Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Rahabu Alisikiliza Habari

Rahabu Alisikiliza Habari

Wafundishe Watoto Wako

Rahabu Alisikiliza Habari

TUSEME kwamba ni miaka 3,500 hivi iliyopita. Tuko katika jiji la Yeriko, katika nchi ya Kanaani. Msichana mmoja anayeitwa Rahabu anaishi katika jiji hilo. Alizaliwa baada ya Musa kuwaongoza Waisraeli kutoka katika utumwa huko Misri kupitia Bahari Nyekundu kwenye nchi kavu! Hakuna redio, televisheni, wala Intaneti, lakini Rahabu anajua kuhusu muujiza huo, hata ingawa ulitukia mbali sana na mahali anapoishi. Je, unajua jinsi alivyopata habari hizo?— *

Bila shaka, wasafiri wamekuwa wakisimulia kuhusu miujiza hiyo. Anapoendelea kukua, Rahabu anakumbuka mambo ambayo Yehova aliwafanyia watu wake. Kisha anasikia mambo mengine yenye kustaajabisha kuhusu Waisraeli. Wameingia Kanaani baada ya kukaa nyikani kwa miaka 40, na Mungu amekuwa akiwasaidia kuwashinda watu wote wanaowapinga. Sasa Rahabu anapata habari kwamba Waisraeli wamepiga kambi ng’ambo tu ya Mto Yordani karibu na Yeriko!

Jioni moja, wageni wawili wanamtembelea Rahabu kwa sababu wanajua kwamba anafanya kazi katika nyumba ya wageni. Kwa hiyo, anawakaribisha. Wakati wa usiku, mfalme wa Yeriko anapata habari kwamba wapelelezi Waisraeli wameingia Yeriko na kwamba wameenda katika nyumba ambako Rahabu anafanya kazi. Kwa hiyo, mfalme anawatuma wajumbe kwa Rahabu, na wanamwambia awatoe nje wanaume ambao wamemtembelea. Je, unajua tayari Rahabu amepata habari gani, na amefanya nini kuhusu habari hizo?—

Kabla ya wajumbe wa mfalme kufika, Rahabu alipata habari kwamba wageni waliomtembelea ni wapelelezi Waisraeli. Kwa hiyo, aliwaficha darini, na sasa anawaambia hivi wajumbe wa mfalme: “Ni kweli, wanaume hao walikuja kwangu . . . Ikawa wakati wa kufungwa kwa lango, kulipokuwa na giza, wanaume wale wakatoka.” Kisha, Rahabu anawahimiza hivi: “Wafuatilieni haraka.”

Unafikiri ni kwa nini Rahabu amewalinda wapelelezi hao?—Anaeleza sababu, anawaambia hivi: “Najua hakika ya kwamba Yehova atawapa nchi hii . . . Kwa maana tumesikia jinsi ambavyo Yehova aliyakausha maji ya Bahari Nyekundu mbele yenu wakati mlipotoka Misri.” Pia, amesikia jinsi Mungu alivyowasaidia Waisraeli kuwashinda maadui wao.

Bila shaka, Yehova alifurahi kuona Rahabu akiwalinda wapelelezi hao, kama Biblia inavyotuambia kwenye Waebrania 11:31. Pia, alifurahi Rahabu alipowasihi hivi wapelelezi hao: ‘Basi sasa, tafadhali, niapieni kwa kuwa nimewatendea ninyi fadhili, mniahidi kwamba Yeriko likitekwa mtamwokoa baba yangu na mama yangu na ndugu zangu na dada zangu.’ Wapelelezi hao wanaahidi kufanya hivyo ikiwa Rahabu atafuata maagizo yao. Je, unajua wanampa maagizo gani?—

Wapelelezi hao wanasema: ‘Chukua kamba hii ya uzi mwekundu uifunge katika dirisha lako, na uwakusanye watu wote wa familia yako ndani ya nyumba. Ukifanya hivyo, kila mtu aliye ndani ya nyumba atakuwa salama.’ Rahabu anafanya kama tu wapelelezi wanavyomwambia. Je, unajua kinachotukia sasa?—

Waisraeli wanafika nje ya kuta za Yeriko. Kwa siku sita wanazunguka jiji hilo mara moja kila siku bila kupiga kelele. Siku ya saba, wanalizunguka mara saba kisha wanapaaza sauti kubwa. Ukuta unaanguka, isipokuwa nyumba ambayo ina kamba nyekundu katika dirisha! Rahabu na familia yake wanaokolewa.—Yoshua 2:1-24; 6:1-5, 14, 15, 20-25.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo ambayo Rahabu alifanya?— Rahabu hakusikiliza tu habari kuhusu mambo ambayo Mungu alikuwa anafanya ili kuwalinda watu wake, lakini yeye pia aliwasaidia watu wa Mungu alipopata nafasi ya kufanya hivyo. Ndiyo, Rahabu alichagua kumtumikia Yehova pamoja na watu wake! Je, utafanya hivyo pia?—Tunasali ili ufanye hivyo.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 3 Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.

Maswali:

○ Ni habari gani za maana ambazo Rahabu alisikia alipokuwa mtoto?

○ Aliwatendea namna gani wapelelezi Waisraeli, na kwa nini?

○ Rahabu aliwaambia wapelelezi hao wamwahidi nini?

○ Tunajua jinsi gani kwamba Yehova alipendezwa na Rahabu, na unaweza kuwa kama yeye ukifanya nini?