Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jilinde Ili Pepo Wasikudhuru

Jilinde Ili Pepo Wasikudhuru

Jilinde Ili Pepo Wasikudhuru

JAMES alilelewa katika maeneo ya mbali ya kisiwa kimoja cha Visiwa vya Solomon kinachoitwa Malaita. Tangu utotoni alifundishwa kuwaheshimu pepo, au roho. Anasema hivi: “Sikufikiria kamwe kuwaomba pepo wawaumize wengine, lakini sikuamini kwamba ningeweza kufurahia maisha bila kutumia rarafono [mila za kuomba msaada wa pepo] ili kuepuka madhara.”

Watu wa Visiwa vya Solomon, kama vile watu wa sehemu nyingi za dunia, wanaamini kwamba pepo wanaweza kumsaidia au kumdhuru mtu. Wamelanesia wengi hawaogopi pepo wanaoonwa kuwa wazuri, bali wanawapenda.

Watu wanazifuata desturi nyingi mbalimbali kwa sababu wanaamini pepo. Kwa mfano, James alipokuwa mtoto, wanawake katika kijiji chao waliwaingiza watoto ndani ya nyumba haraka waliposikia kilio cha ndege anayeitwa korokoro (ndege wa jamii ya kukuu). Walifanya hivyo kwa sababu waliamini kwamba kilio cha ndege yule kilimaanisha kwamba mtu angepatwa na madhara.

Baadhi ya wanakijiji hao wanaweka jiwe jeupe la pekee juu ya mlango wa nyumba zao. James alifanya hivyo kwa sababu aliamini kwamba lile jiwe lingemlinda na pepo wabaya. Pia, James alipokuwa kazini alikusanya mabaki yote ya chakula chake cha mchana na kuyaweka katika mfuko ili ayatupe baadaye. Alifanya hivyo kwa sababu alikuwa na wasiwasi kwamba mchawi angeyapata na kuyatumia kumroga ili awe mgonjwa.

Labda mila kama hizo si za kawaida katika eneo lenu, lakini huenda unahisi kama James kwamba ni muhimu kufuata mila fulani ili pepo wasikudhuru. Huenda unaamini kwamba usipofuata mila hizo utapatwa na madhara.

Ikiwa unaamini Biblia, bila shaka unataka kujua inavyosema kuhusu maswali yafuatayo: (1) Pepo wanaweza kukudhuru kwa njia gani? (2) Je, pepo wanaweza kukudhuru kwa sababu unafuata mila fulani? (3) Unaweza kupata ulinzi wa kweli jinsi gani ili uwe mwenye furaha?

Jinsi Pepo Wanavyowadhuru Watu

Biblia inaonyesha kwamba pepo si roho za wafu. Neno la Mungu linasema hivi: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Pepo ni malaika walioasi ambao wamemuunga mkono Shetani kujaribu kuwapotosha wanadamu.—Ufunuo 12:9.

Maandiko yanaonyesha wazi kwamba tunahitaji ulinzi ili pepo wasitudhuru. Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo huko Efeso hivi: “Tuna kushindana mweleka, si juu ya damu na mwili, bali juu ya . . . majeshi ya roho waovu [pepo] katika mahali pa kimbingu.” Mtume Petro alisema kwamba mtawala wa pepo, Shetani Ibilisi ni kama “simba anayenguruma, akitafuta kummeza mtu.”—Waefeso 6:12; 1 Petro 5:8.

Shetani anawadhuru watu hasa kwa kuwapotosha, kuwadanganya, au kuwashawishi watende kwa njia inayomchukiza Mungu. Biblia inasema kwamba Shetani “huendelea kujigeuza mwenyewe kuwa malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:14) Anajifanya kuwa roho anayelinda, lakini anataka kutudhuru. Shetani anapofusha watu wasione ukweli kumhusu yeye wala kumhusu Mungu. (2 Wakorintho 4:4) Lengo lake ni nini anapowapotosha watu?

Shetani anatamani watu wamwabudu, wawe wanajua au hawajui. Mwana wa Mungu, Yesu, alipokuwa duniani, Shetani alitaka ‘amfanyie tendo la ibada.’ Yesu akamwambia: “Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu.’” (Mathayo 4:9, 10) Yesu alikataa kufanya tendo lolote lile ambalo lingeonyesha kwamba anamwabudu Shetani.

Yehova ni roho mwenye nguvu kuliko roho wengine wote, naye hataruhusu madhara ya kudumu kuwapata wale wanaomtii. (Zaburi 83:18; Waroma 16:20) Tukitaka kumpendeza Yehova Mungu kama Yesu alivyofanya, ni lazima tuepuke kumwabudu Shetani kwa kumtii au kuwatii mashetani wake. Ili tuepuke kumtii Shetani na mashetani ni lazima tutambue mila zinazohusisha kuwaabudu au kuwaheshimu. Unaweza kuzitambua kwa njia gani?

Tambua Mila Zinazomchukiza Mungu

Yehova Mungu aliwaonya watu wake wa kale, Waisraeli, wasiige mila za mataifa jirani. Alisema hivi: “Asipatikane ndani yako yeyote . . . anayefanya uaguzi, mwenye kufanya uchawi au yeyote anayetafuta ishara za bahati au mlozi, au anayefunga wengine kwa kuwatakia maovu.” Biblia inasema hivi kuwahusu wale waliofuata desturi hizo: “Kwa maana kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova.”—Kumbukumbu la Torati 18:10-12.

Kwa hiyo, unapochunguza mila zilizo za kawaida katika eneo lenu, jiulize maswali yafuatayo: Je, mila hii inamfanya mtu aamini ishara za bahati mbaya? Je, inafuatwa kwa sababu watu wanaamini kwamba vitu visivyo hai vina nguvu za kichawi za kulinda? Je, inahusisha kuroga au kulinda mtu asirogwe? Je, inahusisha tendo la kumtii roho mwingine isipokuwa Yehova au Yesu, mwakilishi wake aliyewekwa?—Waroma 14:11; Wafilipi 2:9, 10.

Ni muhimu kukataa mila zote zinazohusisha desturi kama hizo. Kwa nini? Mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Hamwezi kuwa mkishiriki ‘meza ya Yehova’ na meza ya roho waovu.” Alionya kwamba wale wanaojaribu kumpendeza Mungu na vilevile roho wengine ‘wangemchochea Yehova awe na wivu.’ (1 Wakorintho 10:20-22) Yehova Mungu anastahili ibada isiyohusisha yeyote mwingine na anataka watu wake wajitoe kikamili.—Kutoka 20:4, 5.

Fikiria swali hili pia: Je, ile mila inaendeleza wazo la kwamba mtu hawezi kulaumiwa kwa matendo yake? Kwa mfano, uzinzi na ngono kabla ya ndoa zinashutumiwa katika jamii nyingi na vilevile katika Biblia. (1 Wakorintho 6:9, 10) Hata hivyo, katika baadhi ya jamii za eneo la Pasifiki, mazoea kama hayo yanakubalika msichana akisema kwamba “amerogwa kwa jani la kijani kibichi,” * yaani, akisema kwamba alilazimika kufanya ngono kwa sababu amerogwa.

Hata hivyo, Biblia inafundisha kwamba sisi tutatozwa hesabu kwa matendo yetu. (Waroma 14:12; Wagalatia 6:7) Kwa mfano, mwanamke wa kwanza, Hawa, alihisi kwamba alishawishiwa na Shetani kumuunga mkono na kutomtii Mungu. Alisema: “Yule nyoka—alinidanganya nami nikala.” Hata hivyo, Yehova alimwadhibu Hawa kupatana na matendo yake. (Mwanzo 3:13, 16, 19) Pia atatutoza hesabu kupatana na matendo yetu.—Waebrania 4:13.

Unapaswa Kufanya Nini?

Ukitaka kumpendeza Mungu na kuishi kupatana na kanuni za Biblia itakubidi kuchukua hatua bila kuchelewa. Watu wenye moyo mweupe walioishi huko Efeso katika karne ya kwanza walionyesha mfano mzuri kuhusiana na jambo hilo. Ili kujiepusha na uvutano wa pepo, walikusanya vitabu vyao vyote vilivyohusu desturi za uchawi na “wakaviteketeza mbele ya kila mtu.”—Matendo 19:19.

Kabla ya kuteketeza vitabu vyao, watu hao walikuwa “wanakuja na kuungama na kueleza juu ya mazoea yao waziwazi.” (Matendo 19:18) Paulo alipowafundisha kumhusu Kristo waliguswa moyoni, wakasukumwa kuviharibu vitabu vyao vya uchawi. Pia walibadili maoni yao kuhusu mila zao.

Kuacha mila si rahisi. James aliyetajwa mapema alikabili uamuzi mgumu wa kuacha mila. Alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na alipenda yale aliyojifunza. Hata hivyo, aliendelea kufuata mila ya rarafono. Alipojichunguza kuhusiana na mila hiyo, alitambua kwamba aliamini ahadi za Yehova kuhusu wakati ujao, lakini alifikiri kwamba bado anahitaji kutegemea mila ili kupata ulinzi.

Ni nini kilichomsaidia James kubadili maoni yake? Anasema hivi: “Nilimwomba Yehova anilinde na anisaidie kumtegemea. Wakati uo huo, niliacha mila.” Je, alipatwa na madhara yoyote? James anasema: “Hapana. Nimejifunza kumtegemea Yehova. Nimetambua kwamba Yehova anaweza kuwa rafiki wa karibu sana.” James amekuwa mtumishi wa wakati wote kwa miaka saba na anawafundisha wengine kweli za Biblia.

Tunakutia moyo ufuate mfano wa James. Chunguza mila za kawaida za jamii yako, na utumie ‘nguvu zako za kufikiri’ kuona kama zinapatana na “mapenzi ya Mungu.” (Waroma 12:1, 2) Kisha jipe moyo na ujiepushe na desturi zote za ushirikina. Ukifanya hivyo, unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ‘atakukaribisha’ na kukulinda. (2 Wakorintho 6:16-18) Kama James utaona ukweli wa ahadi hii ya Biblia: “Jina la Yehova ni mnara wenye nguvu. Mwadilifu hukimbilia humo na kupewa ulinzi.”—Methali 18:10.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 18 Msemo huo unamaanisha kwamba msichana alipewa jani au chakula kilichorogwa. Lile jani au chakula kinadhaniwa kumfanya yule msichana avutiwe na mwanamume fulani. Desturi hii si sawa na kumpa msichana dawa za kulevya bila yeye kujua, kisha kumlazimisha kufanya ngono kinyume cha mapenzi yake. Katika kisa hiki cha pili msichana hana hatia.

[Picha katika ukurasa wa 19]

“Korokoro”

[Hisani]

Courtesy of Dr. Bakshi Jehangir

[Picha katika ukurasa wa 19]

Msichana anakusanya mabaki ya chakula ili yasitumiwe kumroga