Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Mungu Anaahidi Kuwapa Watu Zawadi ya Uzima wa Milele?

Kwa Nini Mungu Anaahidi Kuwapa Watu Zawadi ya Uzima wa Milele?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Kwa Nini Mungu Anaahidi Kuwapa Watu Zawadi ya Uzima wa Milele?

▪ Biblia inasema kwamba Mungu ametupa nafasi ya kupata “uzima wa milele.” (Yohana 6:40) Ni nini kinachomsukuma afanye hivyo? Je, anataka tu kutenda haki?

Kutenda haki kunahusisha kuwatendea watu kulingana na mambo yanayofaa na yaliyo sawa. Je, kweli sisi tunastahili kupewa uzima? Hapana. Biblia inasema: “Hakuna mwanadamu aliye mwadilifu duniani ambaye huendelea kufanya mema na asifanye dhambi.” (Mhubiri 7:20) Anayetenda dhambi anaadhibiwa. Mungu alimwonya mtu wa kwanza, Adamu, kwamba siku ile ambayo angefanya dhambi angekufa hakika. (Mwanzo 2:17) Baadaye, mtume Paulo aliongozwa na roho ya Mungu kuandika: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Kwa hiyo, ikiwa kwa haki wazao wote wa Adamu wanastahili kufa, kwa nini Mungu anatupa nafasi ya kupata uzima wa milele?

Nafasi ya kupata uzima wa milele ambayo Mungu anatupa ni “zawadi ya bure.” Inaonyesha kwamba Mungu ana upendo mwingi na fadhili nyingi sana zisizostahiliwa. Biblia inasema: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu, nayo ni zawadi ya bure kwamba wanatangazwa kuwa waadilifu kwa fadhili zake zisizostahiliwa kupitia kuachiliwa huru kwa njia ya fidia ambayo Kristo Yesu alilipa.”—Waroma 3:23, 24.

Ingawa sote tunastahili kufa, Mungu ameamua kuwapa uzima wa milele wale wanaompenda. Je, anatenda isivyo haki? Biblia inasema: “Basi, tuseme nini? Je, Mungu ana ukosefu wa haki? Isiwe hivyo kamwe! Kwa maana yeye anamwambia Musa: ‘Nitamwonyesha rehema yeyote ninayetaka kumwonyesha rehema, nami nitamwonyesha huruma yeyote ninayetaka kumwonyesha huruma.’ . . . Kwa kweli wewe ni nani ndipo uthubutu kumjibu Mungu?”—Waroma 9:14-20.

Katika maeneo fulani ulimwenguni, mkuu wa serikali au hakimu anaweza kumsamehe mhalifu aliyefungwa kwa muda mrefu. Ikiwa mhalifu anakubali adhabu anayopewa na anabadili mtazamo na mwenendo wake, hakimu au rais anaweza kuamua kumsamehe kwa kupunguza kifungo chake au kumsamehe kabisa. Katika hali kama hiyo, mfungwa anaonyeshwa fadhili, kwa kuwa anapaswa kukamilisha kifungo chake.

Vivyo hivyo, Yehova anaweza kuamua asiwaadhibu watenda dhambi wote wanaostahili kuadhibiwa. Badala yake, kwa kusukumwa na upendo, anaweza kuwapa uzima wa milele wale wanaompenda na wanaofuata kanuni zake. Biblia inasema: “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.”—Matendo 10:34, 35.

Yehova alionyesha upendo usio na kifani alipomtuma Mwana wake kuja kuteseka na kufa kwa ajili yetu. Yesu alisema hivi kumhusu Baba yake: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

Wote wanaokuja kumpenda Yehova na kufanya mapenzi yake wanakubalika kwake, hata wawe wa malezi gani. Kwa hiyo, tumaini la kupata uzima wa milele ni wonyesho hasa wa upendo wa Mungu usio na kifani na fadhili ambazo hatustahili kuonyeshwa.

[Blabu katika ukurasa wa 29]

Uzima wa milele ni wonyesho hasa wa upendo wa Mungu usio na kifani na fadhili ambazo hatustahili kuonyeshwa