Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Roho Takatifu Ni Nini?

Roho Takatifu Ni Nini?

Roho Takatifu Ni Nini?

PINDI moja Yesu aliwauliza wanafunzi wake hivi: “Ni baba gani kati yenu ambaye, ikiwa mwana wake anaomba samaki, labda atampa nyoka badala ya samaki? Au ikiwa pia anaomba yai, atampa nge?” (Luka 11:11, 12) Watoto walioishi Galilaya walifurahia kula mayai na samaki; walijua walichotaka.

Yesu alisema tunapaswa kuendelea kuomba roho takatifu kama vile tu mtoto mwenye njaa anavyoomba chakula. (Luka 11:9, 13) Kujua roho takatifu ni nini kunaweza kutusaidia kuelewa kwa nini ni muhimu tuwe nayo. Acheni kwanza tuchunguze Biblia inafundisha nini kuhusu roho takatifu.

“Nguvu za Aliye Juu Zaidi”

Maandiko yanaonyesha wazi kwamba roho takatifu ni nguvu ambazo Mungu anatumia kutimiza mapenzi yake. Malaika Gabrieli alipomwambia Maria kwamba angepata mtoto hata ingawa Maria alikuwa bikira, malaika huyo alimwambia hivi: “Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu za Aliye Juu Zaidi zitakufunika. Kwa sababu hiyo pia kile kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.” (Luka 1:35) Kulingana na maneno ya Gabrieli, kuna uhusiano kati ya roho takatifu na “nguvu za Aliye Juu Zaidi.”

Wazo kama hilo linapatikana katika Maandiko mengine. Nabii Mika alisema: “Nami nimejaa nguvu, kwa roho ya Yehova.” (Mika 3:8) Yesu aliwaahidi wanafunzi wake: “Mtapokea nguvu wakati roho takatifu itakapofika juu yenu.” (Matendo 1:8) Na mtume Paulo alizungumza kuhusu “nguvu za roho takatifu.”—Waroma 15:13, 19.

Hivyo, tunaweza kukata kauli gani? Kuna uhusiano wa karibu kati ya roho takatifu na nguvu za Mungu. Roho takatifu ndio njia ambayo Yehova anatumia nguvu zake. Kwa maneno rahisi, roho takatifu ni nguvu za utendaji za Mungu. Na hizo ni nguvu zenye kustaajabisha kama nini! Hatuwezi hata kuwazia nguvu zilizohitajika kuumba ulimwengu mzima. Kupitia nabii Isaya, Yehova anatuambia tutafakari maneno yafuatayo: “Inueni macho yenu juu, mwone. Ni nani ameviumba vitu hivi? Ni Yeye anayelileta jeshi lake kulingana na hesabu, ambaye zote anaziita kwa jina. Kutokana na wingi wa nguvu zenye msukumo, yeye pia akiwa hodari katika nguvu, hakuna hata moja kati ya hizo inayokosekana.”—Isaya 40:26.

Kwa hiyo, Biblia inaonyesha kwamba utaratibu na upatano uliopo katika ulimwengu unatokana na “nguvu zenye msukumo,” au nguvu za Mungu Mweza-Yote. Ni wazi kwamba nguvu za utendaji za Mungu ni nyingi sana, na tunazihitaji ili kuendelea kuishi.—Ona sanduku “Utendaji wa Roho Takatifu.”

Yehova anaweza kutumia roho yake takatifu kwa kiwango kikubwa, kama vile alivyoitumia kuumba ulimwengu. Lakini anaweza pia kuitumia kwa niaba ya wanadamu. Biblia ina mifano mingi inayoonyesha jinsi ambavyo watumishi wake hapa duniani walivyojazwa nguvu na roho takatifu.

“Roho ya Yehova Iko Juu Yangu”

Huduma ya Yesu inatuonyesha kwa njia yenye kupendeza jinsi ambavyo roho takatifu ya Mungu inaweza kuwapa nguvu watumishi wake. “Roho ya Yehova iko juu yangu,” Yesu akawaambia watu wa Nazareti. (Luka 4:18) Yesu alitimiza nini kwa “nguvu za roho”? (Luka 4:14) Aliponya kila namna ya magonjwa, akatuliza mawimbi ya bahari iliyochafuka, akalisha maelfu ya watu kwa kutumia mikate na samaki wachache, na hata akafufua wafu. Mtume Petro alimfafanua Yesu kuwa “mwanamume aliyeonyeshwa hadharani na Mungu . . . kupitia kazi zenye nguvu na mambo ya ajabu na ishara ambazo Mungu alifanya kupitia kwake.”—Matendo 2:22.

Wakati wetu roho takatifu haiwawezeshi watu kufanya miujiza kama hiyo. Hata hivyo, inaweza kufanya mambo yenye kustaajabisha kwa niaba yetu. Yehova huwapa waabudu wake roho yake takatifu, kama Yesu alivyowahakikishia wanafunzi wake. (Luka 11:13) Kwa sababu hiyo, mtume Paulo angeweza kusema hivi: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” (Wafilipi 4:13) Je, roho takatifu inaweza kufanya hivyo maishani mwako? Habari inayofuata itazungumzia jambo hilo.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 5]

Roho Takatifu Si Mtu

Biblia inalinganisha roho takatifu na maji. Alipokuwa akiwaahidi watu wake baraka za wakati ujao, Mungu alisema: “Nitamimina maji juu ya mwenye kiu, na vijito vinavyotiririka juu ya mahali pakavu. Nitaimimina roho yangu juu ya uzao wako, na baraka yangu juu ya wazao wako.”—Isaya 44:3.

Mungu anapomimina roho yake juu ya watumishi wake, ‘wanajaa roho takatifu,’ au ‘wanajazwa roho takatifu.’ Yesu, Yohana Mbatizaji, Petro, Paulo, Barnaba, na wanafunzi waliokuwa wamekusanyika pamoja siku ya Pentekoste 33 W.K., wote wanasemwa kuwa walijaa au, walijazwa roho takatifu.—Luka 1:15; 4:1; Matendo 4:8; 9:17; 11:22, 24; 13:9.

Fikiria hili: Je, mtu anaweza ‘kumiminwa’ juu ya watu wengi? Unaweza kusema kwamba mtu mmoja ‘alijaza’ kikundi kizima cha watu? Hilo halipatani na akili. Biblia inataja watu wakijazwa hekima, uelewaji, au hata ujuzi sahihi, lakini haijawahi kusema kwamba mtu amejazwa na mtu mwingine.—Kutoka 28:3; 1 Wafalme 7:14; Luka 2:40; Wakolosai 1:9.

Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “roho” ni pneuʹma, ambalo linaleta wazo la nguvu isiyoonekana. Kulingana na kamusi ya Vine’s Expository Dictionary of New Testament Words, neno pneuʹma “kimsingi huwakilisha upepo . . . pia pumzi; kisha, hasa roho, ambayo, kama tu upepo, haionekani, si kitu halisi, na ina nguvu.”

Basi ni wazi kwamba roho takatifu si mtu. *

[Maelezo ya chini]

^ fu. 19 Kwa habari zaidi, ona sehemu yenye kichwa, “Ukweli Kuhusu Baba, Mwana, na Roho Takatifu,” ukurasa wa 201-204, katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Hisani]

Photodisc/SuperStock