Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Dunia Itakwisha?

Je, Dunia Itakwisha?

Je, Dunia Itakwisha?

“MWISHO wa ulimwengu ni suala linalovutia sana, hasa katika utengenezaji wa sinema,” akasema mwandishi John Scalzi. Kwa nini watazamaji wanavutiwa sana na sinema kuhusu mwisho wa ulimwengu? “Kwa sababu zinaonyesha mambo ambayo tunaogopa,” akasema Scalzi. Je, unakubaliana naye? Je, tuna sababu nzuri za kuogopa kwamba wakati mmoja dunia na viumbe wote waliomo wataharibiwa kwa njia fulani?

Karibu kila siku tunasikia kuhusu misiba ya asili inayosababisha uharibifu mkubwa. Mambo yenye kuogopesha kuhusu uharibifu huo yanaonyeshwa tena na tena kwenye televisheni na kwenye Intaneti. Tunapotazama televisheni au Intaneti na kuona maeneo halisi na watu halisi wakiharibiwa, ni rahisi kufikiri kwamba mwisho wa ulimwengu ni tisho halisi, bali si jambo tunaloona tu kwenye sinema.

Wanasayansi wanafanya watu wawe na woga hata zaidi kwa makisio yao kuhusu jinsi ambavyo dunia itakwisha. Wengine hata wanatabiri wakati ambapo dunia itakwisha. Mnamo Machi (Mwezi wa 3) 2008, jarida fulani (Monthly Notices of the Royal Astronomical Society) lilisema kuwa wataalamu wawili wa nyota walitabiri kwamba katika muda wa miaka bilioni 7.59 hivi, jua litaimeza dunia yetu na kuifanya kuwa mvuke.

Je, dunia itakwisha siku moja?

Je, Dunia Yetu Itakwisha Siku Fulani?

Biblia inatuhakikishia hivi: “Kizazi chapita na kingine chaja, lakini dunia yadumu daima.” (Mhubiri 1:4, Biblia Habari Njema) Yehova Mungu “ameiwekea dunia msingi [imara] juu ya mahali pake” na alikusudia idumu “mpaka wakati usio na kipimo, au milele.” (Zaburi 104:5) Je, maneno hayo ya Mungu yanasikika kama ndoto tu? Kwa nini uamini kwamba dunia yetu haitakwisha, hali wanasayansi fulani wanadai kwamba itakwisha?

Fikiria bidhaa zilizo dukani. Bidhaa fulani zinaonyesha tarehe ya mwisho ambayo bidhaa inaweza kutumiwa. Ni nani aliyeweka tarehe hiyo? Je, mwenye duka alitegemea ujuzi wake kukisia tarehe hiyo, kisha akaiweka kwenye bidhaa? Hapana. Mtengenezaji wa bidhaa ndiye aliyeamua tarehe ya mwisho ambayo bidhaa fulani inaweza kutumiwa. Tunaamini tarehe hiyo kwa sababu mtengenezaji wa bidhaa anazijua vizuri zaidi kuliko mtu mwingine yeyote. Hivyo basi, tunapaswa kumwamini hata zaidi Mtengenezaji wa dunia yetu! Neno lake linasema waziwazi kwamba ‘ameiweka dunia imara’ ili idumu milele. Hakuna tarehe iliyowekwa ambapo dunia itakwisha!—Zaburi 119:90.

Hata hivyo, je, inawezekana wanadamu wasiojali waiharibu dunia kabisa? Hapana! Tofauti na wanadamu wanaotengeneza bidhaa, Yehova ‘anaweza kufanya mambo yote.’ (Ayubu 42:2) Hiyo ndiyo sababu anaweza kusema hivi kwa uhakika kabisa: “Neno langu linalotoka katika kinywa changu . . . hakika litafanikiwa.” (Isaya 55:11) Tunaweza kuwa na hakika kwamba “Mtengenezaji wetu” hataruhusu chochote kimzuie asitimize kusudi lake kuhusu dunia. (Zaburi 95:6) Kusudi hilo ni nini, na Mungu atalitimiza jinsi gani?

Ufalme wa Mungu Utatimiza Kusudi Lake

Zaidi ya kutuhakikishia kwamba dunia haitakwisha, Neno la Mungu pia linatuambia kuwa “aliiumba ili ikaliwe na watu.” (Isaya 45:18) Ingawa dunia yetu imekaliwa kwa maelfu ya miaka, kusudi la Mungu kuihusu halijatimia bado.

Yehova ni “Mungu mwenye furaha” na “mpenda-haki.” (1 Timotheo 1:11; Zaburi 37:28) Kusudi lake ni kwamba wanadamu wote waishi kwa furaha, bila kutendwa isivyo haki. Ili kutimiza kusudi lake, Mungu alitabiri kwamba atasimamisha Ufalme mbinguni ambao utaitawala dunia yote. (Danieli 2:44) Alipokuwa duniani, Yesu alizungumza mara nyingi kuhusu Ufalme au utawala wa Mungu. Aliwatia moyo wanafunzi wake waombe Ufalme huo uje kwa sababu alijua baraka nyingi ambazo watakaoishi duniani watafurahia chini ya utawala huo. (Mathayo 6:9, 10; 24:14) Ona baadhi ya baraka hizo.

Kutakuwa na amani na usalama kwa sababu Mungu anaahidi kukomesha vita vyote.—Zaburi 46:9.

Kutakuwa na chakula cha kutosha kwa wote.—Zaburi 72:16.

Matatizo ya afya hayatakuwapo kwa sababu “hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24.

Watu hawataomboleza kwa kuwa “kifo hakitakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.

Mungu anaahidi kwamba watu wake watajenga nyumba zao wenyewe, wataishi kwa usalama, na ‘kuwa na shangwe milele.’—Isaya 65:17-24.

Bila shaka, unatamani kufurahia hali hizo ambazo zimetajwa. Yehova anatamani sana kutimiza mambo yote ambayo ametabiri. (Isaya 9:6, 7) Lakini huenda ukauliza: ‘Maelfu ya miaka imepita tangu ahadi za Mungu ziandikwe katika Biblia, mbona hazijatimia?’

Subira ya Mungu Inaleta Wokovu

Uwe na hakika kwamba “Yehova hakawii kuhusiana na ahadi yake.” Biblia inasema kwamba Mungu ametutendea kwa upendo na subira. Kwa hiyo, tunatiwa moyo kuiona “subira ya Bwana wetu kuwa wokovu.” (2 Petro 3:9, 15) Lakini kwa nini subira ya Mungu ni muhimu ili kupata wokovu?

Kwanza kabisa, Mungu anajua kuwa kabla ya kuwaandalia wanadamu waadilifu makao salama na mazuri, lazima ‘awaharibu wale wanaoiharibu dunia.’ (Ufunuo 11:18) Hata hivyo, kwa sababu anawapenda wanadamu, Yehova “hataki yeyote aangamizwe.” Kwa subira Baba yetu wa mbinguni amekuwa akijaribu “kumwonya mwovu aiache njia yake ya uovu.” Kwa hiyo, Yehova ameagiza ujumbe kuhusu Ufalme wake uhubiriwe duniani kote. * (Ezekieli 3:17, 18) Wote wanaosikiliza onyo hilo la Mungu na kutenda kulingana na kanuni zake za uadilifu, watapata wokovu na kufurahia uzima wa milele katika dunia paradiso.

Mgeukie Mungu Upate Kuokolewa

Hapana shaka kwamba Biblia ina “habari njema” kwa ajili yetu. (Mathayo 24:14) Inatupa ahadi ya Mungu isiyoweza kukosa kutimia kwamba dunia yetu haitakwisha! Isitoshe, kulingana na unabii wa Biblia, tunaweza kuwa na imani kwamba “bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena.” Hivi karibuni, ni wale tu walio waadilifu machoni pa Mungu ‘watakaoimiliki dunia, na kupata furaha yao tele katika wingi wa amani.’ (Zaburi 37:9-11, 29; Mathayo 5:5; Ufunuo 21:3, 4) Hadi wakati huo, Mungu ataendelea kuwaita watu kwa subira: “Geukeni mje kwangu mkaokolewe, ninyi nyote mlio katika miisho ya dunia.” (Isaya 45:22) Wewe utaitikiaje?

Tunakutia moyo uazimie kumgeukia Mungu. Andiko la Zaburi 37:34 linatuhimiza: “Mtumaini Yehova na kuishika njia yake, naye atakuinua uimiliki dunia.” Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kujifunza mengi kuhusu kusudi la milele la Mungu kuihusu dunia na jinsi unavyoweza kuishi uone kusudi hilo likitimia.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 21 Kwa kutii amri ya Yesu kwenye Mathayo 28:19, 20, Mashahidi wa Yehova zaidi ya milioni saba katika nchi 236, wanatumia muda wa saa bilioni moja na nusu kila mwaka kufundisha watu juu ya kusudi zuri la Mungu kuhusu dunia hii.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 22]

NASA photo