Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Walilipenda Neno la Mungu

Walilipenda Neno la Mungu

Walilipenda Neno la Mungu

KWA kawaida ujumbe muhimu unatafsiriwa katika lugha nyingi ili kuhakikisha kwamba watu wengi iwezekanavyo wanauelewa. Biblia, ambayo ni Neno la Mungu ina ujumbe muhimu. Ingawa iliandikwa zamani sana, mambo yaliyo katika Biblia “yaliandikwa ili kutufundisha” na kutupa faraja na tumaini kwa ajili ya wakati ujao.—Waroma 15:4.

Hivyo basi, ni jambo linalopatana na akili kwamba Biblia ambayo ina ujumbe muhimu sana kuwahi kuandikwa, itafsiriwe katika lugha nyingi. Kwa miaka mingi, watu walijitahidi sana kuitafsiri Biblia licha ya kuwa wagonjwa sana, kazi yao kupigwa marufuku na serikali, au hata kutishwa kwamba watauawa. Kwa nini walijitahidi hivyo? Kwa sababu walilipenda Neno la Mungu. Masimulizi yanayofuata yanaonyesha kwa ufupi tu historia isiyo na kifani ya kutafsiriwa kwa Biblia.

Waingereza Watajifunza Sheria ya Kristo Vyema Katika Kiingereza”

John Wycliffe alipozaliwa mwaka wa 1330 hivi, kanisa huko Uingereza lilikuwa likiendesha ibada kwa Kilatini. Hata hivyo, watu walitumia Kiingereza katika shughuli zao za kila siku. Walizungumza na jirani zao kwa Kiingereza, hata walisali kwa Mungu katika Kiingereza.

Wycliffe, aliyekuwa kasisi Mkatoliki, alizungumza Kilatini kwa ufasaha. Hata hivyo, aliona kwamba haifai kutumia Kilatini kuwafundisha watu Biblia, kwa sababu kwa maoni yake, hiyo ilikuwa lugha ya wasomi. Aliandika hivi: “Watu wanapaswa kufundishwa sheria ya Mungu katika lugha wanayoweza kuelewa kwa urahisi zaidi, kwa sababu wanafundishwa neno la Mungu.” Kwa hiyo, Wycliffe na wenzake wakafanyiza kikundi cha kutafsiri Biblia katika Kiingereza. Iliwachukua miaka 20 kuitafsiri.

Kanisa Katoliki lilipinga kutafsiriwa kwa Biblia. Kitabu fulani (The Mysteries of the Vatican) kinaeleza hivi kuhusu kilichofanya kanisa lipinge jambo hilo: “Kutafsiriwa kwa Biblia kuliwasaidia watu wa kawaida kujua jinsi maisha na mafundisho rahisi ya Wakristo wa karne ya kwanza yalivyokuwa tofauti na mafundisho na maisha ya Wakatoliki wa wakati huo . . . Ilikuwa wazi kabisa kwamba mafundisho ya Mwanzilishi wa Ukristo yalikuwa tofauti sana na ya [papa], anayejidai kuwa wa pili kwa ukubwa baada ya Kristo.”

Papa Gregory wa 11 alitoa maagizo matano ya kumshutumu Wycliffe. Lakini mtafsiri huyo hakuacha kazi yake. Alisema: “Waingereza watajifunza sheria ya Kristo vyema katika Kiingereza. Musa na pia mitume wa Kristo waliisikia sheria ya Mungu katika lugha zao wenyewe.” Mwaka wa 1382 hivi, muda mfupi kabla ya Wycliffe kufa, tafsiri ya kwanza ya Biblia nzima katika Kiingereza ilitolewa na kikundi cha Wycliffe. Miaka kumi hivi baadaye, mmoja wa watafsiri waliofanya kazi naye akatoa tafsiri iliyosahihishwa na iliyo rahisi kusoma.

Kwa kuwa mashini za kuchapishia hazikuwapo, kila hati ilihitaji kunakiliwa kwa makini, kazi ambayo ingechukua miezi kumi! Lakini kanisa liliogopa sana kusambazwa kwa Biblia hivi kwamba askofu mkuu alitishia kumtenga na kanisa mtu yeyote aliyeisoma. Miaka 40 baada ya Wycliffe kufa, makasisi waliufukua mwili wake kwa agizo la baraza la papa, wakaiteketeza mifupa yake, na kuyatupa majivu katika mto Swift. Hata hivyo, bado watu wanyoofu waliotaka kujua kweli waliitafuta Biblia ya Wycliffe. Profesa William M. Blackburn alisema: “Nakala nyingi za Biblia ya Wyclif, zilinakiliwa na zikasambazwa sana kwa vizazi mbalimbali.”

Biblia kwa Ajili ya Watu wa Kawaida

Baada ya miaka 200 hivi, watu walikuwa wameacha kutumia Kiingereza kilichotumiwa na Wycliffe. Mhubiri mmoja kijana aliyeishi karibu na Bristol alitamauka sana kwa sababu ni watu wachache tu walioweza kuielewa Biblia. Pindi moja, mhubiri huyo, William Tyndale, alimsikia mtu fulani mwenye elimu akisema kwamba ni afadhali kukosa sheria ya Mungu kuliko kukosa sheria ya papa. Tyndale alijibu kwa kusema kwamba ikiwa Mungu atamruhusu, kwa muda mfupi atahakikisha kwamba watu wa kawaida wamepata ujuzi mwingi wa Biblia kuliko mtu mwenye elimu.

Wycliffe alikuwa ametafsiri kutoka katika Vulgate ya Kilatini na kuyanakili Maandiko kwa mkono. Mwaka wa 1524, baada ya Tyndale kuondoka Uingereza na kwenda Ujerumani, alianza kutafsiri moja kwa moja kutoka katika lugha ya Kiebrania na Kigiriki cha awali, kisha akachapisha nakala kadhaa kwa kutumia mashini ya kuchapishia iliyokuwa jijini Cologne. Punde si punde, adui za Tyndale wakajua kuhusu tafsiri hiyo na kulishawishi Baraza la Cologne liagize nakala zote za tafsiri hiyo zitwaliwe.

Tyndale alikimbilia jiji la Worms, Ujerumani, na kuendelea na kazi yake. Muda mfupi baadaye, nakala za Maandiko ya Kigiriki ambayo Tyndale aliyatafsiri katika Kiingereza, zilipelekwa Uingereza kisiri. Katika kipindi cha miezi sita, nakala nyingi zilikuwa zimeuzwa hivi kwamba maaskofu wakafanya mkutano wa dharura na kuagiza Biblia ziteketezwe.

Ili kuwazuia watu wengi wasisome Biblia na pia kuzuia kuenea kwa ule ulioitwa uzushi wa Tyndale, askofu wa London alimwagiza Sir Thomas More aandike ujumbe wa kumshambulia Tyndale. More alikasirika hasa kwa sababu Tyndale alitumia neno “kutaniko” badala ya “kanisa,” na “mzee” badala ya “kasisi.” Maneno hayo yalitilia shaka mamlaka ya papa na tofauti kati ya viongozi wa dini na watu wa kawaida. Thomas More pia alishutumu Tyndale kwa kulitafsiri neno la Kigiriki a·gaʹpe kuwa “upendo” badala ya “misaada.” Kitabu fulani (If God Spare My Life) kinasema: “Tafsiri hiyo ilihatarisha Kanisa, kwa kuwa neno hilo lilionekana kupunguza umuhimu wa kutoa misaada, jambo ambalo lingewazuia watu wasitoe michango, malipo ya kupata msamaha, na kuacha urithi. Iliaminika kwamba kufanya mambo hayo kungewasaidia waumini kujitayarishia njia ya kwenda mbinguni.”

Thomas More aliunga mkono kuteketezwa kwa “wazushi,” jambo lililofanya Tyndale anyongwe na mwili wake kuteketezwa mtini mnamo Oktoba (Mwezi wa 10) 1536. Baadaye, naye Thomas More alikatwa kichwa baada ya kukosana na mfalme. Hata hivyo, mwaka wa 1935 Kanisa Katoliki lilimtangaza kuwa mtakatifu, kisha mwaka wa 2000 Papa John Paul wa Pili akamtawaza More kuwa mtakatifu wa kuwalinda wanasiasa.

Kanisa Katoliki halikuthamini kazi ya Tyndale. Hata hivyo, kabla ya Tyndale kufa, rafiki yake, Miles Coverdale, aliunganisha visehemu vya tafsiri ya Tyndale na kufanyiza Biblia nzima, iliyokuwa tafsiri ya kwanza ya Kiingereza ambayo ilitafsiriwa kutoka katika lugha za awali! Sasa watu wa kawaida wangeweza kulisoma Neno la Mungu. Namna gani Biblia katika lugha nyinginezo?

“Ilionekana Kana Kwamba Haiwezekani”

Licha ya upinzani wa familia na marafiki, mmishonari Mwingereza Robert Morrison, aliazimia kabisa kuchapisha Biblia nzima katika Kichina, hivyo akafunga safari kwenda China mwaka wa 1807. Kazi yake ya kutafsiri haikuwa rahisi. Charles Grant, aliyekuwa mkurugenzi wa Kampuni ya East India alisema: “Kazi hiyo ilionekana kana kwamba haiwezekani.”

Alipofika China, Morrison alitambua kwamba Wachina hawakuruhusiwa kuwafundisha wageni lugha yao, na yeyote aliyefanya hivyo aliuawa. Kwa ajili ya usalama wake na wa wale waliokubali kumfundisha Kichina, Morrison hakutoka nje kwa muda. Ripoti fulani inasema kwamba “baada ya kujifunza kwa miaka miwili, Morrison aliweza kusoma, kuandika, na kuzungumza zaidi ya lahaja moja ya lugha ya Mandarin.” Muda si muda, maliki alitoa agizo kukataza uchapishaji wa vitabu vya Kikristo na yeyote aliyevichapisha aliuawa. Licha ya tisho hilo, Morrison alikamilisha Biblia nzima katika lugha ya Kichina mnamo Novemba (Mwezi wa 11) 25, 1819.

Kufikia mwaka wa 1836, nakala karibu 2,000, za Biblia nzima, nakala 10,000 za Maandiko ya Kigiriki, na visehemu mbalimbali 31,000 za Biblia katika Kichina zilikuwa zimechapishwa. Kwa kuwa watu hao walilipenda Neno la Mungu, walifanya kazi “iliyoonekana kana kwamba haiwezekani,” iwezekane.

Biblia Ndani ya Mto wa Kitanda

Majuma mawili baada ya kufunga ndoa mnamo Februari (Mwezi wa 2) 1812, mmishonari Mwamerika Adoniram Judson pamoja na mke wake, Ann, walisafiri kwa muda mrefu, na hatimaye wakaamua kuishi Burma mwaka wa 1813. * Bila kukawia walianza kujifunza Kiburma, ambayo ni moja kati ya lugha ngumu zaidi duniani. Baada ya kujifunza kwa miaka kadhaa, Judson aliandika: “Tunajifunza lugha inayozungumzwa na watu katika upande mwingine wa dunia, na mpangilio wa mawazo yao ni tofauti na wetu . . . Hatuna kamusi wala mtu wa kutusaidia kuelewa maana ya neno hata moja.”

Judson hakukatishwa tamaa na matatizo ya lugha. Alikamilisha tafsiri ya Maandiko ya Kikristo ya Kigiriki katika Kiburma mnamo Juni (Mwezi wa 6) 1823. Baadaye, Burma iliingia vitani. Judson alishukiwa kuwa mpelelezi, hivyo akatupwa gerezani, akafungwa pingu sita za chuma, na kufungiliwa kwenye ufito mrefu. Katika kitabu chake cha mwaka wa 1853, Francis Wayland, aliandika hivi kumhusu Judson: “Bwana Judson alipojua kwamba ameruhusiwa kukutana na mke wake na kuzungumza naye Kiingereza, alitaka kwanza kabisa kujua kuhusu hati ya Agano Jipya iliyokuwa imetafsiriwa.” Ann akihofia kuwa hati hiyo iliyokuwa imefichwa chini ya sakafu ndani ya nyumba inaweza kuharibiwa na unyevunyevu na kuvu, aliitia ndani ya mto wa kitanda na kuushona, kisha akampelekea mume wake gerezani. Licha ya hali hizo ngumu, hati hiyo haikuharibika.

Baada ya miezi mingi gerezani, Judson aliachiliwa. Lakini furaha yake ilikuwa ya muda tu. Baadaye mwaka huohuo, Ann aliugua homa kali, akafa majuma kadhaa baadaye. Miezi sita tu baada ya tukio hilo, binti yake, Maria, mwenye umri wa miaka miwili hivi akafa kwa ugonjwa usioweza kupona. Ingawa alivunjika moyo sana, Judson alirudia kazi yake. Hatimaye akaikamilisha Biblia nzima mwaka wa 1835.

Je, Unalipenda Neno la Mungu?

Kama watafsiri hao, watu wengi wamelipenda Neno la Mungu. Katika Israeli la kale, mtunga-zaburi alimwimbia Yehova hivi: “Jinsi ninavyoipenda sheria yako! Ndiyo ninayoihangaikia mchana kutwa.” (Zaburi 119:97) Mbali na kuwa kitabu chenye kuvutia, Biblia ina ujumbe muhimu. Je, unalihangaikia Neno la Mungu kwa kulisoma kwa ukawaida? Unaweza kuwa na hakika kwamba ikiwa unasoma Neno la Mungu na kutenda kupatana na mambo unayojifunza, ‘utakuwa mwenye furaha katika kulitenda.’—Yakobo 1:25.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 22 Sasa nchi ya Burma na lugha ya Kiburma zinaitwa Myanmar.

[Blabu katika ukurasa wa 8]

“Waingereza watajifunza sheria ya Kristo vyema katika Kiingereza.”—JOHN WYCLIFFE

[Picha katika ukurasa wa 9]

William Tyndale na ukurasa wa Biblia ya Tyndale

[Picha zimaeandaliwa na]

Tyndale: From the book The Evolution of the English Bible

[Picha katika ukurasa wa 10]

Robert Morrison na tafsiri yake ya Biblia ya Kichina

[Hisani]

In the custody of the Asian Division of the Library of Congress

Robert Morrison, engraved by W. Holl, from The National Portrait Gallery Volume IV, published c.1820 (litho), Chinnery, George (1774-1852) (after)/Private Collection/Ken Welsh/The Bridgeman Art Library International

[Picha katika ukurasa wa 11]

Adoniram Judson na tafsiri yake ya Biblia ya Kiburma

[Hisani]

Judson: Engraving by John C. Buttre/Dictionary of American Portraits/Dover

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 8]

Wycliffe: From the book The History of Protestantism (Vol. I); Bible: Courtesy of the American Bible Society Library, New York