. Kwa kadiri kubwa, waliokoka kwa sababu walijikinga katika Majumba ya Ufalme yaliyojengwa vizuri. Katika eneo moja, Mashahidi 20 na wanakijiji wengine 80 waliketi juu ya paa la Jumba la Ufalme kwa saa tisa huku kiwango cha maji ya mafuriko kikipanda na kufikia mita 5 hivi. Wote waliokoka. Kwa kusikitisha, watu wengine 300 katika kijiji hicho walikufa. Katika vijiji vingi, Jumba la Ufalme tu ndilo jengo lililobaki likiwa limesimama.

Siku mbili baada ya tufani hiyo, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huko Yangon ilituma kikundi cha kutoa msaada kwenye kutaniko la Bothingone, lililo kwenye mlango wa delta hiyo. Wakipitia maeneo yaliyoharibika sana huku wakihepa waporaji, na kupita miili iliyokuwa ikioza, washiriki wa kikundi hicho walifika Bothingone wakiwa na mchele, tambi zilizokaushwa, maji, na mishumaa. Hicho ndicho kilikuwa kikundi cha kwanza cha kutoa msaada kuwasili kwenye eneo hilo. Baada ya kuwapa Mashahidi wa eneo hilo msaada, kikundi hicho kilitoa hotuba za Biblia ili kuwatia moyo na kikawaachia Biblia na vichapo vinavyozungumzia Biblia, kwa kuwa mali zote za Mashahidi hao zilikuwa zimefagiliwa mbali na tufani hiyo.

Mashahidi walioathiriwa na tufani hiyo walikuwa na mtazamo wenye kustaajabisha. Shahidi mmoja katika kutaniko moja lililo katika eneo la Irrawaddy lililoathiriwa alisema: “Kila kitu tulichokuwa nacho kimepotea. Nyumba zetu zote zimeharibiwa. Mimea yetu yote imeharibiwa. Maji yote ya kunywa yamechafuliwa na mafuriko. Hata hivyo, ndugu na dada hawana wasiwasi kama watu wengine. Wanamtegemea Yehova na tengenezo lake. Tutatii mwongozo wowote tunaopewa iwe ni kukaa hapa au kuhamia mahali pengine.”

Kikundi cha Mashahidi 30 ambao walipoteza kila kitu, waliimba kwa shangwe nyimbo za Ufalme walipokuwa wakisafiri kwa muda wa saa kumi kuelekea mahali vikundi vya kutoa msaada vilikuwa vimewaandalia chakula, mavazi, na mahali pa kuishi. Kabla ya kufika mahali walipokuwa wakienda, walisikia kwamba kulikuwa na kusanyiko la mzunguko la Mashahidi wa Yehova katika mji uliokuwa karibu. Waliamua kuhudhuria kusanyiko hilo kwanza ili wapate chakula cha kiroho na wafurahie ushirika wa Kikristo.

Nyumba 35 za Mashahidi wa Yehova ziliharibiwa, huku nyumba 125 na Majumba 8 ya Ufalme yakaharibiwa kidogo katika eneo hilo lililopigwa na tufani. Kwa kupendeza, ofisi ya tawi haikuathiriwa sana.

Mwanzoni, haingewezekana kufika kwenye ofisi ya tawi kwa kuwa tufani hiyo iliangusha miti mikubwa kwenye barabara zilizokuwa karibu. Saa chache tu baada ya tufani hiyo kwisha, zaidi ya wafanyakazi 30 wa ofisi hiyo waliondoa miti hiyo kwa mikono. Walipokuwa wakifanya kazi, watu walisimama kando wakistaajabu. Baada ya muda mfupi, kikundi cha wanawake Mashahidi kiliwasili kikiwa na vinywaji baridi na matunda kwa ajili ya wafanyakazi hao na majirani ambao hawangeweza kuamini macho yao. Mwandishi wa habari alipoona kilichokuwa kikitukia, aliuliza, “Watu hawa wanaofanya kazi kwa utaratibu hivyo ni akina nani?” Alipojibiwa alisema hivi, “Afadhali watu wengi wangekuwa na roho ya ushirikiano kama Mashahidi wa Yehova!”

Mashahidi walianzisha halmashauri mbili za kutoa msaada katika sehemu mbalimbali za nchi hiyo ili kusimamia kazi ya kutoa msaada. Mamia ya wajitoleaji walifanya kazi katika vikundi vya kutoa msaada. Baada ya siku chache, Mashahidi waliopoteza nyumba zao walijengewa mpya. Kikundi kimoja cha kutoa msaada kilipofika kumjengea Shahidi fulani nyumba mpya, majirani wake walisimama na kutazama kwa mshangao. Jirani mmoja alisema: “Mwanamke huyu Shahidi anajengewa nyumba na kanisa lake. Hakuna yeyote kati ya rafiki zangu Wabudha aliyekuja kunisaidia. Afadhali ningekuwa Shahidi mwanamke huyo aliponihubiria!”

Wafanyakazi wa kujitolea na halmashauri ya kutoa msaada ilipofika katika eneo la Thanlyn ili kuchunguza nyumba moja ambayo ilikuwa imeharibika sana, waliguswa moyo sana familia hiyo ya Mashahidi ilipowaambia hivi: “Hakuna kitu kimetukia hapa. Msihangaike sana kuhusu nyumba yetu. Tunaweza kuishi hapa. Mashahidi fulani hawana hata nyumba. Nendeni mkawasaidie!”

Katika eneo moja la Yangon, watu fulani walijaribu kwenda kujificha katika kanisa moja. Hata hivyo, mlango wa kanisa hilo ulikuwa umefungwa na hakuna mtu angeweza kuingia ndani. Watu walikasirika sana na wakataka kuvunja mlango wa kanisa hilo. Tofauti na hilo, Mashahidi wa Yehova waliwasaidia watu wengi kujificha katika Majumba ya Ufalme wakati wa tufani hiyo. Kwa mfano, kwenye Jumba la Ufalme la Dala, wenzi wa ndoa ambao ni Mashahidi waliwaficha majirani 20 waliokuwa wamekimbilia huko ili wapate usalama. Asubuhi, watu hao hawangeweza kurudi nyumbani, na walikuwa na njaa. Shahidi huyo alipata mtu aliyekuwa akiuza mchele na akanunua kiasi kinachotosha kuwalisha watu hao wote.

Washiriki fulani wa familia moja huko Yangon ni Mashahidi wa Yehova na wengine ni wa makanisa mbalimbali. Baada ya tufani hiyo, familia hiyo yote ilihudhuria mkutano kwenye Jumba la Ufalme. Kwa nini? Mshiriki mmoja wa familia hiyo alieleza hivi: “Viongozi wa kanisa letu walisema wangetutembelea baada ya dhoruba hiyo, lakini hawakuja. Ni Mashahidi tu waliotutembelea. Mlituletea mchele na maji. Ninyi ni tofauti na makanisa mengine!” Washiriki wa familia hiyo ambao si Mashahidi walifurahia kujifunza makala ya Mnara wa Mlinzi yenye kichwa “Yehova Anasikia Vilio Vyetu vya Kuomba Msaada” na hata walitoa maelezo mengi.

Mwanamke mmoja aliyekuwa akijifunza Biblia na Mashahidi alihudhuria mkutano juma moja baada ya tufani hiyo. Wakati wa mkutano, barua kutoka ofisi ya tawi ilisomwa ikieleza mambo yaliyokuwa yamefanywa ili kusaidia na mambo yaliyoonwa na wale waliookoka tufani hiyo. Barua hiyo ilipokuwa ikisomwa, mwanamke huyo alianza kulia. Alivutiwa sana na kufurahi kusikia kwamba Mashahidi wote walikuwa salama. Baada ya hapo, alipewa msaada wa bidhaa fulani na akajengewa hema karibu na nyumba yake. Alisema kwamba alihisi Mashahidi walimtunza vizuri.

Yesu alisema: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.” (Yohana 13:35) Na mwanafunzi Yakobo alikazia kwamba imani ya kweli inaonyeshwa kwa matendo mazuri. (Yakobo 2:14-17) Mashahidi wa Yehova wanachukua maneno hayo kwa uzito na kujitahidi kuonyesha upendo kama huo kwa kuwasaidia na kuwategemeza watu wenye uhitaji.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Biblia inasema kwamba imani ya kweli inaonyeshwa kwa matendo mazuri