Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Mungu Aliwaamuru Waisraeli Wapigane Vita na Wakanaani?

Kwa Nini Mungu Aliwaamuru Waisraeli Wapigane Vita na Wakanaani?

Kwa Nini Mungu Aliwaamuru Waisraeli Wapigane Vita na Wakanaani?

“Mtawaangamiza watu wote: Wahiti, Waamori, Wakanaani, Waperizi, Wahivi na Wayebusi kama Mwenyezi-Mungu, Mungu wenu, alivyoamuru.”—KUMBUKUMBU LA TORATI 20:17, BIBLIA HABARI NJEMA.

“Iweni wenye kufanya amani na watu wote.”—WAROMA 12:18.

JE, MAANDIKO hayo ya Biblia yanapingana? Watu wengi hawaelewi kwa nini Mungu aliamuru Wakanaani waangamizwe, hali Biblia inawaagiza watu wawe wenye kufanya amani. * (Isaya 2:4; 2 Wakorintho 13:11) Wanaona maagizo hayo kuwa yanapingana.

Kama ungeweza kuzungumzia suala hili pamoja na Mungu, ungemuuliza nini? Ona maswali matano ambayo watu wengi wanauliza na jinsi Biblia inavyoyajibu.

1. kwa nini Wakanaani waliondolewa nchini Kanaani? Inaweza kusemwa kwamba Wakanaani walikuwa wakaaji wa nchi ambayo haikuwa yao. Kwa nini? Miaka 400 hivi mapema, Mungu alikuwa amemwahidi Abrahamu mwaminifu kwamba wazao wake wangemiliki nchi ya Kanaani. (Mwanzo 15:18) Mungu alitimiza ahadi hiyo alipowasaidia Waisraeli, ambao ni wazao wa Abrahamu, kumiliki nchi hiyo. Huenda watu fulani wakadai kwamba Wakanaani tayari walikuwa wakiishi nchini humo na hivyo walikuwa na haki ya kuimiliki. Lakini, bila shaka Mungu Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote, ndiye aliye na haki ya kuamua ni wapi ambapo watu wataishi.—Matendo 17:26; 1 Wakorintho 10:26.

2. kwa nini Mungu hakuwaruhusu Wakanaani waishi pamoja na Waisraeli? Mungu alitoa onyo hili kuwahusu Wakanaani: “Wasikae katika nchi yako, wasije wakakufanya unitendee dhambi. Ikiwa utaitumikia miungu yao, itakuwa mtego kwako.” (Kutoka 23:33) Nabii Musa aliwaambia Waisraeli hivi baadaye: “Yehova anayafukuzia mbali mataifa haya kutoka mbele yako kwa sababu ya uovu wao.” (Kumbukumbu la Torati 9:5) Uovu wa mataifa hayo ulikuwa mwingi kadiri gani?

Wakanaani wengi waliabudu miungu ya kipagani, waliwadhabihu watoto wao, na maadili yao yalikuwa mapotovu. Henry H. Halley, mwanahistoria mmoja wa Biblia anasema kwamba wataalamu wa vitu vya kale waliochimbua eneo la Kanaani “walipata mitungi mingi sana iliyojaa maiti za watoto waliokuwa wametolewa dhabihu kwa Baali [mungu maarufu wa Wakanaani].” Yeye anaongeza: “Eneo lote lilikuwa makaburi ya vitoto vichanga. . . . Wakanaani waliabudu, kwa kujiingiza katika uasherati, ukiwa sherehe ya kidini, mbele ya miungu yao; kisha wakawaua watoto wao wa kwanza, na kuwatoa dhabihu kwa miungu hiyohiyo. Yaonekana kwamba, kwa kiwango kikubwa, nchi yote ya Kanaani ilikuwa kama Sodoma na Gomora. . . . Waakiolojia wanaochimbua magofu ya majiji ya Kanaani hushangaa ni kwa nini Mungu hakuwaharibu mapema zaidi ya alivyofanya.”

3. Je, hakukuwa na watu wengine waovu duniani wakati huo? kwa nini ni Wakanaani tu walioharibiwa? Mara nyingi, Mungu ameamua kuwaharibu waovu fulani na kuwaacha wengine. ‘Dunia ilipojaa jeuri’ wakati wa Noa, Mungu alileta Gharika na watu wote wakafa isipokuwa familia ya Noa. (Mwanzo 6:11; 2 Petro 2:5) Mungu aliharibu majiji ya Sodoma na Gomora, dhambi ya wakaaji wake ilipokuwa “nzito” sana. (Mwanzo 18:20; 2 Petro 2:6) Pia alitangaza hukumu juu ya jiji la Ashuru la Ninawi, lililoitwa “jiji la umwagaji wa damu,” ingawa hakutekeleza hukumu hiyo Waninawi walipotubu na kuacha njia zao mbaya. (Nahumu 3:1; Yona 1:1, 2; 3:2, 5-10) Mungu aliwaharibu Wakanaani ili kulilinda taifa la Israeli, ambalo mwishowe lingetokeza Masihi.—Zaburi 132:11, 12.

4. Je, kuharibiwa kwa Wakanaani kunapingana na upendo wa Mungu? Huenda kijuujuu tendo la Mungu la kuwaangamiza Wakanaani likaonekana kuwa linapingana na upendo wake. (1 Yohana 4:8) Lakini tunapolichunguza kwa makini tunaona kwamba hilo ni tendo la upendo.

Mungu alijua zamani kwamba matendo ya Wakanaani yalikuwa mapotovu. Lakini badala ya kuwaharibu mara moja, alingoja kwa subira kwa muda wa miaka 400, hadi dhambi yao ‘ikawa kamili.’—Mwanzo 15:16.

Dhambi ya Wakanaani ilipofikia hatua ambapo hakukuwa na tumaini lolote kwamba wangebadilika, Yehova aliwaangamiza. Hata hivyo, hakuwaangamiza Wakanaani wote. Kwa nini? Kwa sababu baadhi yao walikuwa tayari kubadilika. Wale waliokuwa tayari kubadilika kama vile Rahabu na Wagibeoni, walionyeshwa rehema.—Yoshua 9:3-11, 16-27; Waebrania 11:31.

5. Ni nini kinachoweza kufanya Mungu wa upendo amharibu mwanadamu yeyote? Hilo ni swali zuri kwa sababu wazo la kumwangamiza mtu si jambo lenye kupendeza. Hata hivyo, Mungu alisukumwa na upendo kuwaharibu waovu. Kwa mfano: Mkono au mguu wa mtu unapoanza kuoza kwa sababu ya jeraha au kidonda, mara nyingi madaktari wanalazimika kuukata. Ni madaktari wachache ambao wangefurahia kufanya hivyo, lakini daktari mzuri anajua kwamba asipoukata, hali itakuwa mbaya zaidi. Hivyo, kwa sababu daktari anamjali mgonjwa, anamkata mkono au mguu ili aokoe maisha yake.

Vivyo hivyo, Yehova hakufurahia kuwaharibu Wakanaani. Yeye mwenyewe anasema: “Sikifurahii kifo cha mtu mwovu.” (Ezekieli 33:11, BHN) Wakati huohuo, aliamua Masihi azaliwe katika taifa la Israeli. Masihi angewafungulia njia ya kupata wokovu wote walio na imani. (Yohana 3:16) Hivyo, Mungu hangeweza kuruhusu Waisraeli wachafuliwe na desturi zenye kuchukiza za Wakanaani. Kwa hiyo, aliamua Wakanaani waharibiwe au wafukuzwe katika nchi ya Kanaani. Kwa kufanya hivyo, Mungu alionyesha upendo mkubwa, ambao ulimsukuma kufanya jambo lisilopendeza kwa faida ya waabudu wake waaminifu.

Jinsi Tunavyofaidika

Je, leo tunaweza kufaidika kutokana na masimulizi ya kuharibiwa kwa Wakanaani? Ndiyo, kwa kuwa andiko la Waroma 15:4 linasema: “Mambo yote yaliyoandikwa zamani yaliandikwa ili kutufundisha sisi, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tuwe na tumaini.” Mambo yaliyotukia Kanaani yanaweza kutufundisha na kutupa tumaini jinsi gani?

Masimulizi hayo yanatufundisha mambo mengi. Kwa mfano, Rahabu na Wagibeoni walimtegemea Mungu kwa imani, naye akawahurumia na kuwaokoa. Jambo hilo linatukumbusha kwamba yeyote ambaye kwa kweli anataka kumfurahisha Mungu, anaweza kufanya hivyo, hata awe wa malezi gani au alifanya dhambi gani wakati uliopita.—Matendo 17:30.

Masimulizi kuhusu kuharibiwa kwa Wakanaani pia yanatupa tumaini kwa kuonyesha kimbele hatua ambayo Mungu atachukua hivi karibuni. Yanatuhakikishia kwamba Mungu hataruhusu uovu umeze wema kabisa. Badala yake, Biblia inatuhakikishia kwamba hivi karibuni Mungu atachukua hatua ya kuwaharibu waovu wote, na kuwaokoa wanaompenda ili waishi katika ulimwengu mpya wenye uadilifu. (2 Petro 2:9; Ufunuo 21:3, 4) Wakati huo, maneno haya yenye kufariji yatatimizwa: “Mtumaini Yehova na kuishika njia yake, naye atakuinua uimiliki dunia. Watu waovu watakapokatiliwa mbali, wewe utaona hilo.”—Zaburi 37:34.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Katika makala hii, neno “Wakanaani” linarejelea mataifa yote ambayo Mungu aliwaagiza Waisraeli wayaondoe katika nchi ya Kanaani.

[Sanduku katika ukurasa wa 14]

Maoni ya Biblia Kuhusu Vita vya Wanadamu

Je, amri ya Mungu kwa Waisraeli ya kuwaharibu Wakanaani, inamaanisha kwamba vita vya wanadamu vinakubalika leo? Hapana, kwa sababu ya angalau mambo matatu:

Hakuna taifa lolote duniani leo ambalo lina uhusiano wa pekee pamoja Mungu. Waisraeli walipomkataa Yesu akiwa Masihi, waliacha kumwakilisha Mungu katika njia yoyote ile—hata kutekeleza hukumu zake. (Mathayo 21:42, 43) Kwa hiyo, Yehova anawaona Waisraeli kuwa sawa na mataifa mengine. (Mambo ya Walawi 18:24-28) Tangu wakati huo, hakuna taifa lolote duniani linaloweza kusema kwamba Mungu analiunga mkono katika vita.

Yehova hawapi tena waabudu wake nchi au eneo fulani la kukaa. Badala yake, watumishi wake wanaweza kupatikana katika ‘mataifa na makabila yote’ ya dunia.—Ufunuo 7:9; Matendo 10:34, 35.

Yesu alionyesha wazi kwamba wafuasi wake hawangeshiriki katika vita. Alipotoa onyo kuhusu uharibifu wa Yerusalemu uliokuwa ukikaribia, Yesu aliwaagiza wanafunzi wake wasibaki humo na kupigana, bali wakimbie, nao wakafanya hivyo. (Mathayo 24:15, 16) Badala ya kwenda vitani, Wakristo wa kweli wanautumaini kabisa Ufalme wa Mungu, ambao hivi karibuni utaondoa uovu wote duniani.—Danieli 2:44; Yohana 18:36.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kisa cha Rahabu kinaonyesha kwamba yeyote ambaye kwa kweli anataka kumpendeza Mungu, anaweza kufanya hivyo