Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anataka Nini Kutoka Kwetu?

Yehova Anataka Nini Kutoka Kwetu?

Mkaribie Mungu

Yehova Anataka Nini Kutoka Kwetu?

Kumbukumbu la Torati 10:12, 13

JE, NITII au nisitii? Si rahisi sikuzote kufanya uamuzi huo. Mtu anapokuwa mkali au mwenye kudai mengi kupita kiasi huenda watu walio chini yake wakatii kwa kulazimishwa. Hata hivyo, Yehova Mungu hupewa utii wa hiari na waabudu wake. Kwa nini? Ili kujibu swali hilo acheni tuchunguze maneno ya Musa yanayopatikana kwenye Kumbukumbu la Torati 10:12, 13. *

Akijumlisha matakwa ya Mungu, Musa aliuliza swali hili lenye kuamsha fikira: “Yehova Mungu wako anataka nini kutoka kwako?” (Mstari wa 12) Mungu ana haki ya kudai chochote anachotaka kutoka kwetu. Kwa kweli, yeye ndiye Bwana Mwenye Enzi Kuu na ndiye Chanzo na Mtegemezaji wa uhai. (Zaburi 36:9; Isaya 33:22) Hiyo ni sababu yenye nguvu ya kudai utii kutoka kwetu. Hata hivyo, hataki tumtii kwa kulazimishwa. Anataka nini kutoka kwetu? Kwamba ‘tutii kutoka moyoni.’—Waroma 6:17.

Ni nini kinachoweza kutuchochea tumtii Mungu kwa hiari? Musa anataja sababu moja: “Kumwogopa Yehova Mungu wako.” * (Mstari wa 12) Huo si woga wa kupata matokeo mabaya bali ni woga unaotokana na kumheshimu Mungu na njia zake. Ikiwa tunamwogopa Mungu kwa njia inayofaa, tutaepuka kumkasirisha.

Lakini nia yetu kuu ya kumtii Mungu inapaswa kuwa nini? Musa alisema hivi: “Kumpenda [Yehova] na kumtumikia Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote.” (Mstari wa 12) Kumpenda Mungu kunahusisha mengi kuliko hisia. Kitabu kimoja kinaeleza: “Vitenzi vya Kiebrania vinavyorejelea hisia nyakati nyingine hurejelea matokeo ya hisia hizo.” Kitabu hichohicho kinasema kwamba kumpenda Mungu kunamaanisha “kutenda kwa upendo” kumwelekea Mungu. Kwa maneno mengine, ikiwa kwa kweli tunampenda Mungu, tutatenda kwa njia ambazo tunajua zitamfurahisha.—Methali 27:11.

Tumtii Mungu kadiri gani? Musa anasema: ‘Tembea katika njia zote za Mungu.’ (Mstari wa 12) Yehova anataka tufanye yote anayotuomba tufanye. Je, utii kamili kama huo unaweza kutuletea madhara? Hilo haliwezekani.

Kutii kwa hiari kutatuletea baraka. Musa aliandika hivi: “Kuzishika amri . . . ninazokuamuru wewe leo, [ni] kwa faida yako.” (Mstari wa 13) Naam, kila amri ya Yehova, kila kitu anachotaka tufanye, ni kwa faida yetu. Mbona isiwe hivyo? “Mungu ni upendo,” inasema Biblia. (1 Yohana 4:8) Kwa hiyo, ametupa amri ambazo zitatuletea faida za kudumu. (Isaya 48:17) Kufanya yale ambayo Yehova anataka kutoka kwetu kutatuzuia tusikatishwe tamaa sasa na kutatuletea baraka za milele chini ya Ufalme wake. *

Utatii au hutatii? Inapohusu kile ambacho Yehova anataka kutoka kwetu, kuna uamuzi mmoja tu wenye hekima. Kumtii kikamili na kwa hiari ndio uamuzi unaofaa. Kufanya hivyo kutafanya tuwe na uhusiano wa karibu zaidi na Yehova, Mungu mwenye upendo ambaye sikuzote anatutakia mema.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 1 Ingawa maneno ya Musa yaliwahusu Waisraeli wa kale, yanawahusu pia watu wote wanaotaka kumpendeza Mungu leo.—Waroma 15:4.

^ fu. 3 Katika kitabu chote cha Kumbukumbu la Torati, Musa anakazia kwamba kumwogopa Mungu kunapaswa kuongoza maisha ya watumishi wa Mungu.—Kumbukumbu la Torati 4:10; 6:13, 24; 8:6; 13:4; 31:12, 13.