Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Umaskini Ni Ishara ya Kukosa Kibali cha Mungu?

Je, Umaskini Ni Ishara ya Kukosa Kibali cha Mungu?

Je, Umaskini Ni Ishara ya Kukosa Kibali cha Mungu?

MUNGU aliwaambia Waisraeli wa kale: “Mtu yeyote asije kuwa maskini katikati yako.” Hiyo ilikuwa kwa sababu katika Sheria aliyowapa, kulikuwa na sheria za kuwatunza maskini na hata kuachilia huru deni lao. (Kumbukumbu la Torati 15:1-4, 7-10) Kwa hiyo, hakukupaswa kuwa na maskini yeyote kati ya Waisraeli, kwa kuwa Yehova aliahidi kuwabariki. Hata hivyo, ili wapate baraka hizo walipaswa kutii Sheria, lakini Waisraeli walishindwa kufanya hivyo.

Hata hivyo, hiyo haimaanishi kwamba maskini walikosa kibali cha Mungu na matajiri walibarikiwa na Mungu. Watumishi wengi waaminifu wa Mungu walikuwa maskini. Nabii Amosi alikuwa mchungaji wa kondoo na kibarua tu. (Amosi 1:1; 7:14) Katika siku za nabii Eliya, wakati ambapo kulikuwa na njaa nchini Israeli, Eliya alilazimika kumtegemea mjane maskini, ambaye kwa njia ya kimuujiza unga na mafuta yake hayakumalizika. Eliya na mjane huyo hawakuwa matajiri; Yehova aliwaandalia mahitaji yao ya lazima tu.—1 Wafalme 17:8-16.

Matukio yasiyotazamiwa yanaweza kuwatumbukiza watu katika umaskini. Aksidenti na magonjwa yanaweza kumzuia mtu kufanya kazi kwa muda au hata kabisa. Na kifo kinaweza kufanya wengine wabaki wakiwa mayatima na wajane. Hata hali mbaya kama hizo hazionyeshi kwamba mtu hana kibali cha Mungu. Simulizi la Naomi na Ruthu ni mfano wenye kugusa moyo wa jinsi Yehova anavyowatunza maskini kwa upendo. Ingawa Naomi na Ruthu waliachwa wakiwa maskini hohehahe waume wao walipokufa, Yehova Mungu aliwabariki na kufanya mipango ya kuwaandalia mahitaji yao.—Ruthu 1:1-6; 2:2-12; 4:13-17.

Kwa wazi, umaskini si ishara ya kukosa kibali cha Mungu. Wale waliokuwa waaminifu kwa Yehova Mungu wanaweza kuwa na uhakika katika maneno haya ya Mfalme Daudi: “Nilikuwa kijana, pia nimezeeka, na bado sijamwona mtu yeyote mwadilifu akiwa ameachwa kabisa, wala uzao wake ukitafuta mkate.”—Zaburi 37:25.

[Picha katika ukurasa wa 8]

Ingawa Naomi na Ruthu walikuwa maskini hohehahe, Mungu aliwabariki na kuwatunza kwa upendo