Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Sanduku la agano lilienda wapi?

Waisraeli walihusianisha kuwapo kwa Mungu na sanduku la agano. (Kutoka 25:22) Hilo lilikuwa sanduku takatifu la mbao lililofunikwa kwa dhahabu ambalo Musa aliweka mabamba mawili ya mawe ya Sheria. Waisraeli walipoishi jangwani, Sanduku hilo liliwekwa katika Patakatifu Zaidi pa hema la mkutano. (Kutoka 26:33) Hatimaye, Sanduku hilo liliwekwa katika Patakatifu Zaidi katika hekalu la Sulemani.—1 Wafalme 6:19.

Sanduku hilo linatajwa kwa mara ya mwisho kwenye 2 Mambo ya Nyakati 35:3 wakati Mfalme Yosia alipolirudisha kwenye hekalu mnamo 642 K.W.K. Huenda Sanduku hilo liliondolewa hekaluni na Manase, mfalme mwasi-imani aliyetawala kabla ya Yosia ambaye aliingiza sanamu ndani ya hekalu. Au labda Sanduku hilo lilihamishwa na kuwekwa mahali salama wakati Yosia alipokuwa akikarabati hekalu. (2 Mambo ya Nyakati 33:1, 2, 7; 34:1, 8-11) Baada ya hapo Biblia haisemi Sanduku hilo lilienda wapi, kwa sababu halitajwi katika orodha ya vitu vilivyochukuliwa kutoka hekaluni Wababiloni walipoteka Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K.—2 Wafalme 25:13-17.

Maandiko hayasemi kwamba Sanduku hilo lilirudishwa Patakatifu Zaidi katika hekalu lililojengwa upya na Zerubabeli, wala hayaonyeshi ikiwa sanduku lingine lilitengenezwa.—Ezra 1:7-11.

Wanaume wanaoitwa Yakobo katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo walikuwa akina nani?

Kulikuwa na wanaume kadhaa, na ni rahisi sana kuwachanganya. Maneno “Abrahamu, Isaka, na Yakobo” yanaonekana mara nyingi katika Biblia, na Mathayo 1:16 inasema Yakobo “akamzaa Yosefu mume wa Maria.” Mmoja wao alikuwa baba ya mtume Yuda (siyo Yuda Iskariote), na hakuna habari zaidi kumhusu.—Luka 6:16; Matendo 1:13.

Kisha kuna mwana wa Zebedayo. Yakobo huyo alikuwa ndugu ya Yohana, na wote wawili walikuwa mitume wa Yesu. (Mathayo 10:2) Inaonekana kwamba Salome, alikuwa mama yake, dada ya mama ya Yesu. (Linganisha Mathayo 27:55, 56 na Marko 15:40, 41 na Yohana 19:25.) Ikiwa ndivyo, huyu Yakobo alikuwa binamu ya Yesu. Alikuwa mvuvi, na akiwa pamoja na ndugu yake walifanya kazi pamoja na Petro na Andrea.—Marko 1:16-19; Luka 5:7-10.

Kisha kuna Yakobo mwana wa Alfayo, ambaye pia alikuwa mtume wa Yesu. (Marko 3:16-18) Anatajwa kuwa “Yakobo Mdogo” kwenye Marko 15:40. Huenda aliitwa “Mdogo” kwa sababu alikuwa na mwili mdogo au alikuwa na umri mdogo kuliko Yakobo, mwana wa Zebedayo.

Mwishowe kuna Yakobo mwana wa Yosefu na Maria, na ndugu wa kambo wa Yesu. (Marko 6:3; Wagalatia 1:19) Wakati wa huduma ya Yesu, Yakobo hakuwa mmoja wa wanafunzi wake. (Mathayo 12:46-50; Yohana 7:5) Hata hivyo, kabla ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., Yakobo alisali akiwa na mama yake, ndugu zake, pamoja na mitume katika chumba cha juu kule Yerusalemu. (Matendo 1:13, 14) Hatimaye Yakobo alikuja kuwa na madaraka katika kutaniko la Yerusalemu na akaandika kitabu cha Biblia kinachoitwa kwa jina lake.—Matendo 12:17; Yakobo 1:1.