Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuwa Mmishonari Mwenye Mafanikio

Jinsi ya Kuwa Mmishonari Mwenye Mafanikio

Kuhitimu kwa Darasa la 126 la Gileadi

Jinsi ya Kuwa Mmishonari Mwenye Mafanikio

UMATI wenye msisimuko ulikusanyika katika Kituo cha Elimu cha Watchtower huko Patterson, New York, kwa ajili ya tukio la pekee. Jumamosi (Siku ya Posho), Machi 14, 2009 (14/3/2009) ilikuwa siku ya kuhitimu kwa darasa la 126 la Shule ya Gileadi (Watchtower Bible School of Gilead). Wahitimu walikuwa karibu kutumwa nchi 22 ili kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu.—Mathayo 24:14.

Wanafunzi hao walikuwa wametoka tu kumaliza masomo mengi ya Biblia ya miezi mitano ambayo yangewasaidia kuwa wamishonari Wakristo wenye mafanikio. Siku ya kuhitimu iliwapa nafasi ya mwisho ya kusikiliza mashauri yenye hekima kuhusu jinsi ya kufanikiwa wakiwa wamishonari.

Shule ya Gileadi ilianza kuwazoeza wamishonari mwaka wa 1943, akasema Anthony Morris, mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, ambaye alikuwa mwenyekiti wa programu hiyo. Tangu wakati huo, wahitimu wamechangia pakubwa katika kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote na wamepata matokeo mazuri.

Ingawa waandishi na Mafarisayo waliwadharau na kuwaona mitume wa Yesu kuwa “wasio na elimu na wa kawaida tu” msemaji alisema kwamba wapinzani hao walilazimika kutambua kwamba mitume hao walikuwa wajasiri kwa sababu walikuwa wameshirikiana na Yesu. (Matendo 4:13) Mafundisho ambayo wahitimu hupata yanawasaidia kusema kwa ujasiri.

‘Usiangalie Nyuso’ ndicho kilichokuwa kichwa cha hotuba ya Robert Ciranko, msaidizi wa Halmashauri ya Uandikaji ya Baraza Linaloongoza. Alisema kwamba punde si punde wanafunzi hao watakutana na watu wa tamaduni na desturi tofauti sana. Hata hivyo, itakuwa rahisi kuwahubiria watu hao ikiwa wanafunzi wataiga mtazamo wa Yehova. Kulingana na tafsiri ya moja kwa moja ya Matendo 10:34, “Mungu haangalii nyuso,” yaani, hapendelei watu fulani. “Mungu hana ubaguzi.” (Matendo 10:35) “Kwa kuiga mtazamo wa Yehova na kumwona kila mtu katika eneo kuwa anaweza kukubaliwa na Mungu, mtafanikiwa mkiwa wamishonari,” akasema Ndugu Ciranko.

“Mna Kila Kitu Mnachohitaji”

“Watu fulani humwona ngamia kuwa ana sura mbaya,” hivyo ndivyo Samuel Herd, mshiriki wa Baraza Linaloongoza alivyoanza hotuba yake, “hata hivyo, ameumbwa afaane kabisa na maisha ya jangwani.” Vivyo hivyo, wamishonari hao wapya wana kila kitu wanachohitaji ili wafanikiwe katika maeneo yao. Mambo matano yatawasaidia.

1. Kumpenda Yehova. (Mathayo 22:37, 38) Tayari wanafunzi hao wameonyesha kwamba wameazimia kumtumikia Yehova.

2. Ujuzi wa Neno la Mungu. Ngamia huhifadhi chakula katika mafuta yaliyo kwenye nundu yake. Hata hivyo, hataacha kula na kuanza kutegemea hifadhi hiyo ya wakati wa dharura. Vivyo hivyo wamishonari hawapaswi kutegemea tu habari waliyojifunza katika Shule ya Gileadi lakini wanapaswa kuendelea kujilisha kiroho.

3. Kuwapenda watu. (Mathayo 22:39) Wanafunzi wanawaonyesha watu huruma.

4. Roho ya kujitolea. (Zaburi 110:3) Mmishonari anapoishiwa nguvu, Yehova anamjaza nguvu kamili.—Isaya 40:29.

5. Nguvu za ujana. Kama vile tu ngamia humbeba mwendeshaji wake jangwani, huenda mmishonari akahitajika ‘kumbeba’ Mkristo mwenzake aliye na matatizo ya kiroho. Mtu anahitaji kuwa na nguvu nyingi ili kufanya hivyo, lakini wamishonari wana nguvu za ujana.

Sehemu Nyingine za Programu

Lozi zilikuwa kati ya mazao bora ambayo Yakobo alimpa mtawala wa Misri kama zawadi, akasema Michael Burnett, mwalimu wa Shule ya Gileadi. (Mwanzo 43:11) Lozi zimejaa lishe nyingi. Wanafunzi wametafuna lozi nyingi za kiroho wakati wa masomo yao. Kati ya mambo muhimu ambayo wamishonari wanapaswa kukumbuka ni kuridhika na maandalizi ya Yehova na kujifunza kupenda mazingira yao mapya.

Mark Noumair, mwalimu mwingine wa Shule ya Gileadi, alieleza kwamba Neno la Mungu ni kama “mfuko uliojaa hekima.” (Ayubu 28:18) Tunahitaji kuufungua na kutumia yaliyomo. Ikiwa utumishi wa mmishonari hautakuwa kama alivyotarajia, huenda akamfikiria mtume Paulo. Wanafunzi wa Yesu walimtuma Paulo kwenye mji aliozaliwa, naye alikaa huko kwa miaka tisa. Badala ya kufikiria kwamba akiwa “chombo kilichochaguliwa” alipaswa kutumika mahali pengine, Paulo alifanya kazi kwa bidii mahali popote alipokuwa. (Matendo 9:15, 28-30) Huenda isiwe rahisi kukubali uchaguzi wa Yehova. Mtumishi mwingine aliyekubali uchaguzi wa Yehova ni Yonathani. Akitambua kwamba Daudi ndiye aliyechaguliwa na Yehova kuwa mfalme, Yonathani aliridhika.

Katika sehemu yenye kichwa “Watumishi wa Mungu Husema kwa Ujasiri,” wanafunzi waliigiza mambo yaliyoonwa katika utumishi wa shambani walipokuwa wakihudhuria shule. Wengi wao walianzisha mafunzo ya Biblia. Katika sehemu iliyofuata yenye kichwa, “Wametayarishwa na Tengenezo la Yehova,” wamishonari watatu waliotumikia kwa muda mrefu walihojiwa. Kila mmoja wao alieleza jinsi alivyozoezwa kushirikiana na tengenezo la Mungu.

“Uwe Mmishonari Mwenye Furaha”

Gerrit Lösch, mshiriki mwingine wa Baraza Linaloongoza alitoa hotuba ya msingi yenye kichwa, “Uwe Mmishonari Mwenye Furaha.” Utendaji mwingi ambao watu huona kuwa wenye “kufurahisha” hauleti furaha hata kidogo, akasema. (Methali 14:13; Mhubiri 2:10, 11) Furaha ya kweli hutokana na kufanya mapenzi ya Mungu, ingawa si rahisi kufanya hivyo siku zote. Masomo ya Gileadi hayakuwa rahisi lakini yalileta uradhi mwingi.

Kuna mambo kadhaa yanayowafanya Wakristo wa kweli wawe na furaha. Wanamwabudu Mungu mwenye furaha. (Zaburi 33:12; 1 Timotheo 1:11) Wanaishi katika paradiso ya kiroho, na Biblia inaahidi kwamba hivi karibuni dunia itakuwa paradiso halisi. Wamejua kusudi la uhai—kumtumikia Yehova na kumsifu. Isitoshe, wanapendwa na Yehova na Yesu.

Msemaji aliendelea kusema hivi, “Utakuwa mmishonari mwenye furaha ukijifunza kuridhika.” Kuwapenda wengine na kupendwa nao ni jambo lingine linalochangia furaha. Kwa hiyo, funika makosa ya wengine badala ya kuyakazia. Watendee wengine mema, wasaidie wanyonge, na uwaambie mambo mazuri uliyoona. (Zaburi 41:1, 2; Matendo 20:35) Furaha inatokana na kujitahidi katika kazi ya kuhubiri.—Luka 11:28.

“Nendeni mkiwa wamishonari wenye furaha,” akamalizia Ndugu Lösch, “mkijifurahisha kwa kiasi na kukazia fikira kumsifu Yehova, Mungu wetu mwenye furaha na kuwafanya wengine wengi wawe na furaha.”

Baada ya kusoma salamu kutoka nchi mbalimbali, Anthony Morris aliwapa wanafunzi diploma zao. Baada ya hayo, mwakilishi wa darasa la 126 alisoma barua iliyoandikwa kwa Baraza Linaloongoza. Katika barua hiyo wanafunzi walishukuru kwa kuhudhuria Shule ya Gileadi.

Kwa kumalizia, mwenyekiti alisema kwamba “viungo na kano” vinavyounganisha mwili vinafananishwa na njia ambayo “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” anatumia kuwapa watu wa Yehova chakula na mwelekezo. (Wakolosai 2:18, 19; Mathayo 24:45) Ikiwa wahitimu wa Gileadi watashirikiana kikamili na watu ambao Mungu amewaweka rasmi, watafanikiwa kutimiza kwa ukamili huduma yao.—2 Timotheo 4:5.

[Sanduku katika ukurasa wa 30]

TAKWIMU ZA DARASA

Idadi ya nchi ambazo zimewakilishwa: 6

Idadi ya nchi ambako wametumwa: 22

Idadi ya wanafunzi: 56

Idadi ya wenzi wa ndoa: 28

Wastani wa umri: 32.8

Wastani wa miaka katika kweli: 17.9

Wastani wa miaka katika huduma ya wakati wote: 13.5

NCHI AMBAZO WANAFUNZI WALITUMWA

Wahitimu walitumwa Afrika Kusini, Benin, Bolivia, Bulgaria, Burkina Faso, Ghana, Guatemala, Honduras, Kamerun, Kenya, Kosta Rika, Liberia, Madagaska, Msumbiji, Nikaragua, Panama, Paraguai, Peru, Rumania, Sierra Leone, Togo, na Uganda.

[Picha katika ukurasa wa 31]

Darasa la 126 Lililohitimu la Shule ya Gileadi

Nambari za safu zinaanzia mbele kwenda nyuma, na majina yameorodheshwa kuanzia kushoto kwenda kulia katika kila safu.

(1) Kirchhoff, K.; Nichols, C.; Guzmán, Y.; Coil, H.; Becker, O.; De Simone, A. (2) Manzanares, A.; Bouvier, E.; Peddle, J.; Mason, H.; Braz, J. (3) Lee, J.; Forte, A.; Boucher, T.; Marsh, A.; Leighton, S.; Glover, M. (4) Kambach, H.; Jones, T.; Ferreira, A.; Morales, J.; Chicas, S.; Davis, B.; Dormanen, E. (5) Dormanen, B.; Nichols, J.; Pacho, T.; Titmas, L.; Bouvier, E.; Kirchhoff, A. (6) Leighton, G.; Pacho, A.; Van Campen, B.; Manzanares, A.; Rivard, A.; Lee, Y.; Titmas, L. (7) Boucher, M.; Coil, K.; Marsh, C.; Guzmán, J.; Jones, W.; Kambach, J. (8) Glover, A.; Ferreira, G.; Mason, E.; Forte, D.; Davis, N.; Chicas, O.; Rivard, Y. (9) Braz, D.; Van Campen, D.; Morales, A.; De Simone, M.; Becker, M.; Peddle, D.