Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Kweli Kuna Yeyote Anayejali?

Je, Kweli Kuna Yeyote Anayejali?

Je, Kweli Kuna Yeyote Anayejali?

Je, umewahi kujihisi ukiwa mpweke na huna msaada, kana kwamba hakuna mtu anayeelewa kikweli matatizo unayokabili? Na hata ikiwa watu walijua, ulihisi ni kana kwamba hawakujali.

MATATIZO yanapotupata, maisha yetu huonekana kama dhoruba ambayo haitakwisha. Nyakati nyingine, tunaweza hata kukata kauli kwamba kile kinachotupata ni kibaya sana na ni uonevu hivi kwamba tunashindwa kuvumilia. Mara nyingi hali huwa hivyo tunapopatwa na matatizo ya kihisia, kushuka moyo, aksidenti mbaya, magonjwa wa kudumu, au mambo kama hayo. Huenda tukajihisi hatuna uwezo na tumaini hivi kwamba tujiulize tutapata wapi faraja. Je, kweli kuna yeyote anayejali?

“Mungu wa Faraja Yote” Anajali

Mungu anafafanuliwa katika Biblia kuwa “Baba ya rehema nyororo na Mungu wa faraja yote.” (2 Wakorintho 1:3) Mungu, ambaye jina lake ni Yehova, anajua tunahitaji faraja. Biblia hutumia neno “faraja” mara zaidi ya 100 katika njia mbalimbali kutuhakikishia kwamba Mungu haelewi tu mambo tunayokabili bali pia anatamani kutufariji. Ujuzi huo unatuhakikishia kwamba hata wengine wasipoona, wasipoelewa, au kujali hali yetu mbaya, Yehova Mungu anajali.

Ukweli wa kwamba Yehova anawajali watu mmoja-mmoja unaonekana katika Maandiko. “Macho ya Yehova yako kila mahali,” Biblia inasema, “yakiwaangalia wabaya na wema.” (Methali 15:3) Vivyo hivyo, tunasoma hivi katika Ayubu 34:21: “Macho yake yako juu ya njia za mwanadamu, naye huziona hatua zake zote.” Yehova anaona mambo tunayofanya yawe ni mambo mazuri au mabaya na anatambua hali zetu ili aweze kutenda kwa njia anayotaka. Hilo linaweza kuonekana katika maneno haya ambayo nabii Hanani alimwambia Mfalme Asa wa Yuda: “Kwa habari ya Yehova, macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.”—2 Mambo ya Nyakati 16:7, 9.

Yehova hutuangalia kwa sababu nyingine pia. Yesu anaeleza: “Hakuna mtu anayeweza kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute.” (Yohana 6:44) Yehova anajali sana hivi kwamba anauchunguza moyo wa mtu ili aone ikiwa mtu huyo anapendezwa kumfahamu Mungu vizuri zaidi. Ikiwa mtu huyo anataka, anaweza kumsaidia kwa njia zenye kupendeza. Kwa mfano, katika Jamhuri ya Dominika, mwanamke mmoja alikuwa amelazwa hospitalini ili afanyiwe upasuaji wa kansa. Alimsihi Mungu amsaidie kupata dini ya kweli. Wakati huo, mume wake alimletea broshua yenye kichwa Mungu Anataka Tufanye Nini? * ambayo alikuwa amepewa asubuhi hiyo na Mashahidi wa Yehova waliokuwa wamemtembelea nyumbani. Mwanamke huyo alisoma broshua hiyo na kutambua kwamba Mungu alikuwa akijibu sala yake. Alikubali kujifunza Biblia na Shahidi huyo, na aliweka maisha yake wakfu kwa Mungu na kubatizwa katika muda usiozidi miezi sita.

Katika kitabu cha Biblia cha Zaburi, tunapata maneno mengi yenye kuchangamsha ya watunga-zaburi wa kale, kama vile Mfalme Daudi, ambayo yanaonyesha jinsi Yehova alivyowatunza watumishi wake kwa upendo. Kwenye Zaburi 56:8 tunaona Mfalme Daudi akimsihi Mungu hivi: “Uyaweke machozi yangu katika kiriba chako. Je, hayamo katika kitabu chako?” Kutokana na ulinganisho huo wa kuhifadhi kitu chenye thamani katika kiriba, Daudi alijua kwamba Yehova alijua si kuhusu kuteseka kwake tu bali alijua pia jinsi kuteseka huko kulivyomwathiri kihisia. Yehova alielewa maumivu ya Daudi na kukumbuka kile ambacho Daudi alikabiliana nacho kihisia kilichomfanya atoe machozi. Kwa kweli, Muumba wetu huwatazama wote wanaojitahidi kufanya mapenzi yake “ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.”

Simulizi lingine la Biblia linalofafanua jinsi Mungu anavyowatunza watu kwa upendo ni Zaburi ya 23 inayojulikana sana. Maneno ya kwanza yanamfananisha Mungu na mchungaji mwenye upendo: “Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote.” Mchungaji huko Mashariki ya Kati anatunza kila mmoja wa kondoo zake, hata anawapa majina. Kila siku yeye humwita kila kondoo na kumpapasa kwa upendo na kumchunguza ikiwa ana majeraha. Akipata majeraha yoyote, yeye humpaka mafuta au dawa ili kumfanya apone haraka. Ikiwa kondoo ni mgonjwa, mchungaji atamlazimisha ameze dawa na kumwinua ili asilale na kufa. Kwa kweli, hayo ni maneno yenye kupendeza sana ya jinsi Yehova anavyowajali wale wanaomtumikia.

Sala na Ufufuo —Uthibitisho Kwamba Mungu Anajali

Zaburi hizo na nyingine nyingi hazijaandikwa katika Biblia ili tu tufurahie kuzisoma. Zinatuonyesha jinsi watumishi waaminifu wa Mungu wa kale walivyo mmiminia Yehova mioyo yao na kumweleza kwamba walihitaji msaada wake na pia wakatoa shukrani kwa ajili ya mwongozo na baraka zake. Maneno kama hayo yanaonyesha wazi kwamba watumishi hao wa kale wa Mungu waliamini kwa uthabiti kwamba Mungu aliwajali. Kusoma na kutafakari kuhusu maneno hayo ya kutoka moyoni kunaweza kutusaidia kuhisi vivyo hivyo kumhusu Mungu. Uandalizi wa sala ni uthibitisho wenye nguvu kwamba Mungu anajali.

Hata hivyo, nyakati nyingine tunazidiwa sana na tatizo hivi kwamba hata hatujui jinsi ya kusali kulihusu. Je, hilo linamzuia Yehova asijue mahangaiko yetu? Waroma 8:26 inasema: “Roho pia hujiunga kutoa msaada kwa ajili ya udhaifu wetu; kwa maana lile tatizo kuhusu tunalohitaji kusali hatujui, lakini roho yenyewe hutuombea pamoja na kuugua kusikotamkwa.” Andiko hilo linatuambia kwamba sala za watumishi wa Mungu katika nyakati za kale zilizoongozwa kwa roho ya Mungu zinaweza kulingana na hisia zetu na hivyo kumfanya Yehova, yule “msikiaji wa sala,” azikubali kana kwamba ni zetu.—Zaburi 65:2.

Tumaini la ufufuo ni uthibitisho mwingine wenye kusadikisha kwamba Mungu anapendezwa na kila mtu. Yesu Kristo alisema hivi: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake [Yesu] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Neno la Kigiriki linalotumiwa hapo linatafsiri kwa usahihi “makaburi ya ukumbusho” na si “makaburi” tu. Linatoa wazo la kwamba maisha ya mtu ambaye amekufa yanakumbukwa na Mungu.

Hebu fikiria, ili kumfufua mtu, lazima Mungu ajue kila kitu kumhusu kutia ndani, sura yake, tabia alizorithi na zile alizojifunza, na kumbukumbu lake lote! (Marko 10:27) Kumbukumbu la Mungu la mtu huyo halipotei hata baada ya maelfu ya miaka. (Ayubu 14:13-15; Luka 20:38) Kwa hiyo, kila jambo kuwahusu mabilioni ya watu ambao wamekufa liko katika kumbukumbu la Yehova Mungu—na huo ni uthibitisho wenye kusadikisha kwamba Mungu anatujali sisi mmoja-mmoja!

Yehova Ni Mthawabishaji

Tunapaswa kufanya nini ili tutunzwe na Mungu? Lazima kwanza tuonyeshe kwamba tunamtegemea na kumtii na kwamba tunamwamini. Mtume Paulo anaonyesha uhusiano kati ya kuwa na imani na kutunzwa na Mungu. Aliandika: “Bila imani haiwezekani kamwe kumpendeza vema, kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—Waebrania 11:6.

Ona kwamba aina ya imani inayompendeza Mungu inahusisha mambo mawili. Kwanza, lazima ‘tuamini kwamba yeye yuko’ yaani, lazima tuamini kwamba kuna Mungu na kwamba yeye ndiye Mtawala Mkuu Kuliko Wote, anayestahili utii na ibada yetu. Pili, lazima tuamini kwamba yeye ni “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” Imani ya kweli inatia ndani kuamini kwamba Mungu anapendezwa na maisha ya wote wanajitahidi kwa moyo mweupe kufanya mapenzi yake na kwamba anawathawabisha. Kwa kujifunza Neno la Mungu na kushirikiana na wale wanaomtii, wewe pia unaweza kustahili kuthawabishwa na kutunzwa na Mungu kwa sababu ya imani yako.

Watu wengi leo wanaamini kwamba Mungu hapendezwi na mambo ya wanadamu. Lakini kama vile tumeona, Biblia inaonyesha wazi kabisa kwamba Mungu anapendezwa sana na wale wanaoonyesha kwamba wanamwamini kikweli. Hata ingawa mara nyingi leo maisha yamejaa huzuni, mahangaiko, kukatishwa tamaa, na maumivu, hatuhitaji kuvunjika moyo. Yehova Mungu anajali. Kwa kweli, anatukaribisha kwa upendo ili atutegemeze. “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza,” akasema mtunga-zaburi. “Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.”—Zaburi 55:22.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 7 Iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29]

Maandiko Yanayoimarisha Imani Yako Kwamba Mungu Anakupenda na Anakujali

“Kwa habari ya Yehova, macho yake yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.”—2 MAMBO YA NYAKATI 16:9

“Uyaweke machozi yangu katika kiriba chako. Je, hayamo katika kitabu chako?”—ZABURI 56:8

“Yehova ni Mchungaji wangu. Sitakosa chochote.”—ZABURI 23:1

“Ee msikiaji wa sala, kwako wewe watu wote wenye mwili watakuja.”—ZABURI 65:2

“Wewe utaita, na mimi mwenyewe nitakujibu. Kwa kuwa utaitamani sana kazi ya mikono yako.”—AYUBU 14:15

“Kwa maana yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.”—WAEBRANIA 11:6

“Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza. Hatamwacha kamwe mwadilifu atikisike.”—ZABURI 55:22