Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nililie Msaada Mpaka Wakati Gani?”

“Nililie Msaada Mpaka Wakati Gani?”

“Nililie Msaada Mpaka Wakati Gani?”

“Ninataka tu maumivu yangu yaishe!” akalia Jayne. Alikuwa na ugonjwa wa kansa uliokuwa umeenea mwilini mwake. Watu wa familia na marafiki walitamani sana kumwondolea ugonjwa huo na maumivu makali aliyokuwa nayo. Walimwomba Mungu amsaidie. Je, angesikiliza sala zao? Je, kweli alijali?

MUNGU anajua mambo ambayo familia ya kibinadamu inapitia. Neno lake Biblia, linasema: “Uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.” (Waroma 8:22) Mungu anajua kwamba kuna mamia ya mamilioni ya watu ambao, kama Jayne, wana maumivu kila siku, yawe ni maumivu ya kimwili, kihisia, au kiakili. Mungu anawaona watu milioni 800 ambao hulala njaa kila usiku, mamilioni wengine ambao hutendewa kwa jeuri nyumbani, na wazazi wengi ambao huwa na wasiwasi kuhusu wakati ujao na hali njema ya watoto wao. Je, umewahi kujiuliza ikiwa Mungu atachukua hatua kuondoa mambo hayo? Kwa kuwa sisi tunatamani kuwasaidia wapendwa wetu, je, Mungu hahisi hivyo pia kuihusu familia yake ya kibinadamu, ambayo ni uumbaji wake?

Si wewe tu ambaye umejiuliza maswali kama hayo. Zaidi ya miaka 2,600 iliyopita, mwanamume mwaminifu Habakuki alihisi kama watu wengi wanavyohisi leo, naye alimwuliza Mungu hivi: “Ee Yehova, nililie msaada mpaka wakati gani, nawe usisikie? Nitakuomba msaada kutokana na jeuri mpaka wakati gani, nawe usiokoe? Kwa nini unanionyesha jambo lenye kudhuru, nawe unaendelea kutazama taabu tupu? Na kwa nini kuna uporaji na jeuri mbele yangu, kwa nini kugombana hutokea, kwa nini mzozo huendelezwa?” (Habakuki 1:2, 3) Habakuki, ambaye alikuwa nabii Mwebrania, aliona mashambulizi na matendo ya jeuri yasiyo na sababu katika siku zake. Leo, matendo hayo yanayoonekana kwenye vyombo vya habari kila siku huwachukiza watu wenye huruma.

Je, Mungu alipuuza mahangaiko ya Habakuki? La. Alisikiliza maswali ambayo Habakuki aliuliza kwa unyoofu, kisha akamfariji na kumtia moyo mwanamume huyo aliyekuwa na huzuni. Yehova Mungu aliimarisha imani ya Habakuki kwa kumwahidi kwamba Yeye atakomesha kuteseka. Ujumbe wa Mungu wenye tumaini unaweza kukufariji wewe pia kama ulivyomfariji Jayne na familia yake. Habari inayofuata itajibu maswali haya: Tuna uhakika gani kwamba kweli Mungu anatujali? Mungu atafanya nini ili kukomesha kuteseka, na atafanya hivyo lini?