Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Faraja Kwa Walioathiriwa na Mauaji Darasani

Faraja Kwa Walioathiriwa na Mauaji Darasani

Faraja Kwa Walioathiriwa na Mauaji Darasani

UKURASA wa kwanza wa gazeti ulikuwa na swali hili fupi peke yake: “Kwa Nini?” Hilo ndilo swali ambalo watu wengi walijiuliza tena na tena baada ya kijana mwenye umri wa miaka 17 kufyatua risasi huko Winnenden, Ujerumani kusini na kuwaua watu 15 na mwishowe kujiua mwenyewe. Kila mahali nchini Ujerumani bendera zilipeperushwa nusu mlingoti na habari za tukio hilo zilitangazwa ulimwenguni pote.

Winnenden ni mji mtulivu na wenye ufanisi uliozungukwa na mashamba ya mizabibu na ya matunda. Machi 11, 2009 (11/3/2009), ilianza kama asubuhi nyingine katika Shule ya Sekondari ya Albertville. Ghafula, saa 3:30 asubuhi, jeuri na vurugu zikaanza.

Kijana mmoja aliingia kwa fujo shuleni humo akiwa na bunduki aliyochukua kwenye chumba cha kulala cha wazazi wake. Mara moja, aliwaua wanafunzi tisa na walimu watatu waliokuwa ndani na nje ya madarasa matatu na akawajeruhi wengine. Baada ya dakika chache, polisi walifika. Kijana huyo alitoroka na kuingia kwenye eneo la kliniki ya watu wenye ugonjwa wa akili iliyokuwa karibu. Akiwa huko alimwua mfanyakazi mmoja. Kisha akamteka nyara mtu mmoja akiwa ndani ya gari lake. Mtu huyo alifaulu kutoroka baada ya umbali wa kilomita 40 hivi. Alipofika eneo moja la kuuzia magari, kijana huyo alimwua muuzaji pamoja na mteja wake na kuwajeruhi vibaya polisi wawili waliokuwa wakikaribia kumkamata. Mwishowe, polisi walipokuwa karibu kumkamata, alijipiga risasi kichwani.

Wale waliomfahamu kijana huyo walisema alikuwa kijana wa kawaida tu aliyetaka kukubalika na kuwa na marafiki. Kwa hiyo, mambo yaliharibikia wapi? Huenda alikuwa ameshuka moyo, naye alicheza na bunduki za kujifurahisha, na hata alicheza michezo fulani ya kompyuta yenye jeuri. Lakini watu fulani watapinga na kusema kwamba hata vijana wengine wengi hufanya hivyo pia. Namna gani wale aliowafyatulia risasi? Je, alikuwa amewachagua mapema, au alifyatua bila kuchagua? Watu walikuwa na maoni mbalimbali kwa nini aliwafyatulia risasi wasichana wanane na mvulana mmoja tu. Lakini hakuna aliyeweza kueleza kwa njia yenye kuridhisha.

Jinsi Watu Walivyotenda Haraka

Heike anasema hivi: “Mwana wetu alipopiga simu na kuniambia kwamba risasi zilikuwa zimefyatuliwa shuleni mwao, sikuamini. Lakini niliposikia magari mengi ya polisi na ambulansi zikipita kwa kasi nilishtuka sana.” Huenda kijana huyo hakuweza kuwaua watu wengi zaidi shuleni kwa sababu polisi walifika upesi. Baada ya watu wote kuondolewa katika majengo ya shule, wahudumu wa afya, washauri, na makasisi walifika na kuwashughulikia wanafunzi.

Waandishi wa habari walifika haraka kwenye shule hiyo na kujaribu kuwahoji wanafunzi ambao wengi wao walikuwa bado katika hali ya mshtuko. Mwanafunzi mmoja alihesabu magari 28 ya vituo 26 vya televisheni yakiwa yameegeshwa mbele ya shule hiyo. Vituo mbalimbali vya habari vilishindana kupata habari na hivyo kukawa na habari ambazo hazingeweza kuthibitishwa. Mwandishi mmoja wa habari alipigia simu familia ya msichana aliyeuawa siku hiyo akiomba picha, na waandishi wengine waliwalipa wanafunzi ili wawapige picha. Wakati wa vurugu hiyo, waandishi fulani wa habari walishindwa kuwa na usawaziko kati ya kuwa wa kwanza kupata habari na kuwaheshimu na kuwajali walioathiriwa.

Kama ilivyo katika visa kama hivi, watu hugeukia dini ili kupata faraja na majibu ya maswali yao. Siku mauaji hayo yalipotokea, ibada ya pamoja ya dini mbalimbali ilifanywa. Wengi walithamini jambo hilo. Lakini inahuzunisha kwamba wale waliokuwa wakitafuta kufarijiwa na Neno la Mungu au majibu ya maswali yao yaliyowatatanisha walikatishwa tamaa. Familia moja ilihudhuria mazishi ya msichana fulani aliyekuwa katika darasa moja na mwana wao. Mama ya mvulana huyo alisema hivi: “Askofu alizungumza kuhusu mateso ya Ayubu. Nilisubiri aeleze jambo tunalojifunza kutokana na hilo au atufariji, lakini wapi. Hakueleza kwa nini Ayubu aliteseka au matokeo yalikuwa nini.”

Mtu mmoja alikasirishwa sana na maneno matupu aliyosikia. Mwanamume huyo alikuwa amejifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova miaka 30 hivi iliyopita lakini akaacha kujifunza. Sasa alianza tena kuhudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova.

Valisa, msichana mwenye umri wa miaka 14 ambaye alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi, alikuwa katika darasa lililokuwa karibu na mahali ambapo mauaji yalitokea. Aliposikia milio ya risasi, alianza kusali kwa Yehova. Baadaye alipoulizwa jinsi alivyokuwa akikabiliana na hali hiyo, alisema kwamba matukio hayo yalithibitisha yale ambayo alikuwa amejifunza katika Biblia kuhusu siku hizi za mwisho zilizo hatari. (2 Timotheo 3:1-5) Mashahidi wawili walikuwa wakiwaambia majirani wao maneno yenye kufariji. Mwanamke mmoja mzee aliwakaribia na kuwaambia, “Watu wengi zaidi wanapaswa kufanya kile mnachofanya.” Mauaji hayo yenye kushtua na kuhuzunisha yalifanya watu wengi wasikilize ujumbe wenye kutoa tumaini na faraja kutoka katika Neno la Mungu.

Waathiriwa Bado Wanafadhaika

Bila shaka, hata maneno ya faraja ya kutoka moyoni hayawezi kuondoa mshtuko na mfadhaiko wa wale walioathiriwa moja kwa moja. Hakuna maneno yanayoweza kuondoa kabisa uchungu wa mzazi aliyempoteza mtoto wake au huzuni ya ofisa wa polisi aliyeenda haraka kwenye shule hiyo na kugundua kwamba mke wake alikuwa kati ya wale waliouawa.

Wanafunzi waliookoka msiba huo pamoja na familia zao walifadhaika sana, kila mmoja kwa njia tofauti. Kijana huyo alipoanza kufyatua risasi, Vassilios aliruka kupitia mlango wa dharura. “Niliporuka nje,” anakumbuka Vassilios, “nilisali kwa Yehova. Nilidhani ningekufa. Nilikuwa na hakika kwamba hiyo ilikuwa sala yangu ya mwisho.” Majuma yaliyofuata, alisumbuliwa na ndoto mbaya, na hakutaka kuzungumza na yeyote. Alikasirishwa na jinsi ambavyo vyombo vya habari vilishindana kuripoti kuhusu mauaji hayo, na jinsi waandishi wa habari walivyoingilia bila kujali faragha ya watu ili tu kupata habari. Baada ya muda, aliweza kutulia kihisia.

Jonas, ambaye alikuwa katika darasa moja na Vassilios, aliona wanadarasa wenzake watano wakiuawa. Anasema: “Mara tu baada ya tukio hilo, sikuwa na tatizo lolote kueleza kilichotokea; ilikuwa kama sinema yenye kuogopesha. Lakini sasa, ni vigumu sana kwangu kueleza jinsi ninavyohisi. Hisia zangu hubadilika-badilika. Nyakati nyingine sitaki kuzungumzia tukio hilo; nyakati nyingine nataka kulizungumzia sana.” Yeye pia hupata ndoto mbaya na ana matatizo ya kulala.

Baada ya siku kadhaa, wanafunzi walipewa vitu vyao kutoka kwenye madarasa yao. Wataalamu wanaoshughulika na watu waliohusika katika matukio yenye kutisha walionya kwamba kuona vitu hivyo kunaweza kuwafanya wakumbuke msiba uliowapata. Mwanzoni, Jonas hakutaka kugusa koti, mfuko, na kofia yake ya kujikinga anapoendesha pikipiki. Pia alishikwa na woga alipomwona mtu aliyefanana au aliyebeba mkoba kama wa kijana yule aliyefyatua risasi. Aliposikia mlio wa risasi katika sinema ambayo wazazi wake walikuwa wakitazama, alishikwa na wasiwasi sana. Wataalamu walijaribu kuwasaidia watu walioathiriwa wasihusianishe matukio ya kawaida na mkasa uliowapata.

Jürgen, baba ya Jonas, hufanya kazi katika kliniki ambapo mmoja wa wafanyakazi aliuawa. Alisema kwamba wazazi wengi na wafanyakazi wenzake walihangaika sana na kujiuliza kwa nini jambo hilo lilitukia na ingekuwaje ikiwa wao ndio wangepigwa risasi. Kwa mfano, mfanyakazi mmoja kwenye kliniki hiyo ambaye alimwona mwuaji huyo akipita alihangaika sana alipofikiria kwamba aliponea kidogo tu kupigwa risasi hivi kwamba alihitaji kutibiwa na daktari wa magonjwa ya akili.

Jinsi Wengine Walivyosaidiwa Kukabiliana na Hali

Wengine wamesaidiwa namna gani kukabiliana na tukio hilo lenye kutisha? Jürgen anasema: “Ni vizuri kuwa pamoja na wengine ingawa nyakati nyingine ni vigumu kufanya hivyo. Inafariji sana kujua kwamba wengine wanakujali na kwamba hujaachwa peke yako.”

Jonas pia anathamini kwamba wengine wanamjali. Anasema: “Wengi hunitumia kadi na ujumbe. Wengine wanataja mistari ya Biblia ambayo mimi husoma. Hilo ni jambo nzuri.” Ni jambo gani lingine linalomsaidia? “Nikiamka usiku na kuhisi kwamba siwezi kukabiliana na hali, mimi husali. Nyakati nyingine ninasikiliza muziki au kaseti za gazeti Amkeni!” * Anaendelea kusema kwamba Biblia inatueleza ni kwa nini mambo hayo yote yanatokea: Shetani anautawala ulimwengu, na tunaishi katika kipindi cha mwisho. Baba yake anasema kwamba kujua hivyo humsaidia Jonas kukabiliana na tukio hilo.

Mateso Yote Yatakwisha Hivi Karibuni

Siku chache tu baada ya tukio hilo, mishumaa, maua, na barua zilijaa mbele ya shule hiyo. Kerstin aliona kwamba watu kadhaa waliandika barua na kuuliza ni kwa nini mauaji hayo yalitokea na kwa nini Mungu aliruhusu jambo hilo. Alitambua kwamba maswali hayo yalihitaji kujibiwa, kwa hiyo yeye na Mashahidi wengine wawili waliandika barua na kuiweka mahali zile nyingine zilikuwa.

Wakati wa siku iliyowekwa rasmi ya kuwakumbuka waliouawa, kituo kimoja cha televisheni kilionyesha barua ya Kerstin na kunukuu mistari kadhaa ya kwanza: “Kwa nini? Katika siku za mwisho swali hilo limeulizwa mara nyingi, na hasa maswali kama vile: Mungu alikuwa wapi? Na kwa nini aliruhusu jambo hilo?” Kwa kusikitisha barua hiyo ilinukuliwa tu kufikia hapo.

Kwa nini ni jambo lenye kusikitisha? Kwa sababu barua hiyo iliendelea kueleza kwa nini tunateseka na kusema kwamba Mungu “atahakikisha kwamba mateso yote ambayo yamesababishwa na wanadamu yataondolewa.” Kisha ikaongezea hivi: “Katika kitabu cha mwisho cha Biblia, Mungu anasema kwamba atafuta kila chozi kutoka katika macho ya watu, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” Yehova Mungu atawafufua wafu. Chini ya Ufalme wake utakaokuja hivi karibuni, hakutakuwa tena na misiba, mauaji ya kikatili, au kuteseka. Mungu anaahidi: “Tazama! Ninafanya vitu vyote kuwa vipya.”—Ufunuo 21:4, 5.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 20 Gazeti Amkeni! ambalo pia limerekodiwa katika kaseti huchapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 12]

Jonas alipokea kadi inayosema, “Tunakufikiria”

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 9]

Focus Agency/WPN

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 9]

© imagebroker/Alamy

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 10]

Foto: picture alliance

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 11]

Foto: picture alliance