Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kutafuta Msaada Unaofaa

Kutafuta Msaada Unaofaa

Kutafuta Msaada Unaofaa

IWAPO unatafuta mashauri, yanapatikana kwa wingi. Biashara ya kutayarisha video na kuandika vitabu vyenye mashauri ya jinsi ya kujisaidia mwenyewe, ndiyo inayositawi kwa haraka zaidi ulimwenguni. Vitabu hivyo vinauzwa kwa wingi sana katika nchi kama vile Uingereza, Amerika ya Latini, Japani, na Marekani. Pia, video, mikutano, na vipindi vya televisheni vinavyozungumzia jinsi ya kujisaidia mwenyewe vimeanza kupendwa sana. Watu wanapenda mashauri hayo kwa sababu wanaamini kwamba yanaweza kuwasaidia kutatua matatizo yao bila kutafuta msaada kutoka kwa wanasaikolojia, washauri wa ndoa, au viongozi wa dini. Watu hao wanapata mashauri ya aina gani?

Kupata uradhi, kufurahia uhusiano wa kimapenzi, na kulea watoto ndiyo mambo yanayozungumziwa sana katika miongozo hiyo. Mambo mengine yanayozungumzia sana ni kushuka moyo, huzuni, na matokeo ya talaka. Pia watu wengi wanatafuta mashauri kuhusu jinsi ya kukabiliana na kula kupita kiasi, kuvuta sigara, na ulevi. Je, mashauri wanayopata yanafaa? Si wakati wote. Kwa hiyo, ni jambo la hekima kufikiria onyo hili la Biblia: “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake.”—Methali 14:15.

Vitabu vyenye mashauri ya jinsi ya kujisaidia mwenyewe ni tofauti sana na vitabu vya maelekezo vinavyofundisha mambo kama upigaji picha, uhasibu, au lugha. Mtu anaweza kusoma vitabu hivyo vya maelekezo ambavyo si vya bei ya juu badala ya kujiunga na chuo fulani maalum. Vitabu vyenye mashauri ya jinsi ya kujisaidia mwenyewe, viwe vinazungumzia mambo ya biashara, ndoa, kulea watoto, au afya ya akili, vinatofautiana. Kwa kawaida vinapendekeza njia fulani ya maisha au ya kufikiri. Kwa hiyo, ni vizuri kujiuliza: ‘Ni nani anayetoa mashauri hayo? Na chanzo cha habari hiyo ni nini?’

Huenda mara nyingi wataalamu wasitoe maoni yaliyofanyiwa utafiti wa kutosha. Baadhi yao huenda wakatoa mashauri ambayo wanajua yatawaletea pesa nyingi kwa kuwaambia watu mambo ambayo wanapenda kusikia. Katika nchi moja tu, dola bilioni nane zinachumwa kila mwaka kutokana na biashara ya video na vitabu vyenye mashauri ya jinsi ya kujisaidia mwenyewe!

Je, Miongozo Hiyo Inafaa?

Unapoamua kutafuta msaada katika miongozo kuhusu jinsi ya kujisaidia mwenyewe, unatazamia kupata mashauri yanayofaa. Hata hivyo, wakati mwingine, unapata mashauri ya kijuujuu tu au yasiyoweza kukusaidia. Kwa kawaida miongozo hiyo inasema: ‘Ukiwa na maoni yanayofaa, utafanikiwa. Chochote unachotaka, iwe ni pesa, afya nzuri, au mahusiano mazuri, utakipata ikiwa una maoni yanayofaa.’ Je, mashauri hayo yanafaa? Je, yatakusaidia kukabiliana na hali halisi ya maisha?

Fikiria kwa mfano vitabu vinavyozungumzia mahusiano na ndoa, ambavyo vinapendwa sana. Je, vinawasaidia watu kuwa na familia zenye furaha na zilizo thabiti? Si wakati wote. Mkaguzi mmoja anasema kwamba, mwandishi wa vitabu fulani vyenye mashauri ya jinsi ya kujisaidia mwenyewe, vinavyongumzia mapenzi na ambavyo vilinunuliwa sana Amerika ya Latini, “vinawaeleza wasomaji jinsi ya kuwa na mahusiano mazuri na kujiheshimu.” Mwandishi anadai kwamba kuendeleza uhusiano wenye matatizo ni kujidanganya. Kitabu hicho kinakazia jambo moja hasa, yaani, kufanya kile ambacho mtu anafurahia badala ya kutambua matatizo yake na kujaribu kuyatatua.

Ni kweli kwamba miongozo hiyo inaweza kutoa mashauri mazuri. Hata hivyo, inaweza pia kutoa mashauri mabaya. Mtaalamu anaweza kutoa madokezo yanayofaa kuhusu jambo fulani, lakini katika kisa kingine mtaalamu huyohuyo atoe mashauri yanayoweza kuharibu mambo hata zaidi. Ni vigumu sana kupata mashauri yanayofaa kati ya mashauri mengi yanayotolewa na miongozo hiyo, na ambayo mara nyingi yanapingana. Unaweza kutegemea mashauri ya nani? Jiulize: ‘Je, mashauri hayo yamefanyiwa utafiti kwa makini, au ni maoni tu ya mwandikaji? Kutafuta mali au umashuhuri kumeathiri unyoofu wa mwandikaji huyo kwa kadiri gani?’

Mwongozo ambao umewanufaisha watu kwa miaka mingi ni Biblia. Inatoa mashauri yanayofaa kuhusu mambo mengi, hata yale yanayozungumziwa katika miongozo kuhusu jinsi ya kujisaidia mwenyewe. Imewachochea wengi kutii shauri hili: ‘Fanyweni upya katika nguvu zinazoendesha akili yenu. Vaeni utu mpya.’ (Waefeso 4:23, 24) Biblia inatueleza chanzo cha matatizo yetu na inatufundisha jinsi ya kuyatatua. Isitoshe, inatoa sababu zinazotuchochea kutenda yaliyo sawa. Makala inayofuata itazungumzia mambo hayo.