Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wafu Wanaweza Kuwasaidia Walio Hai?

Je, Wafu Wanaweza Kuwasaidia Walio Hai?

Je, Wafu Wanaweza Kuwasaidia Walio Hai?

TAMBA, mwanamume kijana anayeishi Afrika Magharibi, alikuwa karibu kufanya mtihani shuleni. * Mama yake alisisitiza kwamba anahitaji msaada wa watu wa familia yao waliokufa ili afaulu. Huko Palermo, Sicily, watalii huwa wanatembelea maeneo ya makaburi yaliyo chini ya ardhi ambapo wanaweza kuona maiti nyingi zilizohifadhiwa vizuri ili zisiharibike. Watu fulani wanafikiri kwamba maiti hizo zinawalinda walio hai. Kila mwaka, watu hutembelea mji wa Lily Dale, ulio magharibi mwa Jimbo la New York, Marekani. Mji huo una watu wengi isivyo kawaida ambao wanawasiliana na pepo. Watu wanatembelea mji huo wakitumaini kwamba wanaweza kuwasiliana na watu wa familia zao au marafiki waliokufa ili wawasaidie.

Watu wengi duniani bado wanaamini kwamba wafu wanaweza kuwasaidia walio hai. Una maoni gani? Labda umefundishwa jambo hilo au baadhi ya marafiki wako wanaamini jambo hilo. Ni kawaida kutamani kuwasiliana na wapendwa wetu waliokufa. Watu wanaowasiliana na pepo wanadai kwamba jambo hilo linawezekana. Mwanamke mmoja anayewasiliana na pepo aliliambia gazeti la Time kwamba pepo “wako tayari kumsaidia mtu wakati wowote wanapoombwa kufanya hivyo.” Je, hilo ni kweli? Je, wafu wanaweza kwa kweli kuwasaidia walio hai? Huenda jibu la wazi la Biblia likakushangaza.

Je, Wafu Wako Hai Mahali Fulani?

Biblia inaeleza hali ya wafu kwa njia rahisi na yenye kueleweka. Ona andiko la Mhubiri 9:5 linavyosema: “Walio hai wanajua kwamba watakufa; lakini wafu, hawajui lolote kamwe.” Je, wafu wanaweza kuhisi chochote? Mstari wa 6 unajibu: “Upendo wao na chuki yao na wivu wao tayari zimepotea, na mpaka wakati usio na kipimo hawana fungu lolote tena katika chochote ambacho kitafanywa chini ya jua.” Ona pia kwamba mstari wa 10 wa sura hiyohiyo unasema kuwa “hakuna kazi, wala utungaji wala ujuzi wala hekima katika Kaburi, mahali unapokwenda.” Katika andiko hili, neno Kaburi ni tafsiri ya neno la Kiebrania “Sheoli.” Ona vilevile kwamba neno la Kigiriki “Hadesi” linalotumiwa katika Maandiko kuonyesha mahali ambapo Yesu Kristo alikaa kwa muda baada ya kifo chake, lina maana sawa na neno la Kiebrania “Sheoli” au Kaburi.—Matendo 2:31.

Yesu aliwasaidia watu wengi alipokuwa hai, lakini alijua kwamba ingekuwa lazima afe. Je, alitarajia kwamba angeweza kuendelea kuwasaidia hata akiwa kaburini? Hapana. Alilinganisha kifo chake kilichokuwa kikikaribia na wakati wa usiku ambapo kazi haingeweza kufanywa. (Yohana 9:4) Yesu alijua vizuri kwamba wanadamu wanapokufa, wanakuwa “wasiojiweza katika kifo.”—Isaya 26:14.

Yesu alitumia pia mfano kufafanua hali ya kifo. Rafiki yake Lazaro alipokufa, Yesu alilinganisha kifo na usingizi. (Yohana 11:11-13) Hatutazamii mtu ambaye amelala usingizi atusaidie, sivyo? Mtu ambaye amelala hajui lolote na hawezi kumsaidia yeyote.

Je, Nafsi Inaendelea Kuishi Baada ya Kifo?

Watu wengi wamefundishwa kwamba nafsi ni kitu fulani kisichoonekana ambacho kinaendelea kuishi baada ya mtu kufa. Biblia inafundisha jambo lililo tofauti. Kitabu cha kwanza cha Biblia kinatueleza nafsi ni nini. Andiko la Mwanzo 2:7 linasema kwamba mtu wa kwanza alipoumbwa, yeye alikuwa “nafsi hai.” Mtu mwenyewe ni nafsi na wanyama pia ni nafsi. (Mwanzo 1:20-25) Kwa hiyo, ni jambo linalopatana na akili kusema kwamba, mtu au mnyama anapokufa, nafsi inakufa. Biblia inathibitisha jambo hilo.—Ezekieli 18:4, Zaire Swahili Bible.

Hata hivyo, huenda watu fulani wakauliza, ‘Mbona kuna hadithi nyingi kuwahusu watu waliowasiliana na wafu na kusikia sauti zao, na hata kuwaona?’ Kuna hadithi nyingi kama hizo ulimwenguni. Hadithi hizo zinawapa matumaini watu waliofiwa au marafiki wa aliyekufa, na kuwasukuma wengi watafute watu wanaowasiliana na pepo ambao wanadai wanaweza kuzungumza na wafu.

Je, hadithi hizo ni za kweli? Kama ni za kweli, je, hazipingani na Maandiko ambayo yametajwa? Kristo Yesu alisema Neno la Mungu ni kweli. (Yohana 17:17) Kweli haijipingi. Katika Biblia, tuna mwongozo ulio wazi kuhusu jinsi tunavyopaswa kuyaona madai kwamba wafu wanaweza kuwasaidia walio hai. Biblia inatueleza kuhusu mtu fulani aliyejaribu kupata msaada kutoka kwa wafu. Ukisoma simulizi hilo kwa makini, utaelewa ukweli wa mambo.

Mfalme Aomba Msaada Kutoka kwa Wafu

Mfalme Sauli na majeshi yake walikuwa vitani kaskazini mwa Israeli. Walikabili jeshi lenye kuogopesha la Wafilisti. Sauli alipoona majeshi ya Wafilisti, “akaogopa, na moyo wake ukaanza kutetemeka sana.” Wakati huo, Sauli alikuwa ameacha ibada ya kweli. Kwa sababu hiyo, Yehova hakumjibu sala zake. Sauli angefanya nini ili apate msaada? Samweli, nabii wa Mungu, alikuwa amekufa.—1 Samweli 28:3, 5, 6.

Sauli alitafuta mwongozo kutoka kwa mwanamke aliyewasiliana na pepo huko En-dori. Alimsihi mwanamke huyo “nipandishie Samweli” kutoka kwa wafu. Mwanamke huyo alitokeza mzuka. “Samweli” huyo aliyetokea alimwambia Sauli kuwa Wafilisti wangeshinda na kwamba Sauli na wanawe wangekufa vitani. (1 Samweli 28:7-19) Je, kwa kweli huyo alikuwa Samweli aliyerudi kutoka kwa wafu?

Fikiria jambo hili. Biblia inasema kwamba mtu anapokufa ‘anarudi kwenye udongo wake’ na kwamba “mawazo yake hupotea.” (Zaburi 146:4) Sauli na Samweli walijua kwamba Mungu anawashutumu watu wanaowasiliana na pepo. Hapo awali, Sauli alikuwa amewaongoza Waisraeli kukomesha nchini mazoea ya kuwasiliana na pepo!—Mambo ya Walawi 19:31.

Fikiria kisa hicho kwa makini. Kama Samweli mwaminifu alikuwa bado hai akiwa kiumbe wa roho, je, angevunja sheria ya Mungu na kushirikiana na mwanamke mwenye kuwasiliana na pepo ili azungumze na Sauli? Yehova alikuwa amekataa kuzungumza na Sauli. Je, mwanamke huyo angemlazimisha Mungu Mweza-Yote azungumze na Sauli kupitia Samweli aliyekufa? Hapana. Bila shaka, “Samweli” huyu hakuwa kwa vyovyote yule nabii mwaminifu wa Mungu. Alikuwa kiumbe wa roho—roho mwovu aliyejifanya kuwa Samweli.

Mashetani ni malaika ambao waliasi mamlaka ya Mungu mapema katika historia ya wanadamu. (Mwanzo 6:1-4; Yuda 6) Mashetani hawa wanaweza kuwatazama watu walio hai. Kwa hiyo wanajua jinsi mtu alivyozungumza, alivyotenda, na sura yake alipokuwa hai. Wanataka kuendeleza maoni kwamba Biblia inasema uwongo. Si ajabu Biblia inatuonya tusiwe na mawasiliano yoyote na roho kama hao! (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Mashetani hao bado wanatenda kazi leo.

Sasa tunaweza kuelewa ni kwa nini wengi wanasema kwamba “wamewaona” wapendwa wao waliokufa au “kusikia” sauti yao. Ingawa wafu hao wanapotokea kama mizuka wanaweza kuonekana kuwa na nia nzuri, kumbuka kwamba roho waovu wameazimia kuwadanganya watu. * (Waefeso 6:12) Pia, fikiria hili: Yehova ni Mungu mwenye upendo anayetujali. Ikiwa wafu wako hai mahali fulani na wanaweza kuwasaidia marafiki na watu wa familia yao, je, Muumba wetu mwenye upendo angetukataza tusiwasiliane nao na kusema kwamba hilo ni jambo lenye “kuchukiza”? Hapana! (1 Petro 5:7) Hivyo basi, je, kuna chanzo cha msaada chenye kutegemeka?

Msaada wa Kweli kwa Walio Hai na Waliokufa

Tunaelewa kutokana na mambo yaliyozungumziwa kwamba wafu hawana uwezo wowote wa kuwasaidia walio hai. Zaidi ya hayo, jitihada za kutafuta msaada kutoka kwa wafu ni mbaya, ni bure, na ni hatari sana, kwa kuwa zinavunja sheria ya Mungu na zinafanya tuathiriwe na mashetani.

Biblia inatuelekeza kwa Yehova Muumba wetu anayeweza kutusaidia na hata kutukomboa kutoka katika kifo chenyewe. (Zaburi 33:19, 20) Leo pia Yehova anatusaidia kwa kutupa tumaini hakika ambalo ni tofauti na tumaini bandia linalotolewa na watu wanaowasiliana na pepo.

Tamba, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, alijionea tofauti kati ya matumaini bandia yanayotolewa na watu wanaowasiliana na pepo, na ukweli ambao Yehova anatufunza. Watu hao walidai kwamba asipowatolea dhabihu mababu zake waliokufa, ataanguka mtihani. Tamba alikuwa akijifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Alijua hali halisi ya wafu na pia kwamba mashetani wanajifanya kuwa mababu waliokufa. Ijapokuwa mama yake alimshinikiza atafute msaada wa watu wanaowasiliana na pepo, Tamba alikataa na kumwambia, “Nikianguka mtihani, nitajitahidi zaidi mwaka ujao.”

Matokeo yalikuwa nini? Tamba alipata maksi ya juu kushinda wote! Mama yake alishangaa, na akaacha kuwaamini watu wanaowasiliana na pepo. Hakutaja dhabihu za aina hiyo tena. Tamba alijua kuwa Yehova anatuonya tusitoe ‘maombi kwa watu waliokufa kwa ajili ya watu walio hai.’ (Isaya 8:19) Kwa kujifunza Biblia, Tamba alikuwa na uhakika kwamba angefanikiwa kama angependezwa na sheria ya Yehova.—Zaburi 1:1-3.

Namna gani wapendwa wetu waliokufa? Je, wana tumaini lolote? Yehova anatusaidia sisi tulio hai na pia ameahidi kuwasaidia walio makaburini. Baada ya kueleza kwamba wafu hawana uwezo wowote, ona maneno ya nabii Isaya katika sura ya 26, mstari 19: “Wafu wako wataishi. . . . Amkeni, pigeni vigelegele kwa shangwe, enyi mnaokaa mavumbini!” Unabii huo unaendelea kusema kwamba “wale wasiojiweza katika kifo” wataishi tena.

Wazia jambo hilo! Mabilioni ya watu wasiojiweza ambao wanalala makaburini watafufuliwa! Biblia inafunua kwamba Yehova ‘anatamani sana’ kuwafufua wafu. (Ayubu 14:14, 15) Je, ahadi hizo zinasikika kama ndoto tu? Yesu Kristo alikuwa na hakika sana kuhusu tumaini la ufufuo hivi kwamba alisema wafu wako hai machoni pa Yehova.—Luka 20:37, 38.

Je, ungependa kuwa na tumaini hilo? * Endelea kujifunza Biblia. Unapoendelea kujifunza utasadikishwa kwamba Yehova anaweza kuwasaidia walio hai na waliokufa, na kuwa ahadi zake ni za ‘uaminifu na za kweli.’—Ufunuo 21:4, 5.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Jina limebadilishwa.

^ fu. 18 Kwa habari zaidi kuhusu jambo hili, ona broshua Roho za Wafu—Je! Zaweza Kukusaidia au Kukuumiza? Je! Ziko Kweli? iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 26 Kwa habari zaidi kuhusu ahadi ya Biblia ya ufufuo, ona sura ya 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Ni kawaida kutamani kuwasiliana na wapendwa wetu waliokufa

[Picha katika ukurasa wa 20]

Je, nabii Samweli alirudi kutoka kwa wafu na kuzungumza na Mfalme Sauli?